Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupewa nafasi hii kuchangia Wizara yetu muhimu ya Elimu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nipeleke salamu kwa Waziri, Wilaya ya Muleba inakupenda na inakupongeza sana, kuna shule yako inaitwa Profesa Ndalichako; wamenituma nikuambie usiwasahau. (Makofi)

SPIKA: Imekuwa ya ngapi kwenye matokeo? (Kicheko)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, anajua mwenyewe Waziri wa Elimu. (Kicheko)

SPIKA: Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, lakini hizo salamu ni kwamba bado wanamhitaji sana na wanahitaji ulezi wake wa kimama na wa kiuwaziri.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwenye COSTECH. Jana kwenye mjadala hapa liliibuka suala la gongo na konyagi kwamba hao watu wanaotengeneza gongo na konyagi mara nyingi wanakimbizana na polisi kwamba ile ni bidhaa ambayo haitakiwi.

Mheshimiwa Spika, tunao vijana wengi wa Kitanzania ambao wamevumbua vitu vingi. Miaka mitatu iliyopita tulikuwa na maneno hapa, kuna vijana ambao walivumbua helikopta, sijui wako wapi leo? Kuna vijana ambao walivumbua magari, wako wapi leo? Serikali yetu kupitia Wizara hii imewapa msaada gani? Tumewaacha hawa vijana wanahangaika wao kwa wao, wanatumia pesa yao na muda wao na ile end product, kama Serikali, hatui-own. Tunawaacha tu na haya mambo yanapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna kipindi nilisoma siku za nyuma Mwalimu Nyerere alikuwa na wazo la kuanzisha vijiji vya sayansi ambavyo vingewasaidia vijana ambao wana ubunifu wa aina yake waende kwenye vijiji vile wakapate muongozo na ku-shape yale mawazo yao tuweze kupata wabunifu ambao wanaweza kutengeneza vitu. Tunavyoviona vinaelea Ulaya; ndege tunaziona zinatembea na magari, yalibuniwa na kuasisiwa na vijana ambao walikuwa na ubunifu kwenye mioyo yao. Huu ubunifu haufundishwi vyuoni wala shuleni, ila ni mtu anazaliwa ni mbunifu haijalishi amesoma kiwango gani, ana elimu kiasi gani, lakini anao ubunifu ule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kazi yetu kupitia Wizara ya Elimu, hasa ile Taasisi ya COSTECH nadhani ndio kazi yake hiyo. Mwalimu alikuja na wazo la vijiji vya sayansi tukaja na COSTECH, lakini sasa ukiangalia pesa wanayopewa COSTECH hawawezi kuendeleza ubunifu ambao mbele ya safari ungeweza kusaidia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudi kwenye jimbo langu. Tunayo kazi kubwa mbele yetu. Nilikuwa naangalia maoteo kwenye jimbo langu tu, mwaka huu vijana ambao wamesajiliwa kidato cha kwanza walikuwa 9,041. Mwaka 2023 watakuwa 21,159, mwaka 2024 tutakuwa na vijana 30,025, lakini ukiangalia miundombinu ya shule tulizonazo ni ileile. Naomba Wizara ijipange, vinginevyo kufika mwaka 2025 tutafukuzana kwa sababu wanafunzi walio kwenye shule za msingi ambao tunatarajia waingie kidato cha kwanza ni zaidi ya mara tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Elimu ihakikishe kwamba mikoa ambayo iko pembezoni mwa nchi kama Kagera na mikoa mingine waiangalie kwa jicho la pekee. Ukienda kwenye mikoa mingi ya pembezoni walimu hawapo, unakuta shule ya msingi au shule ya sekondari ina wanafunzi 1,200 ina walimu sita halafu tunaongelea ubora wa elimu, tunajidanganya. Naomba Wizara ya Elimu tujipange kuhakikisha kwamba mikoa ya pembezoni tunaipatia kipaumbele na kuhakikisha ina nyumba za walimu otherwise walimu wote wanaopelekwa kule wanakimbia kwa sababu ya mazingira magumu.

Mheshimiwa Spika, lakini nipendekeze, kwa mikoa ambayo iko pembezoni mwa nchi tuangalie kuwapatia motisha au allowance, ile wanaita hardship allowance iweze kuwa-sustain kule kwenye mazingira magumu ambako hakuna umeme, wakati mwingine hakuna barabara na ukienda kule kwa kweli wengi wanakataa kwenda maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja mkono na nawapongeza Mawaziri wetu kwa kazi kubwa wanayoifanya, ila Mheshimiwa Waziri asisahau Ndalichako Secondary School. Nashukuru sana. (Makofi)