Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango mingi na muhimu sana ambayo wameitoa katika mjadala wa bajeti hii na kwa muktadha huu katika eneo la TARURA na afya.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa muhtasari niweze kupita kwenye hoja mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa. Kwanza kwa takriban asilimia 99 ya wachangiaji wamegusa TARURA, wametoa ushauri na michango mingi sana muhimu ya kuhakikisha kwamba tunaiwezesha TARURA kutenda kazi kwa ufanisi mkubwa unaotarajiwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua sana kwamba tuna changamoto kubwa ya barabara zetu zinazohudumiwa na TARURA, lakini uhitaji mkubwa wa madaraja na makalvati, lakini inatambua kwamba pia tuna tatizo la changamoto ya bajeti ya TARURA. Serikali imeendelea kuweka jitihada za kuhakikisha kwamba tunaboresha sana bajeti ya TARURA kuiwezesha kuhudumia mtandao wa barabara ambao inahudumia. Kwa mwaka wa fedha uliopita shilingi bilioni 275 zilitengwa ikilinganishwa na shilingi bilioni 578 za mwaka wa fedha ambao tunaelekea, ongezeko la bajeti ya TARURA kwa zaidi ya mara mbili na nusu. Kwa hiyo hii ni dalili kwamba Serikali inatambua sana umuhimu wa kuiwezesha TARURA.

Mheshimiwa Spika, tunapokea mawazo na michango ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wametoa kuhusiana na kuboresha vyanzo vya mapato kwa maana ya simu, mafuta, lakini na maeneo mengine. Serikali itaendelea kuyafanyia tathmini na kuona njia bora zaidi ya kuongeza bajeti ya TARURA ili kuiwezesha kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wameongelea sana suala la kuona namna ambavyo vyanzo vya ndani vya halmashauri vitachangia ujenzi wa barabara kupitia TARURA na Serikali itatoa mwongozo kwa Majiji na Manispaa kuanza kutenga fedha kwa ajili ya kuchangia nguvu za TARURA kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kwa nguvu ni kuhusiana na vigezo vinavyotumika katika mgao wa fedha za TARURA katika halmashauri. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, Serikali inatambua kwamba halmashauri zetu zinatofautiana kwenye ukubwa wa maeneo na hivyo mtandao wa barabara, lakini hali za kijiografia, milima, tambarare na mvua. Hivyo, katika kuweka vigezo hivi, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali itapitia vigezo hivi, kwa sababu vigezo na mgao uliowekwa awali ulizingatia zile barabara za kilomita elfu 56 na sasa tunakwenda 108,000 na hadi 144,000. Kwa hiyo niwahakikishie kwamba hii itapitiwa vizuri na itakwenda vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya kuthibitisha Mameneja wa TARURA na ni kweli kama tunavyofahamu TARURA haina muda mrefu tangu imeanza na taratibu hizi za uteuzi wa viongozi wa Serikali kuna hatua mbalimbali zikiwemo za upekuzi kwa maana ya vetting. Niwape taarifa Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali imeendelea kufanya kazi hiyo na sasa imeshawafanyia vetting kwa maana ya upekuzi watendaji 111 kati ya 126, sawa na 88% na hawa hatua za kiutumishi za kuwathibitisha zitaendelea na zoezi hili ni endelevu.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ni suala la miradi hii kuchelewa kuanza na barabara mara nyingine kujengwa wakati wa msimu wa mvua. Serikali imeboresha sana utaratibu wa kupata zabuni kwa njia ya kielektroniki kwa maana TANePS. Katika mwaka wa fedha ujao tunatarajia miradi hii yote itatangazwa mapema, wazabuni watapatikana kwa wakati na barabara zitaanza kujengwa na kukarabatiwa kwa wakati na si wakati wa mvua.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili, maeneo ya madaraja na makalvati yamesisitizwa sana na Serikali imekwishatambua jumla ya madaraja 3,182 nchini kote, lakini pia makalvati 62,817 na imeweka mkakati ambao tutahakikisha labda kila baada ya mwaka wa fedha tunakwenda kutengeneza madaraja robo na makalvati pamoja na barabara za udongo kwenda changarawe.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la TARURA kwa ujumla wake Serikali itaendelea kuimarisha sana uwezo wa TARURA lakini pia kuuboresha sana mfumo wa utendaji wa TARURA ili kuhakikisha kwamba barabara zetu zinaboreshwa.

