Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kuchangia katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, mimi ni mmoja kati ya Wajumbe wa Kamati hii. Nitakayoyazungumza ndiyo ambayo tumekutana nayo na ndiyo yaliyopo. Mheshimiwa Waziri hotuba yake ni nzuri sana ukiisoma, lakini uhalisia uliomo humu haumo, kwa sababu ukienda kule uraiani, kule kwenye viwanda kuangalia uhalisia, haupo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeingia ubia na viwanda tofauti tofauti, lakini Serikali haiangalii hivi viwanda vinafanyaje majukumu yake na mwisho wa siku tunajikuta kila siku tunapoteza mapato, kila siku tutapoteza wawekezaji kwa kudhani kwamba tunaweza kufanya miujiza hii nchi iendelee kuwa ya viwanda, hakuna! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya nchi hii inatakiwa kwanza ilinde viwanda tulivyonavyo. Kabla hatujasema tunakwenda kutengeneza viwanda vingine ama kuanzisha viwanda vingine, vilindwe hivi vichache vilivyopo ambavyo vinazalisha kwa chini ya asilimia 50. Viwanda vinazalisha chini ya asilimia 50, leo tunafikiria tutengeneze viwanda vingine eti Tanzania iende kuwa nchi ya viwanda, wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vipo, lakini wafanyabiashara wenye viwanda wana matatizo mengi kweli kweli! Naishauri Serikali, Mheshimiwa Waziri, narudia tena, waendelee kukaa na wafanyabiashara wenye viwanda, wasikilizeni hoja zao, matatizo yao ili hawa basi, waliopo hapa leo waweze kuwa mabalozi wa wawekezaji wengine ambao tunawategemea waje hapa. Hatuwezi kutegemea kuleta wawekezaji wengine, wakati hawa waliopo wana matatizo lukuki ambayo yanawakabili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima kwanza tutoe haya tuliyonayo hapa, tuyarekebishe, hawa wafanyabiashara leo watakuwa mabalozi wa kwenda kututangaza vizuri nchi ya Tanzania ili iweze kuwa nchi ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa, tumekwenda kama Kamati kwenye Kiwanda cha TANALEC, tumekuta transformer zaidi ya 2000 zinatengenezwa zinakwenda Kenya. Tanzania tunaagiza transformer kutoka India, transformer 200, Mkoa wa Katavi zimelipuka baada ya kuwashwa tu! Halafu TANESCO wanawaomba TANALEC wawatengenezee zile transformer ambapo TANALEC wamegoma! Nasi tukawaambia, haiwezekani, wapeleke huko huko walikonunua transfomer hizo zitengenezwe ndiyo wazirudishe hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hili suala wanasema sijui Sheria ya Manunuzi; sidhani kama Sheria ni Msahafu! Sheria zinabadilika! Hebu Waheshimiwa Wabunge tusaidiane basi kuangalia hizi sheria wapi ni mbaya, wapi zinatatiza ili wafanyabiashara waweze kufanya biashara zao wakiwa huru, wasifungwe na hizi sheria ambazo zinawatatiza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kiwanda cha Nondo Tanzania, wanazalisha nondo nyingi kweli kweli, lakini hawana masoko! Miradi ya Serikali inakuja mikubwa mikubwa, nondo zinaagizwa kutoka nje! Tunafanya nini? Tunasema nchi ya viwanda, viwanda gani kama hivi vilivyopo havifanyiwi kazi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku kwenye viwanda watu wanaondoa wafanyakazi kwa sababu hakuna biashara! Hawa vijana waende wapi? Matokeo yake ndiyo tunakabwa kila kukicha kwa sababu vijana hawana ajira na ajira nyingi tunategemea zitoke kwenye viwanda, leo viwanda vinafungwa, hawa vijana waende wapi? Akinamama waende wapi? Hizi panya-road zitakwisha lini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, kama kweli Serikali ina dhamira ya dhati ya kutaka nchi hii iwe ni nchi ya viwanda, iende kwenye huo mfumo ambao mnasema ni wa kati, yaani watu wetu wawe na maisha ya kawaida, basi ni lazima tuboreshe viwanda nyetu vya ndani ili viwanda hivi vikifanya vizuri wawekezaji watakuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nikiiangalia bajeti hii ya Serikali, TIC (Tanzania Investment Center) hawana bajeti zaidi ya mshahara. Wanafanyaje majukumu yao? Wataletaje hao wawekezaji? TBS, mamlaka nzito, kubwa inafanya kazi kubwa; ukiangalia, hawana fedha zaidi ya mshahara. Tunafanyaje mambo haya ndugu zangu? Tutafika kweli?
