Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti ya Wizara ya Maji. Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, aliyetujalia uzima na ametuwezesha kuendelea kuwepo ndani humu na kuendelea kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa nimpongeze sana ndugu yangu Waziri wa Maji, Mheshimiwa Jumaa Aweso kwa kuwa Waziri wa Maji, lakini pia kwa kazi kubwa wanayoifanya yeye na wataalam wake wote kwenye Wizara ya Maji. Wanafanya kazi kubwa sana, nami ni muumini wa kumpongeza mtu anapofanya vizuri. Wanafanaya kazi kubwa na nzuri, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bajeti hii ya mwaka huu, nitumie nafasi hii kutoa ushauri kwenye baadhi ya maeneo machache. Pamoja na kazi nzuri wanayoifanya kwenye Wizara ya Maji na Taasisi zao zote, tumeanzisha RUWASA, RUWASA inafanya kazi nzuri na ni moja ya chombo ambacho kinakwenda kuwakomboa sana watu wetu hasa sisi watu wa vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maboresho machache ninayoshauri tuyafanye kwa upande wa RUWASA ili iendelee kufanya kazi zake vizuri. Eneo la kwanza Mheshimiwa Waziri, nilisema mwaka jana na leo narudia tena. Tuiimarishieni RUWASA kwa kuweka Bodi za Manunuzi, hata kama hatuwezi kwenye Wilaya lakini basi tuwe na Bodi za Manunuzi za RUWASA kwenye mikoa yote. Haiwezekani RUWASA Mkoa wa Tanga kwa mfano, manunuzi wakitaka kufanya mpaka tutegemee Bodi ya Manunuzi ya TANGA - UWASA, ambayo ina majukumu yake, ina mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi tunachelewa na miradi yetu inachelewa kutekelezwa kwa sababu ya kutokuwa na Bodi za Manunuzi. Kila mkoa kwenye Ofisi za RUWASA tupate Bodi ya Manunuzi, kuwe na Mtaalam wa Manunuzi ili manunuzi yafanywe na RUWASA wenyewe tusitegemee Mamlaka nyingine hizi za maji. Huo ni ushauri wangu kwenye eneo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili Mheshimiwa Waziri, sehemu kubwa ya kazi za maji tunafanya kwa kutumia force account, tunatumia wale watu wetu tunaita local-fundi. Hao mafundi wanaofanya kazi ni mafundi wa chini kabisa ambao hawana mitaji mikubwa na hata miradi wanayopewa ni miradi midogo, tuziboreshe na Ofisi za RUWASA kwenye ngazi ya Wilaya. Waweke Wahasibu pale, haiwezekani fundi wa mradi wa milioni 15 anayelipwa labour charge, aki-raise kabarua kake ka kuomba alipwe milioni tatu atoke Lushoto, atoke Mlalo aende Tanga Mjini kwenda kufuata malipo yake ya fedha, haiwezekani. Nawaomba tuziboreshe hizi Ofisi za Wilaya, kuwe na Wahasibu na Wataalam pale ili waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Bodi za Watumia Maji, kama tumeweza kwenye Serikali kuajiri wataalam wa kilimo karibu kwenye kila kata, tunashindwaje kuwa na Mtaalam wa Maji kwenye kila kata ambaye ameajiriwa na Serikali. Sehemu kubwa tunatumia mafundi wale local ambao tunao wanashirikiana na wananchi wenyewe. Naiomba Wizara wafikirie kuajiri watu wa kwenda kufanya kazi za maji kwenye kata zetu, tuwe na Mtaalam wa Wizara, tuwe na Mtaalam wa Serikali aliyeajiriwa na anayelipwa ili kuwa na ufanisi mzuri wa kutekeleza majukumu yao kwenye yale maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ninalotaka kushauri kwa ujumla ni kwenye eneo la Sera ya Maji. Maisha yanabadilika na yanakwenda kasi sana, maendeleo yetu yanakwenda kwa speed kubwa, Sera yetu ya Maji inatwambia kufikisha maji mita 400, nadhani tunapoelekea tunapaswa tuangalie kufikisha maji kwenye nyumba za Watanzania. Miji yetu inakuwa kwa kasi, vijiji vinakuwa kwa kasi, kuna haja ya kuingalia vizuri Sera hii ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ushauri huo wa jumla, niende hasa kwenye mambo ambayo yanawagusa Wanakorogwe. Tunao mradi wa Mwanga – Same – Korogwe, mradi huu umechelewa sana na Mheshimiw;a Waziri ni shahidi. Nimpongeze kwa hatua alizochukua za kuvunja mkataba wa Mkandarasi na kutafuta namna nyingine ya kufanya ile kazi. Pamoja na hilo lakini bado speed ya kazi ile siyo nzuri sana na hairidhishi. Ninachotaka tu Mheshimiwa Waziri akija kuhitimisha atuhakikishie kwamba ni kweli huu muda aliotuambia kwamba mradi utakamilika ni kweli utakamalika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mradi kukamilika kwake ndiyo kuwapa maji wananchi wa Jimbo la Korogwe Vijijini hasa Kata za Mkomazi na Mkumbara ambao ndiyo wapo mwishoni mwa mradi huu. Mradi huu umechelewa kwa muda mrefu, tulitamani sisi tupate maji kutoka hata kwenye Mto Pangani au Mto Ruvu ambao unapita pale Mkomazi, lakini kila tukijaribu kutoa hayo mawazo tunaambiwa haiwezekani kwa sababu kutakuwa na double allocation of resources.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa watuambie kama huu mradi bado sana na kama hakuna uhakika na muda huu, waturuhusu na watutafutie fedha tuchukue maji kutoka kwenye mito tuliyokuwa nayo, ipo mito mingi na maji mengi ya kutosha, tupeleke maji kwa watu wa Mkomazi na watu wa Mkumbara kuliko kusubiri mradi huu mpaka muda ambao haujaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumzia Miradi ya Miji 28 na moja kati ya maeneo ambayo Waziri amesema yanakwenda kunufaika na mradi huu ni eneo la Mji wa Korogwe ambalo ni Jimbo la Korogwe Mjini. Mheshimiwa Waziri anajua kwa sababu tulifanya ziara naye, chanzo cha maji cha mradi huu kupeleka maji Korogwe Mjini na kupeleka Handeni, kupeleka na Muheza na Pangani kinatoka pale Korogwe, kwenye Kata ya Mswaha eneo ambalo vijiji vyake vyote havijapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachomwomba Mheshimiwa Waziri atuhakikishie watu wa Korogwe, tulishaomba kuwa sehemu ya mradi huo, sasa wanapochukua maji kuwapelekea Korogwe Mjini, Muheza na Handeni, hivi vijiji hivi wasivisahau. Kama Mheshimiwa Waziri anavyosema kwamba anapowadhuru wengine asitupite, basi wasiwapite wale wananchi. Tumesema muda mrefu lakini hatujajua kama walitukubalia, walituingiza kwenye mpango au hawajatuingiza. Kwa kuwa tunabmatumaini mradi unakwenda kutekelezwa sasa, tunaomba Waziri atupe ahadi na uhakika wa Serikali kuwa wananchi hawa watanufaika na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna bwawa ambalo nimeshawahi kumwambia Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara, Bwawa la Mayuyu ambalo linapatikana kwenye kule Kata ya Kerenge. Bwawa hili lilikuwa likitoa huduma ya maji kwa wananchi wetu, liliharibiwa na mafuriko, wakatuahidi kwamba wanatafuta fedha na kuna wakati wakasema wamepata fedha kutoka kwa wenzetu wa Misri, lakini mpaka leo bado kupo kimya. Namwomba Mheshimiwa Waziri anapokuja kwenye majumuisho atuambie tu ili tujue lini wananchi wa Kerenge na watu wa Mayuyu wanakwenda kupata ile huduma ya bwawa ili kurudisha huduma ya maji na kuendeleza shughuli za kiuchumi kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema nimeangalia bajeti ya Waziri vizuri na nimeisoma nimeona kwenye ukurasa 219 mpaka 220 ametenga fedha kwa ajili ya Vijiji vya Wilaya ya Korogwe kupata maji. Tunayo miradi ya kutosha pale, tunayo miradi mingi, lakini sehemu kubwa fedha hizi ni fedha za kuanzia na ni fedha ambazo hazitoshelezi na ceiling tuliyopewa ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Wizara ya Maji, lakini pia Serikali, ipo haja ya kuangalia namna ya kuongeza bajeti ya maji ili miradi hii iweze kukamilika. Tunamwomba Waziri atusaidie hilo ili wananchi wetu waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nakushukuru sana. (Makofi)