Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kukushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia katika Bajeti hii ya Wizara ya Katiba na Sheria. Nianze kwa ku-declare interest, mimi ni mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria na hivyo nianze kwa kuipongeza Wizara hii ambayo imefanya kazi kubwa sana katika kuboresha miundombinu ya mahakama. Mahakama zimejengwa, mahakama jumuishi zinazojali haki za binadamu usawa wa kijinsia na haki za watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia, nizidi kupongeza Taasisi zote zilizo chini ya Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya. Tunatambua kwamba, wamekuwa na mifumo mingi ambayo imeanzishwa ikiwemo mifumo ya mitandao, mahakama za kimtandao ambayo itasaidia sana sana wananchi wetu kwenye suala zima la upatikanaji wa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze mchango wangu wa leo kwa kutoa tu ushauri. Langu leo ni ushauri. Kila kinachofanyika kwenye nchi hii ni katika misingi ya sheria na kanuni, maana yake sisi wote tuko hapa leo kwa sababu kuna sheria au kuna kanuni inaturuhusu kuwepo hapa na kufanya haya tunayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa mfano wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali au CAG. Ofisi hii imepewa mamlaka chini ya Ibara ya 143 ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ofisi hii kazi yake au jukumu lake kubwa, ni kudhibiti na kukagua mipango yote na matumizi ya pesa za Serikali katika Taasisi zote kuona kama zinatumika kama mipango yote ilivyowekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wote na sisi Wabunge tunakuwa tuna imani kwamba, kila kitu kinakwenda sawasawa pamoja na mipango yote ya pesa mpaka tutakapopokea ripoti hii ya huyu Mkaguzi, ituonyeshe either kuna sehemu pesa hizi hazikutumika vizuri au kuna sehemu zilipelekwa kinyume na utaratibu au kuna sehemu zimetumika vizuri au kuna sehemu labda tunapata hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoa mfano huu, lakini sasa nirudi katika Wizara hii ya Katiba na Sheria. Inabidi tujiulize ni chombo gani, Taasisi gani au ni mtu gani mwenye mamlaka ya ku-assess whether sheria tunazotunga kama Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinatekelezwa sawasawa na maelekezo ya sheria hizo. Pia ni Tume gani inayoangalia kwamba, sheria hizi either zinakuwa zinawapa haki wananchi, au zinawakandamiza, au sheria imekuwa short kwa kitu fulani tuiongeze wigo sehemu fulani au tuipunguzie mamlaka sehemu Fulani. Pia tunaweza kuona kwamba, Tume fulani iliyotengenezwa kwa mujibu wa sheria inafanya kazi zake sawasawa au haifanyi kazi zake sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba, jukumu la kutunga sheria lipo ndani ya Bunge hili Tukufu, lakini kuna principle ya natural justice inayosema kwamba, you cannot be a judge of your own case. Ni chombo gani kinachotuonesha kwamba sheria tulizopitisha sisi kama Bunge, zinafanya kazi yake sawasawa au zinafuatwa sawasawa kule nje. Tunatambua kwamba, kuna chombo ambacho ni mahakama, mhimili ulioanzishwa kwa ajili ya ku- enforce sheria hizi, lakini mahakama tunatambua wote kwamba, haiwezi ika-move on its own motion lazima iwe moved na mtu, either kuna mgogoro umetokea au kuna mtu anaenda kutafuta tafsiri ya sheria mahakamani. Vile vile tuangalie je, kuna sheria ngapi ambazo tumezitunga leo hii ni source ya grievance nyingi sana kwenye jamii yetu na si wote tuna nguvu ya kwenda mahakamani kufungua kesi kwa ajili ya kupata tafsiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba, Bunge hili mwaka 1980 lilitunga Sheria ya kuanzisha chombo kinachoitwa The Law Reforms Commission, ambacho kimsingi majukumu yake ni haya sasa; ya kuonesha kwamba, sheria zinazotungwa zinaendelea kuendana na wakati? Au sheria zinazotungwa zinatekelezwa sawasawa wapi tuongeze, wapi tupunguze maana yake kulishauri Bunge na Serikali sheria zetu ziendeje?