Mheshimiwa Spika, niende eneo la afya katika eneo hili Waheshimiwa Wabunge wamepongeza sana kazi kubwa ya Serikali ya kujenga na kukarabati miundombinu, hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati. Sisi kama Serikali tunaendelea na tunatambua kweli pamoja na kazi kubwa bado tuna mahitaji makubwa ya vituo vya afya na ndiyo maana katika mwaka wa fedha ujao, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Afya ametangulia kusema hospitali mpya 28 zimetengewa shilingi bilioni 14 zitaanza ujenzi, lakini hospitali za awamu ya kwanza 68 zitaendelea na ujenzi kwa bilioni 55.7, lakini pia hospitali 27 za awamu ya pili nazo zimetengewa bilioni 11.4.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la hospitali tunafahamu hospitali chakavu na kongwe tunakwenda kufanya tathmini na kuona njia bora zaidi kama ni kuzikarabati ama kuanza ujenzi ili ziweze kuwa na viwango bora. Vituo vya afya katika mwaka ujao tunatarajia kuendelea na ujenzi na ukamilishaji wa vituo vile vya afya 52, zimetengwa bilioni 15.6. Pia ujenzi wa vituo vipya 121, kuna shilingi bilioni 60.51. Jumla vituo vya afya 173 nchini kote kwa gharama ya shilingi bilioni 76.1, utaona ni kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, eneo la zahanati, tumetambua kwanza maboma Waheshimiwa Wabunge wameongelea suala la maboma ya zahanati ambayo wananchi wamechangia, tumekwisha yatambua maboma yote, mpaka Februari tulikuwa na maboma 2,350 na tayari katika mwaka huu wa fedha maboma 555 yametengewa shilingi bilioni 27.75 na tayari bilioni 20 zimekwishapelekwa, kazi za ujenzi zinaendelea, bilioni 7.75 zinaendelea na hatua za upelekaji kukamilisha maboma hayo.

Mheshimiwa Spika, mwaka ujao wa fedha maboma 758 yametengewa fedha kiasi cha shilingi bilioni 38.15 na hivyo tutakuwa tuna jumla ya maboma 1,313 ambayo tayari yatakuwa yanaendelea na ujenzi na ukamilishaji, tutabaki na maboma 1,037 ambayo tutaendelea kuyakamilisha kwenye mwaka mwingine wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la vifaa tiba dawa na vitendanishi, Mheshimiwa Waziri wa Afya ameeleza vizuri, lakini Serikali imeendelea kutenga fedha kwenye hospitali za Halmashauri. Hospitali 67 tayari zimeshapata bilioni 32.5, vituo vya afya tayari bilioni 26 mwaka huu, bilioni 15 tayari vifaa vimeshanunuliwa vinapelekwa, bilioni 11 hatua za manunuzi zinaendelea. Kwa mwaka ujao wa fedha bilioni 12.3 tunatarajia pia zitakwenda kununua vifaa tiba. Kwa hivyo tutahakikisha tunaendelea kuboresha vifaa tiba katika maeneo hayo. Dawa imeongelewa na Mheshimiwa Waziri wa Afya, tayari hatua za manunuzi ya dawa hizo zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kuongelea eneo la CHF, Mfuko wa Afya ya Jamii ulioboreshwa na eneo hilo ni kipaumbele cha Serikali, tumepanga kuwa na ajenda ya kudumu kwenye vikao vyote vya kisheria kuanzia ngazi za mitaa, vijiji, kata hadi ngazi za mkoa. Tumekwishahamasisha wananchi na utaratibu huu unaendelea wananchi 3,300,000 wameshajiunga na shilingi bilioni 19 tayari zimekwishakusanywa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.