Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti hii. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Doto Biteko, Waziri kwa wasilisho zuri. (Makofi)

Vilevile nitumie nafasi hii kutoa pole sana kwa Mwenyekiti wa CCM wa Jimbo la Ludewa kwa kuondokewa na Diwani Viti Maalum mama yetu mpendwa Grace Mapunda.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba nianze kwa kusema naamini kwamba rasilimali inafaa kuitwa rasilimali pale ambapo inatumika kikamilifu ili iweze kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa letu. Kama tuna rasilimali halafu tunaziangalia tu hapo inapaswa tutafute jina lingine, sio rasilimali tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hilo, Jimboni kwangu Ludewa kuna madini mengi ambayo watu wa GST wameweza kuyabaini na hivyo watafiti mbalimbali wamekuwa wakienda kule. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba anajitahidi kufanya vizuri sana, wale watafiti wa madini wanavyokwenda kwenye vijiji wanavamia mashamba ya wananchi bila kulipa fidia na mashamba mengine yanakuwa yako kwenye miliki za vijiji kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na.5 ya mwaka 1999.

Mheshimiwa Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Ibara ya 24 inazungumzia haki ya kila mwananchi kumiliki mali na mali yake ilindwe na Serikali na pale inavyotwaliwa anapaswa kulipwa fidia. Sasa watafiti wa madini wakienda kule wanavamia mashamba ya wananchi wanaanza kuchimba bila kulipa fidia.

Mheshimiwa Spika, zile fedha wangekuwa wanalipa kama ni kwenye vijiji au wananchi zingesaidia sana hasa kupunguza michango ambayo wananchi wanatozwa kila leo kwa ajili ya madawati, madarasa na vituo vya afya. Kwa hiyo, kama vijiji vingekuwa vinalipwa ile fedha kama fidia ya ardhi yao ambayo wanaichimbachimba kufanya utafiti kwa sababu wanaochukua leseni za utafiti wengine wanachimba madini, wakilipa zile fidia zitasaidia vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nipongeze Bunge lako Tukufu hasa la Awamu ya Tano ambalo liliweza kupitisha sheria nyingi za kulinda rasilimali zetu. Naomba sasa elimu itolewe kwa wananchi na wapewe maandalizi hasa maeneo ambapo miradi mikubwa inakwenda kuhusu nini sheria hizi zinazungumzia kuhusiana na masuala haya. Kwa mfano, kule jimboni kwangu tunaenda sasa kutekeleza mradi wa Mchuchuma na Liganga lakini wananchi hawajaandaliwa.

Mheshimiwa Spika, wale Waheshimiwa Madiwani pia wanaweza kupewa mafunzo kuhusiana na hii CSR, kwa sababu unakwenda kujadiliana na mtu ambaye ni tajiri, bepari, mwenye uwezo kwa hiyo nao wawe wamejengewa uwezo wazijue vizuri hizi sheria ili waweze kutetea haki zao. Kwa sababu hii CSR ukisoma Sheria ya Kodi ya mwaka 2004, kifungu cha 16 kinatumika katika kufanya assessment ya kodi zingine. Wanaotoza kodi wanaangalia mchango wake alioutoa kwenye hizo CSR kwenye jamii. Kwa hiyo, sio hisani kama ambavyo tunadhani, wale wanasheria wa Halmashauri Waheshimiwa Madiwani na wakuu wa idara wajengewe uwezo ili waweze kujiamini. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naomba sana tumsikilize mchangiaji hata ninyi mkisikiliza kwa masikio yenu mtaona kuna haja ya kupunguza sauti.

Endelea Mheshimiwa Kamonga.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunilinda. Naomba hizi sheria nzuri ambazo zinalinda rasilimali zetu ziweze kutolewa elimu na wananchi wajengewe uwezo ili kuandaliwa na miradi mikubwa ambayo inakwenda kwenye maeneo yao waweze kujua haki na wajibu wao na waweze kutetea haki zao. Vinginevyo wananchi wataendelea kutembea kwenye ardhi tajiri lakini wao wataendelea kuwa maskini. Kwa hiyo, hivi ni vitu vya muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nimuombe Mheshimiwa Waziri atoe tamko juu ya wachimbaji wadogo ambao waliomba vitalu vya makaa ya mawe pale Ludewa kwa sababu soko ni kubwa, rasilimali hizi zipo tumeendelea kuziangalia tu kwa miaka mingi. Ndiyo hayo sasa tunasema kama rasilimali hazitunufaishi hizo sio rasilimali tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wachimbaji wadogo wako tayari na masoko wanayo, kuna wachimbaji wengine wazalendo kama Kampuni ya Maganga Matitu na kuna vikundi kule niliwatembelea wengine nimeona wanachimba copper kwa kutumia nyundo na tindo. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie namna ya kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kukuza mitaji yao, ikiwezekana kuwapa vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)