Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Vilevile, naipongeza sana Wizara kwa kazi nzuri waliyofanya ya kuifikisha sekta yetu ya madini hapa tulipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natajikita zaidi kwa wachimbaji wadogo. Wachimbaji hawa wana mchango mkubwa sana kwenye sekta ya madini na kwenye pato la Serikali kwa jumla. Kama ilivyoelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukiangalia upande wa madini ya dhahabu, wachimbaji wadogo wamechangia asilimia 30; kwa kweli nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, nawapongeza sana wachimbaji wadogo kwani ndiyo wagunduzi wakubwa wa madini ndani ya nchi yetu, pamoja na kwamba hawana vifaa. Migodi yote inayochimbwa karibuni wamegundua wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji hawa wadogo tunatakiwa tuwashike mkono, Serikali pamoja na Wizara tutafute namna sahihi ya kupata mikopo yenye riba nafuu. Napenda kuyashauri mabenki yatafute namna ya kuzungumza na wachimbaji ili wajue hasa sekta inakwendaje, kwa sababu inaonekana hawaamini kuwakopesha wachimbaji wadogo, lakini nina imani wakikaa kwa pamoja watakuja na namna sahihi ya wachimbaji hawa kuweza kupata mikopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawakaribisha mabenki kwenye Jimbo langu la Handeni Vijijini, tuna vijiji zaidi ya kumi ambavyo vinachimba dhahabu; vijiji zaidi ya saba vinachimba feldspars; vijiji viwili vinachimba dolomite. Kwa hiyo, tuna vijiji zaidi ya 30 ambavyo vina madini mbalimbali, mabenki waje tukae nao tutafute namna sahihi ya kuweza kuwakopesha wachimbaji wadogowadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwa upande wa GST. GST inatakiwa itoe mchango mkubwa kwenye kuangalia wapi pana madini na kwa kiasi gani. Katika Jimbo langu la Handeni Vijijini, tuna madini ya chuma, graphite na dhahabu lakini wachimbaji wale hawawezi kujua chuma kile tulichokuwa nacho pale kiko kingi kiasi gani au graphite ile iko nyingi kiasi gani. Vilevile hii ni faida kwa Serikali kwani tukijua tuna graphite kiasi gani na tuna madini ya chuma kiasi gani, tunaweza kujipanga tuone tufanyeje kwa sababu kupanga ni kuchangua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la uongezaji thamani madini. Jambo hili tukilitumia vizuri litatusaidia sana kwenye upande wa ajira za vijana wetu, kwani uongezaji thamani madini siyo lazima madini ya dhahabu au almasi peke yake, kuna madini ya viwandani ambayo yanaweza kutumika kutengeneza vitu mbalimbali. Kwa mfano, insulators za umeme na vito mbalimbali, nina maana vipuri vya akina mama vinaweza kutengenezwa kutokana na madini ya feldspars.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwa mfano nchi ya China, utakuta insulators zinatengenezwa na viwanda vidogo sana, ni kama SIDO type. Kwa hiyo, tukiweza kutafuta ujuzi tukawapa watu wetu ujuzi, kama vile ambavyo imefanyka kwenye vikundi vya akina mama na vijana kupewa ujuzi wa kutengeneza sabuni na batiki, basi tukatengeneza namna vijana wakapata ujuzi wa kutumia malighafi hii ya madini ya viwanda, itatusaidia sana kuongeza ajira kwa vijana wetu na kuongeza pato la madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)