Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. George Natany Malima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba ya Wizara hii ya Elimu. Niwapongeze sana kwa kazi nzuri ambayo wanayoendelea kuifanya katika wizara hii. Napenda nichangie katika eneo la miundombinu. Sera yetu ya elimu bila malipo imepelekea kuwa na ongezeko kubwa sana la wanafunzi wanaojiunga darasa la kwanza, lakini hata wale wanaojiunga kidato cha kwanza. Kwa hiyo utaona kwamba miundombinu haitoshi kwa sababu ya wingi wa wanafunzi. Kwa hiyo, naishauri sana Serikali kupitia Wizara hii ya elimu iangalie eneo hili kwa jicho la karibu sana kwa sababu uwiano wa watoto wanaojiunga shule na uwiano wa miundombinu inayojengwa haufanani kabisa.

Mheshimiwa Spika, niongelee hasa hapa kwenye madawati. Naamini kabisa catalyst ya kufaulu watoto ni mazingira mazuri ya kusomea. Mtoto anayesoma amekaa chini au amesimama hawezi kufaulu sawa na yule anayekaa kwenye viti. Hata hivyo, ninachokiona, mara nyingi msisitizo wa kutengeneza madawati unafanyika mwezi Januari, wanapojiunga darasa la kwanza na kidato cha kwanza ndipo matamko yanatoka kwamba kufika tarehe Fulani madawati yaweshakamilika, watoto waanze shule. Baada ya hayo hakuna kitu kinaendelea na mimi katika Jimbo langu la Mpwapwa, watoto wameathirika, wapo waliosubiri madawati yatengenezwe ndipo wajiunge na shule wakati wengine walishaanza tayari kusoma; wao wanasubiri madawati yatengenezwe.

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa naomba nishauri Serikali tuwe na Mpango endelevu wa kutengeneza madawati. Kwani kuna ubaya gani ikifika Januari tuna madawati store, lazima tuwe na utaratibu wa kutengeneza madawati kwa kutumia halmashauri zetu. Madawati yatengenezwe mwaka mzima ili tuwe na madawati ya kutosha, yawekwe stote. Tunapofungua shule mwezi Januari basi wanafunzi wapate mahali pa kusomea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni walimu, walimu kama tunavyojua wote hawatoshi na mimi ningeshauri Wizara ijitahidi sana kupata vibali kwa ajili ya kuajiri walimu. Lakini kuna tatizo moja dogo. Katika Jimbo langu nime-experience, walimu wanapangiwa vituo, wanaripoti halafu wakiondoka hawarudi tena. Hiyo sielewi kwa sababu unahesabika kama shule il eina walimu saba kumbe ina walimu sita au watano. Walimu wawili waliripoti halafu hawakurudi tena kwenye kazi, ni kwasababu ya mazingira ya namna hiyo. Sasa Wizara lazima ije na Mpango na ikiwezekana ikomeshe tabia hii ya walimu ambao wanaajiriwa na kupangiwa vituo halafu wanaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia vijana wetu wengi wanaomaliza elimu ya vyuo vikuu hawarudi makwao, wanakaa mjini. Kwenye miji kama Dodoma, Dar es Salaam, Arusha na mahali pengine wamejazana na kila siku utakutana nao wana bahasha za kaki wakitafuta kazi za kuajiriwa. Ni kwasababu elimu waliyoisoma hawawezi kui-apply kule walikotoka. Hawawezi kui-apply kwenye mashamba, kwenye entrepreneurship kwasababu hawakujifunza hayo. Kwa hiyo, nataka nitoe wito kwa Wizara, Mheshimiwa rais katika hotuba yake juzi alizungumza habari ya kuboresha mitaala ili iendane na mazingira ya nchi yet una iendane na soko la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilimo ndiyo sekta inayotoa ajira kwa wingi kuliko sekta nyingine yoyote lakini kwa bahati mbaya sana haifundishwi sasa shuleni. Kwa hiyo unategemea vijana wote ambao watamaliza shule hawawezi kwenda kufanya kilimo kwasababu hawajajifunza. Sasa tunapoiangalia mitaala hii kwa upya lazima iendane na mazingira yetu. Tuwafundishe katika sekta ambayo wataenda kufanya ajira, wanaenda kupata ajira ya kutosha. Wataenda kujiajiri wenyewe na ndiyo lengo letu. Elimu yetu i-focus kwenye kujiajiri wenywe. Vijana wetu wajiajiri wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda niwapongeze wamezungumza habari ya ukarabati wa vyuo vyetu vya ualimu. Ni muhimu sana walimu wetu wakafundishwa, wale wanaokuja kufundisha watoto wetu wakasoma katika mazingira mazuri katika Jimbo langu la Mpwapwa chuo chetu kinasaidika katika utaratibu huu. Bajeti inayoisha mwaka huu tulipata shilingi bilioni 2.1 kwa ajili ya ujenzi wa miradi mipya pale chuoni. Kuna ujenzi wa bwalo, kuna ujenzi wa jengo la ghorofa moja kwa ajili ya computer lakini kuna ujenzi wa nyumba za watumishi ambao iko katika mtindo wa two in one. Lakini kinachonisikitisha ujenzi umesimama…

SPIKA: Tayari, muda umekwisha Mheshimiwa.

MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, naomba Wizara iangalie ili ujenzi huu uanze mapema. Naunga mkono hoja. (Makofi)