Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuendelea na mjadala ambao uko Mezani wa bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Profesa Ndalichako, pamoja na timu yake nzima ya Wizara yake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita. Tumeona mafanikio makubwa katika sekta ya elimu, lakini bado katika mpango wa bajeti ya Wizara hii katika utekelezaji wa kipindi hiki cha 2021/2022 tumeona bajeti namna ambavyo inakwenda kuendelea kuboresha sekta ya elimu katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu mbalimbali ikiwemo shule za msingi, sekondari pamoja na vyuo. Hauwezi kwenda chuo ama chuo kikuu bila kuanza shule ya msingi. Tumeona namna ambavyo shule zetu za msingi, hasa zile zilizojengwa tangia miaka ya 1960, 1970, shule ambazo mpaka sasa hivi zinatumika lakini ni shule ambazo zimekuwa chakavu mno. Mabati yameshaoza. Wakati wa mvua watoto wanashindwa kukaa madarasani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba katika mpango wa kuboresha shule kongwe ambao ulitekelezwa kwa kipindi kilichopita ambao Mheshimiwa Prof. Ndalichako alianza nao, tunaomba tuendelee kuboresha shule zetu za msingi ziweze kuwa katika hali nzuri na tuendelee kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waswahili wanasema usipojenga ufa utajenga ukuta, kwa hiyo, kuna kila sababu sasa ya Serikali kuona namna gani tunakwenda kuboresha shule za msingi. Na nina hakika maeneo mengi Waheshimiwa Wabunge wanayalalamikia katika shule hizi za msingi kuona kwamba zina uchakavu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Lindi Manispaa tunazo shule karibia 12, shule ambazo ni chakavu mno kupitiliza. Lakini unajua kwamba Mji wa Lindi ni mji mkongwe sana ambao walianza kukaa wakoloni huko. Kwa hiyo tuna kila sababu sasa ya kutusaidia Lindi kwa sababu maeneo mengi tumerithi kutoka kwa wakoloni kwa hiyo majengo yamekuwa machakavu mno. Ninaiomba sasa Serikali kuangalia namna gani wanaweza kutusadia kuhakikisha kwamba shule hizi za msingi zinaendelea kuboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishukuru Serikali kupitia fedha za EP4R; zimekuwa ni msaada mkubwa na zimesaidia kwa kiasi kikubwa sana kumaliza maboma ambayo wananchi wamejitolea. Na pale Lindi tumefaidika na fedha hizi, zaidi ya milioni 200 zimekuja na zinafanya kazi ya kuendelea kukamilisha madarasa haya ili yawe katika sura nzuri na watoto wetu waendelee kupata masomo yao.

Mheshimiwa Spika, zipo changamoto za jumla upande wa shule za msingi na sekondari. Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukizungumzia karibia wiki nzima, kuna upungufu mkubwa sana wa walimu katika maeneo haya, na Mheshimiwa Rais ameshatoa katika hotuba yake kuajiri watu 600. Ninaomba tuzingatie katika sekta ya elimu kupeleka walimu wa kutosha ili watoto wetu waendelee kusoma vizuri lakini tuweze kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto hiyo ya walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa kuna changamoto ya wlaimu wanaostaafu kutopewa malipo yao kwa wakati. Hizi ni hoja za jumla ambazo zimezungumziwa, pamoja na kupandisha madaraja lakini nina hakika kwamba wahusika wataendelea kusimamia kuhakikisha kwamba changamoto hizi zinaondoka.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha mwaka hadi mwaka kuhakikisha kwamba inatenga fedha kwa ajili ya kwenda kuwekeza katika vyuo vya VETA ambavyo vinawasaidia watoto wetu wanaomaliza darasa la saba wakashindwa kuendelea, pamoja na form four wanaoshindwa kuendelea na masomo ya juu. Kwa hiyo, vimekuwa vikisaidia sana kuwapa mafunzo mbalimbali vijana wetu ili waweze kupata ufundi stadi na waweze kutengeneza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Lindi Manispaa tumebahatika kuwa na Chuo hiki cha VETA na kimejengwa muda mrefu. Kuna changamoto; vifaa vya kufundishia vimeendelea kuwa chakavu lakini hata magari yameendelea kuwa chakavu kwasababu kuna masomo pia ya udereva katika vyuo hivi vya VETA.

Mheshimiwa Spika, vijana hawa wanaokwenda kupata mafunzo katika vyuo vya VETA ninaishauri Serikali kuwa na mahusiano kati ya chuo cha VETA, wanafunzi na halmashauri kwasababu wanavyokwenda kusoma VETA wanapata mafunzo mbalimbali, wanaporudi kwao baada ya kumaliza masomo wanashindwa kujiendeleza kwasababu wanakuwa hawana fedha za kuendelea kuzalisha na kukuza uchumi pamoja na kwenda kuwekeza kwenye viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kwasababu halmashauri tuna asilimia kumi ya mapato, ingeweza kutumika kwenda kuwaboresha vijana hawa ambao tayari wanapata mafunzo kutoka VETA ili sasa kuwawezesha vijana kuendeleza yale mafunzo waliyopata ili kuendelea kukuza uchumi na kuendelea kumudu kuendesha maisha yao. Nafikiri tukifanya hivyo tutakuwa tumepunguza mzigo mkubwa kwa Serikali, lakini tutakuwa tumewawezesha vijana hawa kujiendeleza kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Lindi Manispaa tumetoa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa vyuo vikuu, kampasi ya Lindi. Chuo Kikuu kampasi ya Kilimo tumetoa zaidi ya ekari 120 lakini mpaka leo ujenzi haujaanza. Lakini pia tumetoa ekari 150 kwa ajili ya Chuo Kikuu cha masuala ya Uvuvi na Usafirishaji Baharini.

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali sasa kutoa fedha ili kuendeleza ujenzi huu, kuhakikisha kwamba vyuo vikuu hivi kampasi ya Lindi vinaendelea kujengwa, lakini watakaofaidika na vyuo vikuu hivyo siyo Wanalindi peke yake, Kanda nzima ya Kusini watapata elimu pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali kuhakikisha kwamba tunaendelea kuvisimamia vyuo vikuu hivi ili viweze kukamilika katika ujenzi wake hata kama si kwa asilimia 100 lakini kila mwaka tungeweza kutenga fedha na hatimaye tungeweza kumaliza kuhakikisha kwamba ujenzi huo unakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna chombo kinachoitwa SIDO; SIDO inatoa mafunzo ya ufundi stadi lakini inasimamia masuala mbalimbali ya wajasiriamali pamoja na wanaoingia katika uanzishwaji wa viwanda vidogovidogo. Ninaiomba Serikali kuendelea kutumia SIDO katika maeneo yetu, maeneo ambayo chombo hiki kipo ili kuwezesha fedha za kutosha na kuendelea kuwawezesha vijana wengi kuingia katika maeneo haya ya ufundi stadi na uwekezaji wa viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)