Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kupata muda huu wa kuweza kuchangia. Nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo anavyotuongoza. Pia niwashukuru ndugu zetu wa Kenya kwa jinsi ambavyo wamempokea vizuri Mheshimiwa Rais wetu, basi nasi tunafarijika kwa faida ya pande zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie kwanza na Jimbo langu, niishukuru sana Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kutuwezesha kupata Chuo cha VETA ambacho ningeomba sasa kiweze kuanza na kuondoa kero ya ajira hasa kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, naomba kuna shule ya Mbambabei High School ambayo Wizara iliisaidia lakini sasa hivi kuna jengo pale Jengo la Utawala na Maktaba ambalo ni jengo moja kwa muda mrefu halijaweza kukamilika. Niwaombe kupeleka fedha ili jengo hili sasa liweze kutumika na kuwasaidia hawa wanafunzi ikizingatiwa kwamba shule hii toka imeanza imefanya wanafunzi wake wafaulu vizuri na kweli inashika katika nafasi nzuri za kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna maboma ambayo yalikuwa yamepewa fedha ya mabwalo na michoro maalum, lakini imeonekana kwamba zile fedha huwa hazitoshelezi kujenga hayo mabwalo. Kwa hiyo niombe tumalizie hayo mabwalo kwa sababu fedha nyingi za Serikali zimeshatumika na nguvu za wananchi, hivyo ni vema tuyamalizie. Kuna pale Nyasa, kuna shule ya Engineer Stella Manyanya na Liuli ambayo inaendelea sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba nimefurahishwa pia na michango mbalimbali ambayo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wametangulia kuzungumza. Michango ambayo imekuwa, imetazama kwa kina kiasi kwamba pengine kama itafanyiwa kazi inaweza ikarekebisha sekta hii ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, nipende kuwakumbusha ndugu zangu hawa na wananchi kwa ujumla, si kwamba nchi yetu imekuwa haina mikakati maalum ya elimu, tatizo ninaloliona ni uendelevu na wakati mwingine kufanya maamuzi ambayo yanakuwa, yaani kama vile mmoja hana taarifa za kutosha, kwa hiyo ikifikia kufanya maamuzi akimsikia wa kwanza, wa pili wamezungumza, basi maamuzi yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano katika hili suala la ujuzi linalo zungumzwa siku zote, hili suala si jipya, suala la ufundi si jipya tumekuwa na shule maalum za sekondari za ufundi, lakini shule hizi kwa sababu moja au nyingine, naweza nikasema zilifanyiwa uharamia, vifaa vikauzwa, wanafunzi pale wakawa hawafundishwi tena ufundi. Vile vile unakuta sasa hivi hizo shule zilikuwa kuwachukua sasa wanafunzi wa elimu ya sayansi ya kawaida. Ukifuatilia ni kwa nini? Ndiyo maana nasema pengine kwenye Wizara hii ipo haja sana hata mambo ya usalama yaimarishwe, kwa sababu unaweza ukapewa ushauri mwingine ambao unajua baada ya miaka mitano utaua kabisa ile dhamira ya nchi kuipeleka mahali fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano mimi binafsi niseme kwamba nilikuwa kwenye Wizara hii na ninapozungumza sijaribu kusema kwamba hakuna kinachofanyika, Mawaziri wanafanya kazi kubwa na wataalam wanafanya kazi kubwa, lakini hayo ndiyo niliyoyaona kipindi hicho, vyuo havina Walimu wa ufundi. Leo hata ukianzisha vyuo vya ufundi, hawa Walimu wapo kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna ile hali ya mihemko, kwa mfano kuna wakati ilisemwa kwamba huyu amemaliza Advanced Diploma, ya nini? Labda umeme au ufundi, huyu mshahara wake utakuwa mdogo kuliko yule wa degree. Nani atakuwa mjinga akasome Advanced Diploma ambayo ni competence base aache kwenda kwenye degree na uwezo anao? Kwa hiyo hayo ni mambo ambayo yanasababisha watu kufanya maamuzi yasiyo sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazungumza kwamba Watoto wengi wakimaliza vyuo hawawezi kujiajiri, ni kweli hata wakikaa chuoni hawataweza kupata ujuzi wote, lakini hayo mazingira ya kujiajiri huko kwenye maeneo yetu yakoje? Nani anafurahia sasa hivi aende kujiajiri kwenye uvuvi ambapo uvuvi bado anatumia kale kamtumbwi ambako hajui kama atapona. Kwa hiyo lazima tujenge mazingira mazuri ambayo yanamfanya huyu mtoto akimaliza chuo aweze kwenda kujiajiri. Bila kufanya hivyo tutakuwa tunazungumza lakini hatutafika. Kwa hiyo ninachoomba, wakati utakapofikia wa kufanya marekebisho au maboresho mbalimbali, ni vema kuangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulianzisha chuo kwa mfano Chuo Mahiri kile cha Nelson Mandela, lakini unapokuja kugawa rasilimali unakuta chuo kile ambacho unakitaka kifanye mambo makubwa ya umahiri kinawekewa bajeti sawa sawa na chuo kingine ambacho kinafanya mambo ya kawaida. Kwa hiyo kama hatutakuwa tunawekeza kulingana na mahitaji halisi ya kumwezesha huyu mwanachuo aliyepo kwenye eneo fulani, tutakuwa tunapoteza muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya kiufundi, kisayansi au utafiti mara nyingi tunaona uchungu sana kuyapatia fedha, unaona kama vile unapoteza, ukimpa fedha akanunue sijui ka-resister, ka-transistor unasema mbona hela nyingi hii naenda kununua ka-resister, lakini hatujui kwamba katika mafunzo ya aina hiyo lazima mtu ajue kuharibu, ajue kufanya kitu kikawa sawa. Atajua kitu kimekuwa sawa baada ya kujifunza kwa njia zote. Amekosea, ameharibu lakini baadaye anakuja kupata jambo ambalo ni jambo zuri. Kwa hiyo tusipowekeza kwenye maeneo hayo tuseme tutakavyosema hatutakwenda kufanikiwa. Pia tuhakikishe kwamba tunawekeza kwenye wabobezi wa maeneo hayo ya kazi za vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisiposema kwamba nchi yetu imeweza, imefanya mambo mengi. Siku za nyuma ulikuwa hata nyuma tunazojenga ukiziangalia zipo ovyo ovyo tu, lakini siku hizi baada ya kuwa na hao vijana ambao wengine wametoka VETA, wanajifunza maeneo mbalimbali hali yetu ya kiuchumi na kiujenzi au uwekezaji imekuwa ni tofauti na ilivyokuwa. Kwa hiyo lazima tujipongeze kwa yale ambayo tumeyafanya vizuri, lakini tuendelee kuboresha katika maeneo yale ambayo bado hayajawa vizuri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niseme tu kwamba…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana!