Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kwa kunipa nafasi awali ya yote nichukuwe nafasi hii kwa falsafa ile ile kwamba mnyonge mnyongeni lakini haki mpatieni. Niipongeze sana Wizara ya Maji kwa kazi nzuri inayofanyika, nikupongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa timu yako yote kwa kazi nzuri inayofanyika kwenye sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, lakini pia niwapongeze kwa kazi ambayo kwa kweli mnaifanya kwa uvumilivu mkubwa mara zote nikikufuata wizarani unanipa nafasi ya kunisikiliza na tunajadiliana majadiliano ambayo kwa kweli yanaonyesha dira kwamba wana Hanang wanaenda kupata maji maeneo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukuwe nafasi hii kushukuru kwa bajeti hii kuonyesha maeneo ambayo kwa kweli yalikuwa na matatizo ya maji muda mrefu, kwamba mmetutengea fedha za utafiti wa kupata vyanzo vya maji kijiji cha Mberu, Diloda, Bassodesh, Sasemwega, Mwanga, Lalaji, Wakhama, Masaqa, na ukichukua eneo la Mberu kipindi kirefu wananchi wanaamka saa tisa wanarudi nyumbani saa sita mchana shughuli zingine zote zinasimama wanafuata maji.

Mheshimiwa Spika, lakini zaidi sana mradi wa maji Gehandu eneo lile lilikuwa na changamoto ya muda mrefu tulijadiliana kwa kina na Mheshimiwa Waziri, kisima kimeshachimbwa usanifu umefanyika, lakini kwenye maandiko hapa naona unakwenda Gehandu Ming’enyi na Mugucha nilishaongea na wataalamu kwamba ule mradi kwasababu maji ni mengi tutanuwe kidogo uwende Milongori, uende kijiji cha Gidabwanja, uwende kwenye kitongoji cha Mwanina na kitongoji Marega kwasababu ni maeneo yako karibu na kwenye mteremko ni rahisi kupeleka maji.

Mheshimiwa Spika, lakini pia pale Lalaji tumejenga shule ya sekondari ya kisasa sana na tuna kituo kizuri cha afya na mmeweka angalau mpango wa kupeleka maji na eneo lile halikuwa na maji muda mrefu sana eneo hili nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuangalia na pia tuna mpango huo wa kutanua mtandao wa maji kwenye Kata za Dirima, Lalaji, Mberu pamoja na Hideti. Ni kazi kumbwa naamini kwamba maeneo haya kidogo yatajaribu kupunguza changamoto ya maji ambayo tulikuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na juhudi zote zinazofanyika ninaomba Mheshimiwa Waziri eneo la usimamizi wa utekelezaji wa miradi ili eneo liangaliwe kwa ukaribu, kuna wakati nilishawahi kusema hapa Bungeni tafadhali wasongelee karibu wataalamu wako ili angalau watekeleze miradi hii kwa ufanishi, jana baadhi ya Wabunge walichangia kwamba miradi mingi inatekelezwa kwa njia ya force account, ni wazo nzuri kama tuna rasilimali watu ya kutosha na naamini kwamba ni njia ambayo iko tuseme inathamani ya fedha kwa kazi kutekelezwa tuangalie je, kweli tunao huo uwezo je, hatucheleweshi miradi kwa kufuata hiyo njia lakini pia tuangalie tukiwatumia wakandarasi kwa njia ambazo zimeshauriwa, kwamba wakandarasi wengine inawezekana hawana mitaji tuangalie namna ya ku-manage ili tuhakikishe kwamba miradi inatekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, lakini pia jinsi tunavyozisimamia mamlaka zetu za maji sitaki sana niwe mlalamishi kwenye eneo hilo, lakini kwenye maandiko ya wizara umesema kwa kiwango kikubwa maendeleo ya jamii yoyote inategemea uwepo wa maji ya kutosha na yenye ubora unaotakiwa. Sasa ukiangalia mji wetu wa Kateshi pale umejengwa mradi wa maji wa bilioni 2.5, mradi ule hauleti tija yoyote kwasababu mradi umekamilika kwa maana na umekabidhiwa kwa mamlaka ya maji, lakini uendeshwaji wa Mamlaka ya Maji kwa kipindi kirefu hakuna board, ukifuatilia ni board ni kazi ya mtu mmoja.

Mheshimiwa Spika, naomba zile mamlaka zisimamiwe vizuri lakini pale ambapo hakuna ufanisi, zile mamlaka wakati mwingine zinatuongezea gharama ukiangalia Dar es Salaam na Pwani inasimamiwa na DAWASA na gharama za maji ni nafuu. Huku kwetu unit inaenda mpaka 2,500 tuangalie eneo hili la mamlaka za maji zinaleta gharama kubwa kwa watumiaji wa mwisho. Ninaomba sana eneo hili lisimamiwe vizuri ili kuhakikisha kwamba tunapata tija ambayo tunaitarajia.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kumalizia miradi ya maji jaribu kuongea ndani ya Serikali na watu wa Nishati ili pale ambapo kisima kinaenda kuchimbwa nao umeme uende ili maji yanapopatikana maji yale yaweze kusambazwa kwa watu ili yaweze kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya machache ninashukuru ninaunga mkono hoja ahsante sana.