Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa tena nafasi nzuri ya pekee niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, napenda nimshukuru Waziri, Mheshimiwa Jumaa Aweso, nilifanya naye ziara kwenye Jimbo langu siku saba zilizopita kutokana na swali ambalo nililiuliza hapa siku hiyo alikuwepo Naibu Waziri wa Maji dada yangu Mheshimiwa Maryprisca Mahundi. Nina furaha kubwa kwa niaba ya wananchi wangu wa Mbogwe, kwanza baada ya kumuona Waziri wa Maji anafika kwa wakati muafaka na akanipa ahadi nyingi ikiwemo gari kwa ajili ya wananchi wa Mbogwe kwa maana ya Meneja wa Maji wa Mbogwe. Cha kusema kikubwa mimi niwaombe tu Wabuge wenzangu leo nisingependa hata nione mtu hata mmoja anashikilia shilingi maana huyu Waziri ni mwaminifu sijawahi kuona Waziri mwaminifu namna hii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Rais wetu, Mama yetu kwa ziara zile anazoendelea nazo huko nje. Sisi kama Wabunge tunampa support asilimia mia moja. Tukio lililotupata mwaka huu lilikuwa kubwa sana na mataifa yalitegemea kuona sisi tunaanguka lakini kwa uwezo na nguvu za Mungu mpaka sasa hivi tunajadili bajeti na mipango yetu kama watu wenye akili timamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, nitumie nafasi hii kushauri, Katiba inasema mimi ni mtunga sheria lakini vilevile nimshauri wa Serikali. Pamoja na pongezi zote kwako Mheshimiwa Waziri nikutie moyo, kuna watu wengi kweli unaenda unawaelimisha pengine walikuwa hawajui majukumu yao, ikiwemo watendaji wako wale wa chini kwenye halmashauri huko wilayani, kuwapa maelekezo mazuri ili kusudi wawe karibu na wananchi na wananchi kiukweli wanaimani kubwa sana na awamu hii. Kwa hiyo, kwa vile umeniahidi mimi vitu vingi na mimi nikuahidi tu, kwanza miradi ile mikubwa ikianza kukamilika pale kwenye Jimbo langu nitaandika jina lako Jumaa Aweso ukumbukwe hata kama siku umekufa kwamba palikuwa na Waziri Awamu ya Sita alikuwa anaitwa Jumaa Aweso. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine sasa hivi mimi naishi hapa Dodoma kwa nguvu za wananchi wa Mbogwe. Nipende tu kumsaidia Mbunge wa hapa Dodoma haipendezi sana tupo Makao Makuu halafu tunakuwa hatuna maji, nyumba zetu tunajenga tunaweka ma-simtank, kwa kuwa wewe ni Waziri wa nchi nzima ukimaliza basi kwenye majimbo yetu yale ya Kanda ya Ziwa ufanye juu chini kama unavyofanya ili na Dodoma hapa tupate maji hayo ya mradi mkubwa wa Ziwa Victoria. Maana maji yetu kule ni mazuri halafu huku tunatumia maji yenye chumvi. Sura yangu mimi nilikuwa mzuri sana sikuwa na sura ya hivi, ninarudi nyumbani tena nikiwa na sura nyingine. Kwa maana hiyo nikuombe ndugu yangu Mheshimiwa Mavunde tusaidiane tu kuwa tunamkumbusha Waziri wetu ili na hapa tuweze kuupata huo mradi mkubwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi kwa vile natoka Geita, sasa tuna wilaya tano, mwenzangu amezungumza pale, ni vyema wilaya zetu ambazo zipo karibu na Ziwa Viktoria zipewe huo mradi wa maji mkubwa ili kusudi wananchi wa kule waweze kufaidika na maji yao ya Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niwaombe tu hata Wabunge wenzangu, nina imani kuna Wabunge wengine baada ya kuchaguliwa hawarudi majimboni kutazama shida za wananchi, tusije tukapata tena kazi ngumu 2025 kukawa na jimbo halina maji tena tukaanza tena kampeni zile za kutumia nguvu sana. Maana wananchi tuliwaahidi kwamba watakuwa na maisha mazuri, tutawapa huduma za maji pamoja na mambo mengine lukuki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe Wabunge wenzangu tuwe tunamkumbusha Mheshimiwa Jumaa Oweso ni mtu mzuri sana na atatusaidia tu na nina imani naye maana nimeona kwa vitendo, kuna bilioni karibia 50 mradi mmoja ambao ulikuwa unaenda Katoro, alimpongeza hadharani Engineer mmoja jina nimeshalisahau, kuna dogo mmoja hivi ni Engineer pale Geita alisema ameokoa bilioni karibia arobaini kitu. Kwa maana hiyo, wewe brother ni muaminifu na ungekuwa na tamaa kama watu wengine siwezi kuwataja hapa, wanaomtumikia shetani ina maana hizo ungepiga kimya tu na wala hakuna mtu angekusumbua, kama ni kesi ina maana ingeendelea mbele kwa mbele. Brother wewe ni muaminifu endelea kuwa na imani hiyo na Mungu atakusaidia mambo mengi na siku zako zitakuwa nyingi sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nikupongeze wewe mimi leo nina miezi sita hapa Bungeni, nilikuwa kiukweli sijui kabisa kuongea mbele ya watu wakubwa kama nyie hivi, wakiwemo Mawaziri ambao nilikuwa nawaona tu kwenye screen wakina Prof. Palamagamba Kabudi lakini sasa hivi kwa vile tunaonana vizuri sana. Niwaombe Mawaziri muige mfano kwake huyu Waziri Jumaa Aweso kwenye Wizara zenu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana toka tuanze kuchangia bajeti hapa kila mtu aliyeleta bajeti yake tunaipitisha, ni vyema sasa unapoipokea ile bajeti yako uwe na kumbukumbu kwamba nilipitishiwa bilioni 60 zimefanya kazi hivi hivi. Mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge tupate siku moja kuja kuwahoji hawa Mawaziri kwamba tulipitisha bajeti mwaka 2020 zilienda wapi? Kwa mawazo hayo tutaenda vizuri na wananchi wetu waliopo kijijini kuliko tu kila kitu tutasema ndiyo, ndiyo halafu vitu vyenyewe vinakuwa havifanyiki huko majimboni na vijijini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, wale watumishi wa Mungu mmenielewa lakini wale wenye roho mbaya na dhamira mbaya message sent mjipange. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)