Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia katika hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu, kwanza kipekee kuipongeza Wizara, Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso; Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Mhandisi Maryprisca Mahundi na watendaji wote wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu, Eng. Sanga na mwanamama machachari Naibu Katibu Mkuu, Eng. Nadhifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tuseme kwenye Wizara hii kazi kubwa imefanyika. Serikali imefanya kazi kubwa ya kufanya utambazaji wa maji kwenye nchi yetu. Na wote mmesikia kwenye hotuba kwamba malengo ya kusambaza maji vijijini kwa asilimia 85 kufikia 2025 mpaka kufikia mwezi Machi tayari asilimia 72.3 maji yamesambazwa. Lakini malengo ya kusambaza maji mijini tumefikia asilimia 84; tunaipongeza sana Wizara ya Maji kwa kazi kubwa waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee niipongeze Serikali, zaidi ya shilingi bilioni 200 zimewekezwa katika kazi ya kusambaza maji safi na salama kwenye Mkoa wa Dar es Salaam. Lakini iko miradi mingi mikubwa; upo ule mradi wa Arusha, zaidi ya shilingi bilioni 520; upo Mradi mkubwa wa Tabora – Igunga – Nzega, zaidi ya bilioni 600; lakini iko miradi ile ya miji 28 ya zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 500, kazi kubwa sana imefanyika kwenye sekta ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye wanufaikaji wa miradi hii na Jimbo la Ukonga ni wanufaikaji. Sisi kwa miaka yote tulikuwa tukipata maji toka Ruvu chini, maji ambayo yalikuwa mpaka yapite katikati ya Jiji la Dar es Salaam yapandishe Mlima wa Magereza – pale Magereza kulikuwa na mashine ya maji – yaje mpaka Gongo la Mboto – pale Gongo la Mboto kulikuwa na mashine ya maji, na mtafahamu Jimbo la Ukonga lina asili ya Milima ya Pugu mpaka Milima ya Kisarawe kwa kaka yangu, Mheshimiwa Selemani Jafo. Na kwa kipindi kirefu tokea miaka tisini hatukuwahi kupata maji safi na salama ya bomba. Katika uwekezaji huu wa Serikali, Mradi wa Maji wa Ruvu Juu na Ruvu Chini imeboreshwa na uzalishaji umeongezeka kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maji haya yalipofika Kibamba ukabuniwa mradi mwingine ukatoa maji Kibamba mpaka Kisarawe na Kisarawe imejengwa njia ya maji mpaka Pugu limejengwa tanki kubwa la lita milioni mbili na tayari mradi ule umezinduliwa, na hivi ninavyozungumza Jimbo la Ukonga linapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa shukrani kwa niaba ya wananchi wa Ukonga, Mheshimiwa Waziri alifika, alikuja na Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais kuzindua mradi ule; tunawashukuru sana. Na DAWASA kupitia Mhandisi Cyprian Lwemeja, wanafanya kazi kubwa ya kuendelea kusambaza maji yale kwa uwezo wao wa ndani. Tayari kazi ya transmission imekamilika na hivi wmaeshapata fedha wanaanza kazi ya distribution. Sisi tunaamini katika malengo ya 2025 tutakuwa wa kwanza kuyafikia kabla ya wakati na maji yatasambaa kwenye Jimbo la Ukonga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri, mpaka kufikia mwezi huu Aprili, fedha za maendeleo zilizopokelewa ni asilimia 54.1. Katika fedha zilizopangwa za Mwaka wa Fedha 2020/2021 mpaka kufikia mwezi huu wa Aprili ni asilimia 54.1 tu ndiyo zimepokelewa na Wizara. Imebaki miezi miwili, siamini kwamba kufikia mwisho wa bajeti hii Wizara ya Maji itakuwa imepata fedha zote za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Wizara hii isipopata fedha maana yake maombi yote uliyoyasikia hapa Waheshimiwa Wabunge wakiyaomba, miradi yote ambayo umeisikia inaendelea kwenye majimbo yote ndani ya Bunge hili haitakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wenzetu wa Wizara ya Maji ni waombaji kama sisi tunavyoomba, inapokuja hapa bajeti kuu ya Serikali naomba tusimame tuseme Wizara hii ipatiwe fedha za kutosha. Pia isipatiwe tu fedha kwa maana ya kuzitenga kwenye bajeti lakini na fedha zenyewe zipelekwe tena kwa wakati ili miradi ya kuwasambazia maji Watanzania iweze kufanyika kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie pia ama kuongezea pale alipochangia Mheshimiwa Anne Kilango Malechela, miradi ya maji hasa vijijini ukiondoa hii ya mijini ambayo inasimamiwa na Mamlaka ni kweli inagharimu fedha nyingi. Niungane na mama yangu Mheshimiwa Anne Kilango, Wizara ya Maji, RUWASA, Menejimenti ya RUWASA na DG yupo hapa nadhani anasikia, Clement anafanya kazi nzuri kujenga taasisi hii mpya na changa iliyoanzishwa muda mfupi uliopita, mjitahidi mtengeneze mfumo utakaofanya wale akina Ali Mabomba waliokuwa Same waweze kupatikana kusimamia miradi hii nchi nzima. Itakuwa ni kichekesho kutengeneza miradi ya thamani kubwa ya mabilioni ya shilingi lakini kuiacha kwenye mikono ya watu ambao hawana utaalamu, lakini hawana usimamizi wa kitaalamu chini ya taasisi yetu hii ya RUWASA.Ni vyema tukajipange na hili litawezekana kama Wizara hii itakuwa na fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiendelea kusisitiza RUWASA kutengeneza utaratibu wa kuwa na wataalam wa kutosha kusimamia miradi lakini nitaendelea kuliomba Bunge lako na tutakutana tena hapa kwenye bajeti kuu ya Serikali kuendelea kuitaka na kuishauri Serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maji ili utendaji huu uliotukuka tunaouona wa Waziri wetu Mheshimiwa Jumaa Aweso uweze kwenda kwa vitendo akiwa na fedha za kulipa makandarasi wanaofanya kazi kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi hii, naunga mkono hoja. (Makofi)