Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maji, Mkoa wa Songwe pia umekuwa ni miongoni mwa mikoa ambayo imekumbwa na changamoto kubwa sana ya maji. Mkoa wa Songwe ni mkoa wenye kata 94 lakini kati ya kata zote hizo hakuna kata ambayo ina uhakika wa kupata maji. Hivyo changamoto hiyo imepelekea wananchi wa Mkoa wa Songwe kutumia muda wao mwingi sana kuhakikisha wanapambana kutatua changamoto ya maji kwenye maeneo yao.

Mheshimia Naibu Spika, naamini kabisa changamoto hii ya maji ikiweza kutatuliwa itaweza kuepusha migogoro mingi ya ndoa ambayo inatokea pasipo sababu za msingi. Pia changamoto hii ikitatuliwa endapo tutaweza kuondoa migogoro ya ndani ya ndoa tutaepusha pia changamoto kubwa ya watoto wa mitaani ambao ni zao kubwa la migogoro ya ndoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba utekelezaji wa miradi ya maji umekuwa na changamoto kubwa sana na utekelezaji huu bajeti yake imekuwa ikitekelezwa kwa kiwango kisichoridhisha sana.

Mheshimiwa Naibu Spika,katika mwaka wa fedha wa 2016/2017, fedha ambazo zilikuwa zimetengwa katika utekelezaji wa bajeti ya maendeleo katika miradi ya maji ni bilioni 913.83, lakini fedha ambayo ilikuwa imetolewa ilikuwa ni bilioni 230.99 tu. Jambo hilo lilisababisha utekelezaji wa miradi ya maji kutekelezwa kwa asilimia 25 tu na kutotekelezwa kwa asilimia 75, jambo ambalo pia linawakwamisha sana wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2017/2018, Wizara ilitengewa bilioni 623.6, lakini fedha ambazo zilikuwa zimetolewa zilikuwa ni bilioni 135.19, ambapo miradi iliweza kutekelezwa kwa asilimia 22 tu, hivyo tuliweza kufeli kwa asilimia 78, miradi ya maendeleo ya maji haikuweza kutekelezwa kwa asilimia 78 jambo ambalo tulifeli.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2018/2019, bajeti iliweza kutekelezwa kwa asilimia 15 tu na kwa mwaka 2019/2020, bajeti iliweza kutekelezwa kwa asilimia 61, lakini kwa mwaka 2021 bajeti iliweza kutekelezwa kwa asilimia 40. Jambo hili linatupelekea kukwama sana kwa miradi ya maendeleo kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto hiyo ya bajeti ndogo, kumekuwa na changamoto kubwa pia ambayo inapelekea kufeli sana hasa kwenye visima ambavyo tunachimba. Changamoto hiyo inasababishwa na upungufu wa wataalam wa kufanya tafiti kwenye maeneo yetu ili kujua ni wapi maji yanaweza kupatikana; kuna maeneo tumechimba visima maji hayajapatikana kabisa, hivyo ikapelekea kuonekana kama fedha tunatupa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa ripoti ya CAG, inaonyesha wazi kabisa kwamba kati ya visima 10,485 visima vilivyochimbwa visima 490 havikuweza kuwa na maji. Pia CAG alibaini wazi kwamba, kati ya fedha bilioni 768 zilizopelekwa kwa ajili ya uchimbaji wa visima ambazo pia baada ya visima hivyo kuchimbwa, visima hivyo havikuweza kuwa na maji, maana yake tukapelekea kuonekana kwamba tumetupa karibu ya kiasi cha Shilingi bilioni 764.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hizi zinasababishwa na kutokuwa na watafiti wa kutosha katika maeneo yetu. Hivyo naishauri Serikali, tuna sababu kubwa ya kuwa na wataalam wengi wa kufanya tafiti kabla ya kuchimba visima vya maji ili Serikali tusiweze kuingia hasara. Tukifanya hivyo naamini tutaweza kufanikiwa katika suala zima la maji katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto kubwa ambayo pia imebainishwa na CAG, suala zima la madai ya Wakala wa Usambazaji wa Maji na Usafi wa Mazingira (RUWASA), imebaini kuwa karibu kiasi cha bilioni 12 wanaidai Serikali. Ili tuweze kufanikiwa katika miradi ya maji, tulipe haya madeni ambayo tunadaiwa na RUWASA ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi na kwa moyo kabisa. Tukifanya hivi naamini tutaweza kupunguza changamoto kubwa ya maji ambayo imekuwa ikiwakabili wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote naomba nizungumze wazi, nimesema hapo awali wananchi wa Mkoa wa Songwe ni wahanga wakubwa wa suala zima la maji safi na salama. Jambo hili limekuwa likipelekea wananchi wetu kuugua typhoid mara kwa mara kwa sababu maji wanayoyapata sio safi na salama, lakini bado hawapati maji ya kutosha maana yake hayohayo yasiyo na salama bado sio ya kutosha kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake atuambie ni lini atatekeleza mradi wa maji kutoka Ileje ili uweze kuwakomboa wananchi wa Mkoa wa Songwe, waweze kuondokana na changamoto kubwa ambayo imekuwa ikiwakabili katika kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)