Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami nichangie kidogo hii hoja ambayo iko mbele yetu. Niwapongeze Mawaziri kwa kazi yao nzuri, lakini ninazo hoja mbili. Nitaongelea Sheria ya Bima, tunapoisoma pamoja na Sheria ya Usalama Barabarani. Sheria ya Bima hasa inapokuja kwenye makosa yanayotokana na ajali za barabarani, inayo matatizo makubwa sana na ukiisoma hii sheria ya bima, ajali inapotokea barabarani, Jeshi la Polisi watakwenda watapima, kesi itapelekwa mahakamani, tutasubiri hukumu itoke na wote tunajua, ni mashahidi hukumu zetu zinachukua muda gani! Hukumu ikishatoka yule muhanga wa ajali ya barabarani ndio anaweza akaambatanisha ile hukumu kwenda kudai fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa ni kwamba anapokwenda kudai ile fidia, Sheria ya Bima iko kimya anakwenda kulipwa kiasi gani, ni maamuzi ya kampuni ya bima. Tumeshuhudia ndugu zetu wengi wakipoteza maisha yao kwa sababu, ajali inapotokea baadhi ya familia zetu tunazijua ni masikini, hawana hata pesa ya kumtibia huyu muhanga wa ajali ya barabarani. Wanaanza kuchangishana ukoo mzima ili kupata hela ya kumpeleka hospitalini. Anapokwenda sasa kudai ile fidia/compensation ambayo inalipwa na kampuni ya bima, anakwenda pale wanamwambia tunakupa shilingi laki tano. Ni maamuzi ya kampuni ya bima ndio inaamua amlipe kiasi gani, mtu ametoka Kagera na tunajua makampuni makubwa ya bima yapo Dar es Salaam au hapa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anatoka Kagera analipa nauli anakwenda Dar es Salaam anaambiwa tunakupa shilingi laki tano, hatuwatendei haki watu wetu. Niwaombe Sheria ya Bima ya Tanzania itoe kima au kiwango cha chini, ambacho mtu anapopoteza maisha katika ajali ya barabarani anapaswa kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria nyingine si kwamba hatuna mifano, tunayo mifano. Usafiri wa anga mtu anapokufa akiwa kwenye ndege, sheria zetu pamoja na kanuni za TCAA za usafiri wa anga za mwaka 2008 zinatoa kima cha chini ambacho mtoa huduma anapaswa kumlipa muhanga wa ajali anapokuwa kwenye ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma regulation 24 ni 120,000 USD tunajua hiyo hatuna shida nayo. Lakini usafiri wa majini, nayo ukisoma Shipping Merchant Act kipengele cha 352 kimetoa kima cha chini ambacho muhanga wa ajali ya usafiri wa majini anapaswa kulipwa endapo atapata kifo au ajali au kupoteza mali zote akiwa kwenye meli.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo Sheria ya Usafiri wa Majini (Merchant Shipping Act), ukiisoma ni kichekesho tu, haitekelezeki. Niwaombe Tume ya Kurekebisha Sheria; twenda tukaipitie hiyo Sheria. Unaposema mtu akifa kwenye meli anapaswa kulipwa units wanasema laki 333 units of account nikalifuatilia kuangalia hizi laki 333 units of account maana yake ni nini? Nikaenda kupata kwamba hizo ni sawasawa na one special drawing like the SDR. Na SDR moja ni sawasawa na Euro moja, ni kampuni gani ya Kitanzania inayoweza ikalipa hizi fedha? Haipo!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, na Sheria hiyo tunayo, likitokea la kutokea, hatuwezi kuya-enforce kwasababu ya ugumu wake. Lakini tunajua kwamba hii Sheria ukiisoma na Sheria ya Australia ni cut and paste. Kwa hiyo, niiombe Tume ya Kurekebisha Sheria ipitie hii sheria iweze kuiweka katika viwango ambavyo ni vya kitanzania ambavyo ikitokea ajali hii inaweza ikalipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudi kwenye masuala la ajali za barabarani. Naomba niishauri wizara, twenda tukapitie Sheria ya Bima tuioanishe na Sheria ya Usafiri wa Barabarani Road Traffic Act, tuje na mapendekezo au kiwango ambacho kinahimilika ili watanzania wenzetu wanapopata ajali waweze kulipwa kama sheria inavyosema to compensated adequately lakini sheria ilivyo hatuwatendei haki Watanzania. Tusiyaachie Makampuni ya Bima yaamue juu ya maisha ya Watanzania wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa ushauri mwingine kuhusiana na hii, wananchi wetu wanapopata ajali wakati wanasubiri kesi iende mahakamani ihukumiwe, hapa katikati hatuna chombo cha kuwahudumia tunajua wengi hawawezi kujihudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri wizara tuunde chombo ambacho kitachangiwa na makampuni yote ya Bima mtu anapopata ajali leo, kile chombo kitoe fedha zikamuhudie huyu mhanga wa ajali wakati tunasubiri Shirika/ Makampuni ya Bima kumlipa, atakapolipwa zile fedha ambazo tutakuwa tumempatia kumuhudumia basi tutazikata kurudisha kwenye mfuko ambao nashauri na kupendekeza uundwe chini ya sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo janga lingine, tunayo Sheria ya TASAC. Tulitunga hapa Bungeni lakini ukiisoma leo katika mazingira ambayo leo tunasema tunakwenda kujenga uchumi shindani; ile sheria ni janga la Kitaifa. Nashauri hii sheria tukaipitie upya, haileti ustawi wa sekta binafsi kwenye usafiri wa majini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema TASAC ni mdhibiti na tunajua udhibiti tulionao Tanzania tuliochagua kuuchukua ni udhibiti wa pamoja; lakini TASAC yenyewe ukiiangalia imeunganisha shughuli za kiudhibiti na shughuli za kutoa huduma. Huwezi ukawa referee wakati huo huo unacheza mpira uwanjani ni makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza na kushauri, shughuli za kiudhibiti ambazo ziko chini ya hii sheria zitenganishwe tuwe na mamlaka na chombo ambacho kinaangalia masuala ya udhibiti wa usafiri wa majini na tuwe na kampuni ambayo itatuangalizia kwa nia ileile ambayo tulikuja na hii sheria ya TASAC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua zamani tulikuwa na NASACO, turudishe mfumo uleule lakini tuwe na chombo ambacho kinafanya kazi ya udhibiti peke yake na chombo ambacho kinafanya biashara. Na misingi ya udhibiti, mdhibiti ana hadhi ya kimahakama na hawa wengine wote ambao wanafanya zile shughuli wanapokuwa na matatizo wanakuja kwa mdhibiti ili akawapatie suluhu ya matatizo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunapokuwa na Taasisi ambayo kimsingi ni mdhibiti, ni mahakama, lakini na yeye anafanya zile shughuli inakuwa ni kinyume na utawala bora inapokuja kwenye kusuluhisha matatizo yanayojitokeza kwenye hiyo sekta. Niiombe Tume ya Kurekebisha Sheria, iiangalie hii sheria; badala ya kuleta ustawi nadhani maoni yangu inakwanza ustawi wa sekta hii ya usafiri wa majini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache naomba niunge hoja mkono. (Makofi)