Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia na kwa sababu ya muda moja kwa moja naomba nijielekeze kuzungumzia Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, katika Jeshi la Polisi kozi mbalimbali zinatolewa na tunafahamu wazi kwamba kozi hizi ni nzuri kwa sababu zinawajenga askari wetu. Hata hivyo, kuna hii refresher course kwa ajili ya kuwajenga uwezo askari na utaratibu wa sasa hivi ni kwamba ni lazima ifanyike kwenye vyuo vya askari ambavyo viko Zanzibar, Moshi pamoja na Kidatu.

Mheshimiwa Spika, kozi hizi ni nzuri lakini utaratibu unaotumika sasa hivi si rafiki sana na hauleti tija. Katika kozi hizi askari wanajitegemea chakula na tunafahamu kabisa mishahara ya askari au watumishi mingi ni midogo lakini pia inakuwa na makato mbalimbali. Askari wetu wengi wanategemea sana posho lakini wanapokuwa kwenye mafunzo haya inawalazimu kukatwa Sh.7,000 kwa siku kwa ajili ya chakula.

Mheshimiwa Spika, jambo hili si jambo rafiki sana kwa sababu kwanza linazuia tija ya kozi ile badala ya askari ku- concentrate na kozi anakuwa anawaza kwamba anatakiwa achangie pesa hiyo na inakatwa moja kwa moja kwenye posho. Tunafaahamu kwamba kwa siku posho ya askari anapewa shilingi 10,000, kwa hiyo, tunapokata shilingi 7,000 tunamlazimisha abaki na shilingi 3,000 ili aweze kuitumia na familia yake. Kwa hiyo, jambo hili linamfanya awe na mawazo lakini pia atashindwa ku-concentrate kwenye mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe tu ushauri, utaratibu wa zamani ulikuwa ni mzuri, hizi refresher course zilikuwa zinafanyika kwenye mikoa husika kwa maana kwamba zilikuwa hazina makato ya gharama za chakula.

T A A R I F A

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa endelea.

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa mchangiaji kwamba kozi hiyo inaitwa ya utayari na ilianza kutolewa kwa muda wa wiki mbili, wiki tatu, mwezi mmoja sasa hivi inatolewa kwa muda wa miezi mitatu. Akimaliza kozi hiyo baada ya wiki moja imeanzishwa tena kozi nyingine, kwa hiyo, ni tabu kidogo. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa unapokea taarifa hiyo?

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo kwa sababu hiyo miezi mitatu kama askari akiwa kozi atakatwa Sh.7,000 kila siku.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naendelea na utaratibu wa zamani ambapo kozi hizi zilikuwa zinafanyika kwenye mikoa husika hizi gharama za chakula hazikuwepo. Askari wali-concentrate kwenye kozi kwa sababu mwisho wa siku walirudi nyumbani kwenye familia zao. Kwa hiyo, naishauri Serikali aidha utaratibu huu wa zamani ufuatwe au basi kama itawezekana Serikali ichukue gharama hizi za chakula kwa sababu haiwezekani tumpe mafunzo polisi halafu ajigharamie chakula. Kwa hiyo, naomba kuishauri Serikali aidha ichukue changamoto hii ya chakula igharamie au urudishwe mfumo ule wa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze sana Wizara pamoja na Kamati imetoa ushauri mzuri lakini bado kuna changamoto kubwa ya vitendea kazi pamoja na stationeries.

Hivi navyoongea sasa hivi Kituo cha Polisi Kigoma Mjini hakina gari la askari. Sasa unaweza ukaona ufanisi utatoka wapi kama vitendea kazi vinakuwa adimu hasa tukijua kabisa Kigoma Mjini pale kuna bandari, benki na mambo mengi ambayo yangehitaji ulinzi wa raia na mali zao lakini mpaka sasa hatuna gari la askari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini imekuwa ni utamaduni bajeti hizi zinazotengwa hazitoshelezi kuendesha haya magari ya askari. Leo hii ukipata tatizo ukipiga simu polisi utaambiwa gari haina mafuta, mbovu au haipo. Kwa hiyo, napenda kuishauri sana Wizara iingilie kati jambo hili hasa kwenye mfumo wa bajeti ya mafuta ili askari wetu hawa wawezeshwe vizuri na tutakapokuwa tunahitaji huduma tuzipate kwa wakati kwa sababu imekuwa ikileta shida sana kwa wananchi wanapotaka huduma ya kipolisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 12, ameeleza namna ambavyo wanashughulikia makosa na taarifa zinazotolewa Polisi, lakini kumekuwa na mlundikano mkubwa sana wa mahabusu katika Vituo vya Polisi. Utaratibu huu tunaona ni kinyume na sheria. Sheria inatutaka tusizidishe masaa 48 mtu awe ameshafikishwa Mahakamani, lakini utaratibu huu haufwatwi, vijana wanawekwa ndani, ukiulizia unaambiwa upelelezi unaendelea au unaambiwa maelezo hayajachukuliwa. Kwa kweli hali hii inawatesa sana wananchi. Kwa hiyo, naiomba Wizara ione namna nzuri ya kushughulikia jambo hili, kupunguza msongamano wa mahabusu katika Vituo vya Askari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona kabisa na ni wazi kwamba katika majeshi mengine kumekuwa na utaratibu mzuri wa kuwa-handle hawa Askari wa kike, wamekuwa wakipatiwa fedha ya kujikimu katika mazingira yao ya kike hasa ya hizi pads, lakini katika Jeshi la Askari Polisi, Askari wa kike hawapatiwi. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara, kama yote ni majeshi, kwa nini wengine wapatiwe, wengine wasipatiwe? Kwa hiyo, naomba sana jambo hili liweze kuchukuliwa serious, kwani Askari hawa wanafanya kazi ngumu, nzito na pia wanafanya kazi ambayo inaleta maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

MHE. NEEMA F. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa Neema, endelea.

T A A R I F A

MHE. NEEMA F. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kutoa taarifa kwamba jambo hili la uhitaji wa taulo za kike siyo tu kwa watumishi maskari wanawake, pia kwa wafungwa na mahabusu wanawake.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imekuwa ikitenga bajeti ndogo kwa ajili ya kuwawezesha wafungwa na mahabusu wanawake, lakini bajeti hii imekuwa haitoki na matokeo yake hawa wanawake walio mahabusu na wafungwa wanatumia magodoro na magazeti wanapokua kwenye siku zao jambo ambalo ni hatarishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Kabla Mheshimiwa Sylivia hujaendelea, hii inanikumbusha wakati wa vita vya Kosovo na Herzegovina palikuwa na vita moja kule Yugoslavia ya zamani ambayo ilikuwa mbaya sana. Sasa baada ya vita ile kwisha, wakawa wanamhoji mtu mmoja, raia wa kule kwamba katika vita hii, kitu gani kilikuwa ni shida kubwa sana katika kipindi cha vita? Yule mtu akasema, yaani hebu imagine wakati ule kulikuwa hakuna toilet paper. Yaani kwake katika shida kubwa wakati wa vita, kulikuwa hakuna toilet paper kabisa. Sasa you can imagine matatizo makubwa kama haya! Endelea Mheshimiwa Sylivia. (Kicheko)

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naipokea taarifa.

SPIKA: Nafikiri siyo kwa Polisi peke yake, itakuwa na Magereza, Uhamiaji na Zimamoto labda. Ahsante, endelea. (Makofi)

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimalizie kama nilivyokuwa naeleza. Kwa hiyo, jambo hili linabidi lichukuliwe kwa uzito wake, wanafanya kazi ngumu, lakini pia mazingira siyo Rafiki.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia kabisa, kwenye hizo stationary, sisi tunaotokea mikoa ya pembezoni, mgao huu wa stationaries unachelewa kutufikia. Leo Kigoma na mikoa mingine ya pembezoni, nafikiri hata na Rukwa, tunachelewa kupata vitendea kazi (stationary). Unakuta hizi log book pamoja na mambo mengine havitufikii kwa wakati. Tunaomba sana Wizara izingatie mgawanyo huu, hat sisi wa mikoa ya pembezoni tuzipate basi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunapozungumzia suala la vitendea kazi ambavyo nimesema, ilikuwa ni ajabu sana, juzi nilipigiwa simu na mwananchi, amefika Kituo cha Polisi hajapata PF3, anaambiwa zimekwisha, akatoe copy nje. Nadhani tuweke utaratibu mzuri, kama hizi document… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)