Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi)

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba ya Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninapenda tu niishauri Serikali yangu kwamba suala la watumishi wa umma kwenye Wizara ya Afya na Elimu ni muhimu sana, kwa sababu tunapozungumzia maendeleo ni lazima tuhakikishe kwamba wananchi wetu wana afya njema. Kwa hiyo, watumishi wamepungua sana kwenye maeneo hayo kwa hiyo wapelekwe watumishi wa kutosha na kwamba tumesikia juzi kwamba kuna ajira mpya ya kwenda kwenye maeneo hayo. Basi ajira hizo zifanywe kwa wepesi kwenye maeneo hayo (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, demokrasia, tunazungumza suala la demokrasia katika nchi yetu, tunamshukuru Mungu sana nchi yetu imeendelea kuwa vizuri zaidi kwenye masuala ya demokrasia na ndio maana maendeleo yanazidi kupaa kwa kasi katika nchi yetu ya Tanzania. Niseme tu hapa mimi nitazungumzia kidogo kwenye suala la ukatili wa kijinsia. Kumekuwa na ukatili wa kijinsia hasa kwa Wabunge wa Viti Maalum wa vyama vyote tunapokuwa tunawajibika kwenye maeneo yetu kutekeleza wajibu wetu kama Wabunge wa Viti Maalum, tumekuwa tukinyanyapaliwa, tukinyanyaswa na Wabunge wenzetu wanaume kwa maana ya hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hasa pale ambapo Mbunge wa Viti Maalum anatoka Jimbo moja na Mbunge wa Jimbo hilo, wanakuwa na wasiwasi hofu yao ni kwamba Mbunge wa Viti Maalum akifanya kazi eneo hilo maana yake mwisho wa siku atapata mileage na kwamba anaweza akagombea Jimbo. Mimi niwaombe tu ndugu zetu Wabunge wenzetu kwamba sisi sote tunajenga nyumba moja mtupe nafasi tufanya kazi kwenye maeneo yote bila kutuwekea vipingamizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii unyanyapaa huu sasa hivi umekuwa ukiota mizizi, tumekuwa tukitishiwa, tunaambiwa maneno makali na hata wakati mwingine kutudhoofisha ili tusiweze kufanya kazi. Niombe sana Mheshimiwa Rais jana ametoa hotuba nzuri sana, kwa hiyo niseme tu kwamba tunamsubiri mama yetu akabidhiwe kijiti kwenye chama, sisi kama Wabunge wa Viti Maalum tunaopitia Chama cha Mapinduzi tutakwenda kwake ili atusaidie namna gani tuweze kufanya kazi ili kukomesha huu unyanyapaa kwa Wabunge Wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda kwenye masuala ya biashara. Juzi juzi; ni wiki tatu tu baada ya kifo cha aliyekuwa Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tumesikia hotuba ya Mwenyekiti mmoja ambaye ana Mbunge mmoja wa chama chake ndani ya Bunge, lakini ana Wabunge 19 wa Viti Maalum akizungumzia kunyanyaswa na kufanyiwa vitu tofauti dhidi ya biashara zake. Sasa nataka Watanzania watege masikio ninataka niwaeleze ukweli juu ya masuala mazima yanayohusiana na Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivi kwa sababu ile ameizungumza hadharani na amehutubia katika …, kwanza inasikitisha sana muda mfupi tu baada ya Rais wetu kufariki badala ya kuja aeleze katika maelezo yake na masikitiko yake angeeleza hata baadhi ya kazi nzuri ambazo amezifanya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, badala yake ameeleza kinyume chake, lakini hatumshangai ni kwa sababu alikuwa anatetea tumbo lake. Niseme tu alieleza kwamba Serikali ilimfanyia ukatili wa kuzuia biashara zake na kuzifunga.