Mheshimiwa Naibu Spika, chombo hiki nasukumwa kusema bado hakijafanya kazi yake sawasawa, aidha kuna upungufu wa bajeti au kuna upungufu kwenye utendaji wa chombo hiki au composition ya chombo hiki. Nitoe mfano, kuna sheria kwa mfano, sheria inayo-deal na Bodi ya Mikopo. Kuna mambo mengi sana ambayo Wabunge wengi wamesimama na kuzungumza juu ya Sheria hii ya Bodi ya Mikopo. Suala zima la kupandisha interest kutoka asilimia nane (8) kwenda 15. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chombo hiki kingekuwepo hili lilikuwa ni jukumu lake la ku-assess na kuihoji Serikali kwamba, justification ya kutoa asilimia nane interest kwenda 15 imepatikana wapi? Je, kima cha chini cha mshahara wa Kiserikali tukitoa asilimia 15, tukatoa PAYE, tukatoa makato ya NSSF au PSSSF kinamtosha kijana kuweza kumudu maisha yake na ndio maana tukatoa nane kwenda 15? Pia, chombo hiki kingekuwa na mamlaka ya kuihoji Serikali katika utungaji wa sheria hii, ni wapi wamepata justification ya kuweka asilimia sita kama retention fee ya mikopo hii, wakati tunajua kwamba inflation ya pesa yetu katika nchi yetu mwaka 2019 tulikuwa na 3.4 percent, 2020 tulikuwa na 3.2 na mwaka 2021 mpaka Machi tumekuwa na kama 3.2 mpaka sasa Machi mwaka huu, lakini wenyewe tumewekewa asilimia sita kama kulinda thamani ya pesa hii, justification hii imetoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, justification nyingine ya kuweka grace period ya miaka mwili ndio mtu aanze kulipa, je, tumekusanya takwimu za kututosha ili kuona kwamba katika nchi hii kijana akihitimu ana window ya miaka miwili tu atakuwa amepata ajira! Kuna watu wanakaa mpaka miaka saba mpaka 10 hawajapata ajira. Maana yake chombo hiki kingekuwa na uwezo wa kuhoji utekelezaji wa baadhi ya sheria, ikatupa maoni yake na kikawa na nguvu na ripoti hizi zikaletwa Bungeni tukazijadili na zikatumika kama ushauri wa moja kwa moja kuli-guide Bunge na kui-guide Serikali namna gani tunarekebisha sheria zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe mfano wa mfumo mzima wa upatikanaji wa haki hasa kwenye mfumo wa makosa ya jinai. Mahakama zetu zina mamlaka ya kutoa hukumu ya mwisho, lakini hazina mamlaka ya ku-guide namna gani uchunguzi au investigation zinafanyika kule kwenye hizi kesi zetu. Kwa hiyo, unakuta kuna kesi inakaa miaka miwili, mitatu, minne au mitano bado uchunguzi unafanyika, aidha mtu yuko ndani au yuko nje, lakini anazidi kupoteza muda wa msingi wa kuwa anahudhuria mahakamani kila siku na haki yake haijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chombo hiki kingekuwa na mamlaka ya moja kwa moja kutuonesha kwamba, wapi turekebishe, wapi tuongeze nguvu katika mahakama zetu ili ziweze kusukuma vyombo vya kufanya uchunguzi wa haraka. Chombo hiki kingetuonesha kwamba kwenye sheria labda kuna makosa tuweke time limit investigation, ili iwabane watu wale wafanye uchunguzi kwa muda mfupi ili haki za watu ziweze kutendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yote hii ni kuonesha kwamba chombo chetu cha Law Reforms Commission kipo na majukumu yake yapo kisheria lakini hakijafanya kazi yake sawasawa. Mmigogoro mingi inayotokea kati ya Serikali na wananchi ni katika utekelezaji wa sheria. Sheria zetu zipo, ndio kuna baadhi zina upungufu lakini zile ambazo zipo sawasawa, labda hazitekelezwi sawasawa huko kwenye jamii zetu. Chombo hiki kingekuja na ripoti ya kila mwaka kama sheria inavyosema, ili kutueleza kwamba sheria hizi ziko hivi, lakini hazitekelezwi na wapi turekebishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefuatilia, ni muda wa miaka mingi sana tangu chombo hiki kitii takwa la kisheria la kuleta ripoti yake kwenye Bunge hili Tukufu. Nimekwenda kwenda Kitengo cha Hansard wameshindwa hata kupata record halisi ya lini ripoti imepokelewa hapa Bungeni, kitu ambacho ni kinyume cha sheria. Ripoti ya CAG inapokelewa kila mwaka na inatu-guide kama Serikali kuona kwamba wapi mapato yetu hayakwenda vizuri, wapi turekebishe, wapi tufanye vizuri zaidi. Kwa hiyo, naishauri Wizara hii ya Serikali kuangalia namna ya kukifufua chombo hiki, aidha tukifumue tukiweke sawa ili kipate nguvu ya kuwa kinaleta ripoti katika Bunge hili Tukufu, ili tuweze kuona utekelezaji wa sheria unakwenda kama ambavyo sheria zetu zimetungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa niipongeze tena Wizara hii, kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yake ambao unaendelea kufanyika na tunaamini kwamba kama Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025 inavyotuelekeza, hasa katika ukurasa wa 167 upatikanaji wa haki utaendelea kuwepo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)