Mheshimiwa Naibu Spika, bado tunazungumza suala la EPZ; kwanza hii EPZ nafikiri sisi Wabunge hapa ambao tunaelewa ndiyo tunafahamu EPZ ni nini. Huko kwetu watu hawaelewi chochote. Unapowaambia habari ya EPZ, hawakuelewi! Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu ya uraia, angalau hata tunapokwenda kuomba maeneo, Watanzania wawe wanajua kitu gani ambacho kinaombewa haya maeneo ili wasiwe wagumu kutoa maeneo yao yaweze kuwekezwa hivi viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia, nenda EPZ leo, hakuna chochote kinachonunuliwa kutoka Tanzania, hakuna! Nimeuliza na nikamwuliza hata Mtendaji Mkuu pale, kwa nini hakuna chochote kinachonunuliwa hapa? Tukaambiwa tunazalisha chini ya kiwango.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, hadi vifungo ambavyo wanatengenezea mashati, suruali, wanasema tunaagiza nje! Nikauliza, tunanufaika na nini hapa kama Watanzania?
Mheshimiwa Naibu Spika, wako vijana na wanawake wamewekwa pale, ukiuliza mshahara wao, utalia! Je, hawa watu baada ya kuondoka, wanatuachia nini? Kuna teknolojia yoyote Watanzania ambayo tutabaki nayo ili kesho na kesho kutwa watoto wetu waweze kuikuta hiyo teknolojia, waweze kufaidika nayo? Hakuna! Wamejaa wenyewe pale, wako wenyewe tu. Mheshimiwa Waziri unajua, tunaomba sana Serikali ihakikishe inawasaidia Watanzania kuelewa na kufahamu kabla hatujafanya maamuzi. Maamuzi tunayafanya juu, lakini huko chini Watanzania hawana taarifa nayo! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo kuna deni kubwa! Deni la shilingi bilioni 60 limezaa shilingi bilioni 190! Mheshimiwa Waziri ukija hapa kumaliza, tuambie hizi shilingi bilioni 190.9 imekuwaje mpaka zimefikia hapa kwa mwaka mmoja, eti ni fidia! Watazitoa wapi ikiwa bajeti yenyewe ni shilingi bilioni 81? Ndugu zangu tunadanganyana hapa! Hatuna kiwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri, watu wa Tabora tunahitaji viwanda, tuwekee hata hicho kimoja tu kwanza, halafu mambo mengine yatafuata wakati ukiwa unaendelea na mikakati yako mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niiombe Serikali sasa, iangalie kwa umakini bajeti ya Wizara hii. Hii Wizara ni mtambuka; ni Wizara ambayo inaingiza vitu vingi sana ambavyo vipo. Hebu basi Serikali ibadilike na ione uwezekano wa kuiangalia bajeti ya Wizara hii ili kweli tuweze kufika kwenye nchi ya viwanda kama tunavyofikiria. Kama tutaendelea kusuasua, mipango ikawa mingi, mikakati mingi, fedha hakuna, haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba basi sasa ifike mahali tuamue, kama tunataka kutengeneza viwanda, tuamue tunaanza na nini? Haya mambo leo kuna hiki, kuna hiki, kuna hiki kwa bajeti ya shilingi bilioni 41 ambayo ni ya maendeleo, tunawadanganya Watanzania, hatutafika. Tunasema leo, tunaishauri Serikali leo, lakini mwisho wa siku haya maneno yataendelea kuwepo kwa sababu hakuna kinachokwenda kufanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, yangu yalikuwa hayo. Ahsante.