Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu lakini nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunajadili Wizara ya Katiba na Sheria ambayo ndiyo msingi wa Taifa letu. Nchi yetu inaongozwa na misingi ya Katiba na Sheria ambayo kila mmoja wetu anapaswa kuifuata na kuiheshimu. Hii ni Katiba ambayo sisi sote humu ndani tuliapa kuilinda na kuiheshimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu kuna mambo ambayo binafsi nadhani sio sawa kuendelea kufanyika. Nikaanza kujiuliza, je, ni watu gani au chombo gani ambacho kina mamlaka ya kuzitumia sheria na kutoa hukumu? Wapo baadhi ya viongozi wa Serikali wanatumia sheria, wanatoa hukumu mikononi mwao pasi na kuheshimu Katiba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona namna gani baadhi ya watu wanavyodhalilishwa na baadhi ya viongozi wa Serikali. Tunaona kuna baadhi ya viongozi wa Serikali wanawadhalilisha kwa kuwapiga bakora watumishi wengine wa Serikali. Sidhani kama viongozi hawa wamepewa mamlaka, ni kwa sababu wameshindwa kuheshimu Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi kwenye mitandao, tuliona Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa mmoja…

MBUNGE FULANI: Wa Wilaya.

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nazungumzia Mkuu wa Mkoa kule Zanzibar, acha huyu Mkuu wa Wilaya huku, anampigisha pushup mtumishi wa Serikali mbele ya vyombo vya ulinzi na usalama likiwemo Jeshi la Polisi halafu tunakaa tunasema tunaheshimu Katiba wakati wao ndiyo wanaoivunja Katiba hii. Mimi nitoe rai kwamba ipo haja kwa viongozi hawa kupewa elimu juu ya Katiba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kusema tuna kila sababu sisi Wabunge kuhimizana na kuheshimu mihimili mikuu ya Serikali. Mhimili Mkuu wa Bunge sisi lazima tuwe na kazi moja tu ya kutunga sheria. Mhimili mwingine ambao ni wa Mahakama, tuipe kazi yake ya kutafsiri sheria na Serikali kwenda kutekeleza sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu Serikali ilione hili juu ya watu hawa wanaowadhalilisha wananchi jambo ambalo halikupaswa kuwa hivyo. Walitakiwa wawachukue wapeleke polisi na polisi ifuate taratibu nyingine za kisheria. Ndiyo utaratibu kwa mujibu wa Katiba hii, tukiiangalia ukurasa wa 92 Ibara ya 107A inasema: “Mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji wa haki katika Jamhuri ya Muunganoo itakuwa ni Mahakama na siyo Mkuu wa Mkoa wala Mkuu wa Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Katiba na Sheria. Tunafahamu kwamba utaratibu na mwenendo wa kesi umeandaliwa sheria zake lakini tuna kundi kubwa la watu ambao kesi zao ziko ndani ya upelelezi. Sasa tufike mahali uletwe Muswada wa sheria Bungeni tubadilishe baadhi ya mambo. Hatuwezi kila siku tukasema upelelezi unaendelea, miaka nane, tisa hadi kumi wakati hao ambao upepelezi wao unaendelea wameacha familia, tunawaathiri kisaikolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tufahamu sasa Taifa letu leo linapiga vita chokoraa, wana Watoto, nini faida yetu, wale watoto watakuwa chokoraa. Wameacha wake, wale wake watakuwa wajane. Taifa linahitaji uchumi, wale ambao tumewaweka ndani upelelezi wao unaendelea Taifa litakosa mapato kwa sababu baadhi yao walikuwa ni wafanyabiashara na kila Mtanzania anachangia mapato ndani ya Taifa hili. Naomba sana tutumie fursa tuliyonayo kupitia Bunge hili na vyombo vyenye mamlaka ya kubadilisha sheria, tulete Muswada tubadilishe sheria tuweke ukomo wa upelelezi, tusiende tu kama tunakata kamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kuchangia, tuna Katiba mbili; Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Zanzibar. Ibara ya 93 ya Katiba ya Zanzibar imeeleza kwamba Zanzibar ina Mahakama Kuu na tukirudi kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeelezea kwamba nako kuna Mahakama Kuu, kila Mahakama inajitegemea, inafanya kazi pasi na kuingiliwa na Mahakama nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya kusikitisha, hali ya maajabu tunaidhalilisha nchi yetu na tunaonekana si watu wenye kufuata Katiba. Leo Mahakama upande mmoja inaingilia Mhimili wa Mahakama nyingine. Wako baadhi ya watu wametoka upande mmoja wa Zanzibar wameshtakiwa, kesi zao wamehamishiwa Mahakama Kuu ya Bara. Naiomba Serikali ikija hapa ieleze Bunge hili na Watanzania ni mamlaka gani ambayo imepewa Mahakama Kuu ya Bara kuingilia Mhimili wa Mahakama Kuu ya Zanzibar watuhumiwa wa Zanzibar kushtakiwa Mahakama Kuu ya Bara. Tuelezeni kwa ufanisi kabisa ili tufahamu na wananchi wetu wajue kwamba kumbe Mahakama Kuu ya Bara ina uwezo wa kusikiliza kesi ya Mahakama Kuu ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nishukuru sana kwa kunipa nafasi hii na niwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Chonga kwa kuniamini kwamba naweza kuwatumikia. Ahsante sana. (Makofi)