Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa ili niweze kutoa mchango wangu katika hii sekta muhimu sana kama ambavyo umeshaeleza hapa kwamba huu ndiyo moyo wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza vizuri sana hotuba ya Mheshimiwa Waziri na nimesikiliza vizuri sana taarifa ya Mwenyekiti wetu wa Kamati ambayo maeneo mengi mbalimbali wameyagusa, lakini nataka tu kujikita katika mambo haya yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo mengi ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi kwa haraka ili kuwezesha utoaji wa elimu katika sekta shule zetu za sekondari na msingi ili kwenda vizuri zaidi. Kwa mfano, tunalo tatizo kubwa sana sasa hivi la vyoo vya kisasa katika shule zetu za msingi na sekondari ambavyo maeneo mengi kutokana na ukosefu wa hivi vyoo vya kisasa, vinajaa kila siku. Kwa sababu vinajaa na vyoo vile siyo vya kisasa, inabidi kila kinapojaa mbomoe miundombinu ile mjenge mingine.

Mheshimiwa Spika, kuna shule moja eneo lililochimbwa vyoo sasa hivi limefikia ekari tatu. Kwa hiyo, itafika mahali eneo la shule lote litachimbwa vyoo kila sehemu. Kwa hiyo, ni lazima Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI kuja na mkakati wa haraka sana wa kujenga vyoo vya kisasa, lakini pamoja na kuandaa madampo ya kisasa kwa ajili ya kumwaga zile taka. Hilo ndio litakalotuwezesha kuwa salama zaidi, ili vijana wetu katika shule za msingi na sekondari wasome vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii kampeni lazima tuende nayo kwa speed kubwa sana ya ukamilishaji wa magofu ambayo wananchi wameyaanzisha. Tuna upungufu mkubwa wa madarasa, magofu yapo wananchi walishajenga wamefikia ile hatua, lakini bado hayajamaliziwa. Tuna maabara, bado hazijakamilika, nyingine zimejengwa zimekamilika, lakini vifaa hamna, tuna mahitaji makubwa sana ya hostels.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi kubwa sana iliyofanywa katika Serikali ya Awamu ya Tano, lakini bado kuna mahitaji makubwa ambayo tunatakiwa kuhakikisha kwamba, tumeyakamilisha kikamilifu ili vijana wetu waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ni muhimu sana, limezungumzwa na kila tukizungumza suala la ajira, tunazungumza suala la ujuzi. Mambo haya ni makubwa sana na wewe umekuwa uki-comment hapa Bungeni, lakini nataka niseme hivi tunataka kupata vijana wenye ujuzi, vijana ambao wameandaliwa. Tunawapataje…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge nawaomba sana, kama kawaida yetu tumpe nafasi anayezungumza, tumsikilize vizuri.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, tunawapataje vijana wenye ujuzi wakati masomo ambayo yangeweza kuwawezesha vijana hawa kupata ujuzi hayapo, yameondolewa. Kwa mfano, leo hii vijana wanaoenda internship ni wale tu wanaosoma masomo ya udaktari wa binadamu, lakini wale wanaosoma masomo ya udaktari wa mifugo hawaendi intern. Wale wanaoenda kusoma mafunzo mengine ya uvuvi, mafunzo mengine ya kilimo, ili tuweze kuandaliwa wataalam ambao wamepitishwa kwenye tanuru na wakaiva, lakini hawaendi intern. Sasa mwisho wa siku unategemea unawapata wapi vijana wenye ujuzi wanaoweza kutumika sawasawa?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo unakuta kwa upande wa Madaktari kwa sasa hivi wanafanya vizuri sana kwa sababu, wanapata mwaka mmoja kwa ajili ya intern na wanalipiwa na Serikali. Sasa shida iko wapi kwa vijana wengine hawa? Tunahitaji Maafisa wa Mifugo na Madaktari wa Mifugo walioandaliwa vizuri, wanafundishwaje? Tunahitaji wataalam wa uvuvi walioandaliwa vizuri, wamefundishwaje? Tunahitaji wataalam wa kilimo walioandaliwa vizuri, wanafundishwaje na mtaala wetu unasemaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulifika mahali hapa masomo kwa mfano ya kilimo yaliondolewa shuleni; shule ya msingi yakaondolewa, sekondari yakaondolewa, lakini unafundisha vijana shule ya msingi, unafundisha vijana sekondari ambao unatarajia baada ya kumaliza masomo yao asilimia 70 waende kulima, halafu somo lenyewe la kilimo halifundishwi na liliondolewa shuleni. Sasa tunategemea mabadiliko gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, somo la ujasiriamali nalo kwa nini halijawekwa kuwa la lazima? Kwa sababu, hata ukisoma udaktari si lazima ujifunze kutunza hizo fedha na huo mshahara ili uweze kukutosheleza? Si lazima ujifunze ku-debit na ku-credit ili ujue matumizi yako unasimamiaje mwisho wa mwezi? Kuna shida gani somo la ujasiriamali kufundishwa kwa kada zote kuanzia shule za msingi, vijana wakafundishwa vizuri ujasiriamali, wanafika sekondari wanafundishwa vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa unafundisha watu waende kulima, wakienda kule hawajui hata kufungua tractor, hawajui hata kuwasha tractor, hawajui hata kuswaga plough, hawajui hata kushika jembe, halafu Taifa lenyewe ni la wakulima hili. Sasa Taifa la wakulima, somo la kilimo limehujumiwa, halifundishwi, sasa sababu za kuhujumiwa somo la kilimo ni nini? Sababu za kuhujumiwa somo la ujasiriamali ni nini? Naona ni kuifanya Tanzania hii itengeneze watu ambao hawana uwezo wa kwenda kutumika sawasawa katika kulitumikia Taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la utafiti. Limeelezwa ukisoma vizuri sana wanaongea hapa, lakini niseme suala la utafiti katika nchi yetu halijapewa kipaumbele kinachotakiwa. Hili suala tusipolipa kipaumbele kama inavyotakiwa tutaendelea tu kuanguka kila mwaka kwa sababu, leo hii tunazungumzia udahili wa wanafunzi na tunasema udahili umeongezeka, chuo kikuu umeongezeka, vyuo vya ufundi umeongezeka, lakini nani anayefanya trace study ya kuwajua hawa watoto baada ya kumaliza masomo yao wanaenda wapi? Wanaenda kufanya nini? Wako wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati nikiwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi tulifanya utafiti wa kufuatilia vijana wanaomaliza, waliosoma masomo ya mifugo baada ya kumaliza masomo hayo wanaenda wapi. Katika vijana 8,000 vijana mia saba na kitu tu ndio walioonekana kupata ajira na vijana asilimia 90.5 hawajulikani wako wapi na wanafanya nini. Sasa kama tafiti hizi haziwezi kufanywa mtakuwa mnasema tu tunadahili wanafunzi, udahili umeongezeka. Sasa udahili umeongezeka, umeongezeka kwenye jambo gani?