Mheshimiwa Spika, ukweli uko hivi, katika biashara yake yeye zile biashara anazozifanya ni za urithi wa kifamilia, na kwa kuwa ni za urithi wa kifamilia yeye amejimilikisha kama za kwake na kwamba hatoi mrejesho kwa ndugu zake, kwa hiyo ndugu zake wakaenda mahakamani, walivyokwenda mahakamani wakataka haki itendeke. Mahakama ikatoa amri ya kufunga biashara zake ili asiendelee na biashara mpaka mgogoro utakapokwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii anakuja anawadanganya Watanzania, anatafuta kuendelea kujipambanua kisiasa na wananchi wamwamini, hii si kweli na haikubaliki. Kwa hiyo, arudi akamalize mgogoro na familia yake asisingizie Serikali kwa imemnyanyasa na kumfungia biashara zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kuna jengo la Bilcanas lile jengo lilikuwa ni la Serikali la National Housing. Amekaa pale miaka na miaka halipi kodi anapenda vitu vya bure. Serikali ilipokuja kudai kodi analeta blaa blaa, Serikali iliyokuwa inaongozwa na Dkt. Magufuli ilikuwa haitaki blaa blaa na hata hii sasa inayoendeshwa na Mama yetu Samia Suluhu Hassan nayo haitaki blaa blaa. Asiyelipa kodi akae pembeni. Kwa misingi hiyo… (Makofi)

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani kuna Taarifa. Mheshimiwa Aida Khenani.

T A A R I F A

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa Taarifa mzungumzaji lakini pia niombe kiti chako kituongoze. Mimi ni Mbunge wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo - CHADEMA, kinachozunguzwa hapa ni Wizara ya Utumishi, kuzungumzia maisha ya mtu binafsi ndani ya Bunge ambaye hawezi kujibu, tena hazungumzii mambo ambayo yanayohusu mjadala uliopo anazungumza maisha yake binafsi, tuna Kanuni zetu niombe utaratibu wa kiti chako utuongoze. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kwanza umesimama kwa Kanuni ya Taarifa, na Taarifa huwa anapewa mzungumzaji sio mwongozo wa kiti, lazima na wewe uwe umezitazama Kanuni vizuri. Na umesema vizuri hoja iliyopo mezani ni ya Utumishi na Utawala Bora, na Kanuni zetu zinaruhusu mtu ambaye alijadiliwa humu ndani kama anaona kile alichojadiliwa amevunjiwa heshima ama hakijawekwa kwa namna ambayo ni uhalisia, Kanuni zetu zinaruhusu namna yeye anavyoweza kuleta malalamiko. (Makofi)

Sasa Mheshimiwa aliyekuwa anachangia, mimi huwa nasikiliza hapa kila neno linalozungumzwa nasikiliza, Mheshimiwa anayechangia anasema huyu aliyetajwa alisema hoja hizo kuonesha nchi hii haina utawala bora na hoja iliyoko mezani inahusu utawala bora. (Makofi)

Kwa hiyo yupo sahihi kwa mchango wake, lakini kuhusu taarifa anazozisema kama kuna mtu humu ndani anafikiri anasema uongo asimame kwa kanuni inayosema kama Mbunge anazungumza uongo. Na kama yeye akisema uongo kuhusu huyo mtu Kanuni zetu zinaruhusu ataleta malalamiko yake kwa Mheshimiwa Spika utaratibu wa kawaida utachukuliwa kama huko nyuma ambavyo imewahi kutokea.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana bado dakika zangu sita naendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapinzani wamekuwa wakiitupia sana Serikali malalamiko juu ya matumizi ya fedha za umma, ni jambo jema, lakini tunapozungumza usawa na kuangalia namna ya uwasilishaji wa mambo yenyewe ni vizuri sasa wewe mwenyewe unayewasilisha jambo hilo ukajitazama kwanza, wanasema tazama kibanzi cha jicho lako kabla hujamuonesha mwenzako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa misingi hiyo nataka niseme Chama cha Demokrasia na Maendeleo tunataka watueleze miaka mitano iliyopita fedha za ruzuku wamefanyia nini? Wamekuwa wakilipwa shilingi milioni 310 huyo Mwenyekiti huyo aseme shilingi milioni 310 kila mwezi, nimekokotoa vizuri nikapiga mara miezi 12 na mara miaka mitano nikakuta kwamba ni shilingi bilioni 18.6 ambazo chama hiki kimepelekewa pesa hiyo na kwamba katika utekelezaji wa majukumu yao dhidi ya ruzuku hii hawajajenga hata jengo moja ambalo lingewasaidia sasa kuonyesha taswira nzima ya chama chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ikapelekea kwamba walishindwa kufanya uchaguzi kwa sababu hawakuwa na pesa, badala yake wakaja wakaanza kusema kwamba uchaguzi…

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …haukuwa wa haki haukuwa huru. Wewe ndugu yangu umekaa kwenye kiti tulia mambo yaendelee, wenzako wako nje huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme sasa…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani subiri kidogo.

Mheshimiwa Aida Khenani umeshatoa Taarifa kwa Mbunge huyu tayari wakati anachangia, labda usimame kwa Kanuni nyingine. Umeshatoa taarifa kwa Mbunge huyu anayechangia, Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, na Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe alipoona ameshafilisi kabisa chama chake akaamua kumsusua Tundu Lissu uchaguzi na kwamba sasa Tundu Lissu akawa anafanya peke yake, lakini ofisi hawana, lakini pia Mheshimiwa ….

Mheshimiwa Naibu Spika, bado dakika zangu tatu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa David Kihenzile anasema ameshamaliza kuongea, kwa hiyo huwezi kumpa Taarifa Mbunge ambaye ameshamaliza kuzungumza ahsante sana. Ahsante sana.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Ameshamaliza?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Aida Khenani hamna Mbunge anatoa taarifa zaidi ya mara moja kwa mtu mmoja, tafadhali. Mbunge unapotoa taarifa kwa Mbunge huwezi kuwa mnajibizana ninyi, ukishatoa taarifa umeshatoa mwambie jirani yako asimame ampe hiyo taarifa.

Waheshimiwa Wabunge tunaendelea. Umesema umemaliza Mheshimiwa ndiyo maana nimeikata ile taarifa nyingine kule ama nimesikia vibaya? Ulikuwa umemaliza au hapana?

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Alikuwa bado, bado hajamaliza Mheshimiwa.

NAIBU SPIKA: Waheshimwa Wabunge, tusikilizane nazungumza na Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani msimsaidie kujibu.

Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani nilizuia ile taarifa ya Mheshimiwa David Kihenzile nikifikiri umeshamaliza kuzungumza, si umeshasema unaunga mkono hoja. Mheshimiwa haya Mheshimiwa David Kihenzile.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ….

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa nilikuwa nataka kumpa Taarifa mzungumzaji kama viongozi wa chama fulani wametueleza mambo ya utawala bora kwa miaka mitano mfululizo na tumeshuhudia ndani ya chama kwa maelezo uliyotupatia. Nataka kumpa taarifa kuanzia sasa kwa kuwa pesa zimetumika zote hizo za ruzuku na hakuna chaguzi za ndani, wamekosa legitimacy na moral authority ya ku-question viongozi wa Serikali katika nchi hii kwamba hakuna utawala wa sheria. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge nadhani wote tunazo Taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali, ile taarifa ndiyo inayotuongoza kama huko kuna shida au hakuna shida. Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani malizia.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Kwa hiyo, Mheshimiwa yule mwenye Mbunge mmoja wa Jimbo Bungeni humu alienda kununua matrekta mawili, hayo matrekta mawili hayajulikani yaliko mpaka leo hii. Lakini amekuwa akizungumza kwenye maelezo yake kwamba kulikuwa na dhambi na ubatili mkubwa sana kwenye utawala wa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mama Samia; hii si kweli kwa sababu hawa watu kama ndivyo ina maana kwamba ubatili wao ni kujenga zahanati 1,900? Ubatili wao ni kujenga hospitali 400 zaidi? Ubatili wao ni kujenga hospitali za mikoa 10? Ubatili wao ni kujenga flyover? Ubatili wao ni kununua ndege? Ubatili wao ni kujenga barabara? Haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Nbu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)