Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Janeth Elias Mahawanga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya TAMISEMI. Kwanza niipongeze Wizara kwa wasilisho zuri na vipaumbele vizuri kabisa ambavyo kama vitaenda kutekelezeka nina uhakika tutapata matokeo chanya na changamoto zote kwenye jamii yetu zitakwenda kwisha.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwenye mikopo hii ya asilimia 10 ambayo wanufaika ni akinamama, vijana na walemavu. Lengo la Serikali kwa mikopo hii lilikuwa zuri sana lakini uhitaji ni mkubwa kuliko pesa yenyewe na hii inatokana na baadhi ya pesa inayotoka kuwa hairudi. Je, halmashauri zetu zinafanya tathmini ya kuangalia ni kiasi gani kimetoka na kiasi gani kimerudi na kwa nini hakijarudi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanufaika wa pesa hii kuna kitu wanakikosa ambacho ni muhimu sana, wanakosa elimu. Akina mama wengi ni wajasiriamali ambao wanafanya shughuli za kijasiriamali kama usindikaji wa vyakula, lakini wanafanya kwa elimu yao binafsi, kwa uzoefu wao wa kufundishana wenyewe kwa wenyewe. Ningeziomba halmashauri zishirikiane na taasisi ambazo zinaunga mkono juhudi za kuwainua wananchi kiuchumi, hasa wajasiriamali wa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano unakuta kuna matangazo ya SIDO yanayotoa elimu ya ujasiriamali hasa upande wa usindikaji, akina mama wengi wanatamani kwenda kusoma mafunzo haya lakini wanashindwa kutokana na kukosa ada. Halmashauri kama itaandaa utaratibu mzuri ikapata wadau kutoka SIDO, kutoka kwenye benki wataalam wa mambo ya fedha, wataalam wa masoko, wataalam wa fursa na wataalam wa kuongeza thamani ya bidhaa za wajasiariamali wadogo wakashirikiana na Maafisa Maendeleo na Madiwani wetu kwenye kata wakapita kwenye vikundi vile vya akina mama, vijana wakatoa elimu hii, nina uhakika itasaidia sana. Tunasema tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda, tunatafuta vyanzo vingine vya mapato, lakini nina uhakika kabisa mikopo hii ni chanzo tosha cha mapato kama tutawaongezea thamani ya ujuzi wanufaika hawa wakaweza kuwa wajasiriamali wakubwa wakalipa kodi, tutapata mapato kwenye Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kundi lingine la vijana ambao wanamaliza vyuo vikuu wako mtaani hawana kazi. Halmashauri ina uwezo kabisa wa kuangalia mikopo hii ya asilimia 10 ikachukua kundi fulani la vijana at least kundi moja kama kikundi kutoka kwenye kila halmashauri wakawapeleka kupata elimu. Kuna taasisi tano zimeungana ambazo ni SIDO, VETA, NSSF, Baraza la Uwezeshaji Uchumi Wananchi na Benki ya Azania, hawa wanatoa elimu baadaye wanatoa mikopo kwa ajili ya viwanda vidogo kuanzia milioni 50 mpaka milioni 500. Vijana wanaomaliza chuo wakichukuliwa na halmashauri, wakasimamiwa kupata elimu hii kwa kulipiwa huko SIDO au VETA wakaweza kufungua kiwanda wataweza kuajiri vijana wenzao, watatoka kwenye wimbi la kukosa ajira na mwisho wa siku watakuwa walipa kodi wataongeza mapato kwenye Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe halmashauri zetu zishirikiane na benki. Benki nyingi zina bidhaa nzuri sana kwa ajili ya wajasiriamali wadogo, lakini wajasiriamali wengi wanakosa taarifa. Kama halmashauri wataweza kushirikiana na hizi benki ambazo zinainua wajasiriamali wadogo zikapita kwenye kata zetu akina mama, vijana na walemavu wakapata taarifa sahihi wakatumia kile kidogo walichokipata kutoka kwenye ile asilimia 10 hawa watu wanakwenda kuinuka. Ni aibu kuona kijana anakuwa machinga ndani ya miaka kumi. Kijana huyo alitakiwa awe ameshatoka kutoka kwenye ujasiriamali mdogo wa kupita barabarani akaweza kukaa kivulini akawa mlipa kodi mzuri, Serikali itaongeza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe ushauri kwa Wizara ya TAMISEMI. Kuwe na training pia za ndani kwa viongozi wetu kuanzia ngazi ya mkoa, wilaya, kata mpaka vijiji. Viongozi hawa wote wajione wao ni kitu kimoja na wanatembea kwenye safari moja, wanatakiwa wafanye kazi kama timu. Mkuu wa Mkoa ni mteule wa Rais, Mkuu wa Wilaya ni mteule wa Rais, Mkurugenzi ni mteule wa Rais, sasa kama hawa watu hawatakuwa kitu kimoja wakaanza kusigina wenyewe kwa wenyewe misuguano ile waathirika ni wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwananchi anapokuwa na tatizo lake ambalo linatakiwa kuwa solved kwa Mkuu wa Mkoa au kwa Mkurugenzi, lakiniā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Janeth.

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)