Mheshimiwa Spika, bado tuna vijana leo anataka sasa achague kozi yake anataka kwenda kusoma mchepuo gani. Anataka kwenda kusoma kilimo, anataka kwenda kusoma uvuvi, anataka kwenda kusoma uhasibu, anataka kwenda kusoma biashara, lakini utafiti uliofanyika wale waliosoma masomo hayo leo wako wapi? Atachaguaje sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pengine unaenda kuchagua unataka kwenda kusoma biashara, vijana toka mwaka 2005 waliosoma biashara graduates hawajapata kazi. Sasa wewe leo unachagua kwenda kusoma biashara ili uajiriwe na nani? Soko la ajira linasema nini? Linahitaji nini? Linahitaji kijana gani aliyeandaliwa wapi? Takwimu hizi na utafiti huu kwa nini haufanywi?

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Elimu kwa nini utafiti huu haufanyiki, ili vijana wakapata base ya kuchagua kwamba, sasa hivi nataka mimi kwenda kusoma mifugo. Sasa nataka nijue vijana waliosoma mifugo ajira katika sekta binafsi ajira zipo? Hamna, ingeoneshwa percent kwamba, leo hii ajira katika sekta ya mifugo ni asilimia mbili. Leo hii ajira katika uvuvi ni asilimia kadhaa, leo hii katika kilimo ni kadhaa, vijana wetu wangeweza kuchagua kulingana na mahitaji ya ajira kwa wakati huo. Hivyo, hata udahili wa wanafunzi sasa hata vyuo vyetu vinavyoweza kupanua udahili vipanue udahili kulingana na madai na mahitaji ya soko yaliyopo kwa sasa, sio tu mtu anachagua tu kwa hiyari mimi naenda kusoma accounts, mimi naenda kusoma business administration; unaenda ku-administer wapi? Mahitaji yako wapi?

Mheshimiwa Spika, lakini hata training pia ya Maprofesa wetu na Madokta wetu tunaowapeleka chuoni kwa sasa bado kuna shida kubwa kwa sababu kijana anayebakishwa shuleni kwa ajili ya kuwa lecturer ni yule aliyepata “A” nyingi, lakini si yule aliye-practice katika lile eneo. Kwa hiyo, unafundishwa biashara na mwalimu ambaye amepata “A” nyingi, lakini hajawahi kufanya biashara yoyote na wala hajawahi ku-practice eneo lolote. Kwa hiyo, mwisho wa siku utatengeneza vijana gani wa namna hiyo? Kwa nini mfumo huu usibadilishwe?

Mheshimiwa Spika, leo hii tunafanya vizuri sana na nataka nipongeze kabisa, kwa sababu, mara nyingi wanaowafundisha madaktari wetu ni wale ambao wanatibu binadamu, kwa hiyo, wanakuwa na experience ya kutosha katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunayo safari kubwa ya kufanya mageuzi kwenye nchi yetu na mageuzi ya kweli yatafanyika kwa kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu. Tukishajipanga vizuri kwenye sekta ya elimu, leo hii tunazo taasisi ambazo zinafanya shughuli ya utafiti, kwa mfano kwenye uvuvi tuna TAFIRI, kwenye mifugo tuna TARIRI, kwenye kilimo tuna TARI, kwenye misitu tuna TAFORI, tuna COSTECH, tuna NBS. Hizi taasisi zinakutana wapi? Nani anaandaa zile agenda za utafiti? Ile database ya tafiti zinazofanyika nchini tutaiona wapi? Hizo tafiti zinazoandaliwa zinawafikiaje watu? Kanuni zilizopo kwa ajili ya tafiti hizo, kuzilinda zile tafiti zipo wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu saa nyingine hata taasisi zetu za utafiti zinafanya hata mambo ya nje ambayo wakati mwingine hayana manufaa kwenye Taifa letu. Tufanye mageuzi ya kweli katika sekta hii. (Makofi)