Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ukiukwaji mkubwa sana wa haki za binadamu ambao umekuwa ukifanywa na Jeshi la Polisi na ukiukwaji huu umefanyika hasa pale Polisi wanapokuwa wakiwakamata watuhumiwa, wamekuwa wakikiuka hizi haki ikiwa na pamoja na kuwafanyia vitu vya hovyo ambavyo pia vinakiuka kabisa haki za binadamu.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ripoti ya Haki za Binadamu iliyotolewa Aprili, 2021, imesema wazi kabisa, ripoti hiyo ilikuwa ni ya mwaka 2019/2020, imesema wazi kabisa kwamba matukio manne ya mauaji ya raia yamefanyika mikononi mwa polisi. Na matukio haya yalifanyika tu kutokana na polisi kuwakamata watuhumiwa kwa kutumia nguvu kubwa sana ambayo ilisababisha pia watuhumiwa kupoteza maisha.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu, Ibara ya 13(6)(b), nitainukuu, inasema wazi kabisa kwamba; “Ni marufuku kwa mtu aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo;”(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini haya mambo tumekuwa tukiyashuhudia wazi kabisa, raia wetu wakitendewa mambo ya ajabu, kana kwamba wameshakutwa na makosa wakati huo bado Mahakama inakuwa haijathibitisha makosa yao, jambo ambalo linakiuka haki za binadamu.

Mheshimiwa Spika, sheria hiyohiyo Ibara ya 13(6)(e), inasema; “Ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili tumeliona likifanywa na Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, lakini mbali na hayo, tunajua wazi kabisa, wakati mwingine watuhumiwa wanapokamatwa na kupelekwa katika vituo vya polisi kule hakuna bajeti ya chakula, lakini watu wamekuwa wakikamatwa, wakijazwa katika vituo vya polisi na sheria inasema mtu akikamatwa anatakiwa akae kwenye kituo cha polisi saa zisizozidi 48. Lakini watu wanakaa mpaka wiki mbili wako mikononi mwa polisi, jambo ambalo limekuwa likikiuka kabisa sheria za…

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa; mwenye taarifa aendelee.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hata matendo ya kikatili kwa watoto wa kike na wanawake yanafanyika katika vituo vyetu vya polisi, wanavyokamatwa watu wanafanyiwa mpaka ubakaji kwenye vituo vyetu vya polisi.

Mheshimiwa Spika, nampa taarifa hiyo kwasababu vipo na kama utakuwa unatakiwa uthibitisho watu waende wakaulize mahabusu ambao wamekaa zaidi ya mwezi vituo vya polisi na wakapelekwa magerezani.


SPIKA: Pokea taarifa Mheshimiwa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa hiyo kwasababu hata mwaka jana, mwezi Agosti nilipokamatwa na Jeshi la Polisi, nilitishiwa kumwagiwa tindikali usoni. Kwa hiyo hivyo ni vitendo ambavyo vinafanywa na Jeshi la Polisi.

SPIKA: Mheshimiwa Stella, yaani kidogo nishtuke kwamba na wewe ilikuwa… endelea kuchangia Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, suala la wananchi wetu kukosa dhamana; leo hii suala la dhamana limekuwa kama tu ni zawadi ya polisi. Wananchi wamekuwa wakikosa dhamana kwa makosa ambayo yanadhaminika kisheria. Na jambo hili limesababisha magereza mengi kujaa sana. Jambo hili la wananchi wetu kunyimwa dhamana limesababisha wananchi wetu kujaa sana huko magereza bila sababu za msingi.

Mheshimiwa Spika, wakati huohuo, kumekuwa na matukio mengi sana ambayo yanasababisha kunyima uhuru wa watu wetu, ikiwa ni pamoja na watu kukaa muda mrefu gerezani, mtu anakaa mpaka miaka kumi, mitano, mitatu, kesi yake bado haijasikilizwa. Akiuliza anaambiwa upelelezi bado haujakamilika. Lakini mwisho wa siku huyu mtu inakuja kutolewa hukumu hajakutwa na hatia, amekaa gerezani miaka kumi, hiki tunawanyima wananchi wetu haki zao za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaishauri Serikali iweze kuleta Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Makosa ya Jinai, tufanye marekebisho ya sheria hizo ili kuwapa uhuru wananchi wetu. Kwasababu mwisho wa siku tunayajaza tu magereza bila kuwa na masuala ya msingi kabisa.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kabisa; ndani ya magereza kumekuwa na mambo mengi sana ambayo wengine wameyazungumzia lakini ntayazumgumzia hapa. Pamoja na changamoto ambayo ameizungumzia dada yangu, Mheshimiwa Esther, magerezani kiukweli kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.

Mheshimiwa Spika, leo hii magereza wanachanganywa na watoto wa miaka 13, 14 hadi 15. Mwanamke wa miaka 60 anakaguliwa mbele ya mtoto wa miaka 14; hili jambo kiukweli linahuzunisha sana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Stella, muda hauko upande wetu.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru.