Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Wizara ya TAMISEMI, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri wake Mheshimiwa Silinde na Mheshimiwa Dkt. Dugange kwa kazi nzuri ambayo wanafanya. Pia kwa upekee kabisa, nimpongeze sana Katibu Mkuu wa Wizara ya TAMISEMI Profesa Silas Shemdoe. Amekuwa na ushirikiano mzuri sana na Wabunge kwa kadri ambavyo tunakwenda kumuona na hata ukimpigia simu usiku anapokea na kujibu changamoto mbalimbali. Nampongeza sana Profesa Shemdoe. Na nimhakikishie wananchi wa Jimbo la Lupembe tuko na yeye, tunamuunga mkono sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaongea masuala machache, Halmashauri ya Njombe DC kwenye Jimbo la Lupembe sisi kama jimbo tunazo changamoto nyingi sana hasa katika eneo zima la kutengewa bajeti ya Serikali Kuu. Kwenye bajeti ya mwaka 2020/2021 Halmashauri ya Njombe DC imepokea fedha kwa kiwango cha asilimia sita tu. Maana yake nini? Zaidi ya asilimia 90 halmashauri hii inajiendesha kwa mapato ya ndani.

Mheshimiwa Spika, ombi la wananchi wa Lupembe pamoja na kwamba Serikali yetu ina majukumu mengi inafanya na inafanya kazi nzuri ya kuhudumia Watanzania mahali pengine, tunajua sungura ni mdogo lakini pia wananchi wa Lupembe wanaiomba Serikali katika bajeti hii mpya ya mwaka 2021/2022 wananchi wa Lupembe waangaliwe kwa jicho la pekee sana hasa katika fedha za Serikali Kuu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tuliomba fedha kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya utawala. Jimbo la Lupembe kwa maana ya Halmashauri ya Njombe DC tumehamia kwenye halmashauri yetu kutoka Njombe Mji. Watumishi wa Halmashauri wanakaa kwenye majengo ya shule ya msingi, hakuna vyoo, hakuna sehemu ya kula na hawana majengo ya utawala. Tunaiomba sana Serikali itoe kipaumbele kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa makao Makuu ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, liko jambo lingine upande wa TARURA, tunaiomba sana Serikali waongeze bajeti zaidi kwenye Mfuko wa TARURA. Jimbo langu la Lupembe kwenye maeneo mengi kuna barabara za vijijini halina barabara ya lami hata kilometa moja. Wananchi wa maeneo ya Kata za Kichiwa, Igongolo na Sovi pale Mtwango barabara ni mbaya sana hazipitiki. Ziko barabara kama ya Igongolo – Ninga na barabara ya Nyombo - Ninga – Lima – Itovo - Ikondo wakati wa mvua hazipitiki, wananchi hawana zahanati wanapata shida sana. Naiomba Serikali kwenye bajeti hii watazame kwa jicho la huruma kwa ajili ya kusaidia wananchi wa Jimbo la Lupembe.

Mheshimiwa Spika, lakini pia niwapongeze sana watumishi wa Halmashauri ya Njombe DC wanafanya kazi nzuri sana. Pamoja na kwamba hatupati fedha ya halmashauri kuu sisi kama halmashauri, tumekuwa tukikusanya mapato ya ndani kwa zaidi ya asilimia 100 na tunajiendesha kwa asilimia zaidi ya 90 kwa mapato ya ndani. Naiomba Serikali iwatie moyo watumishi hawa waendelee kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine watumishi hawa wanadai fedha kwa ajili ya uhamisho kutoka Njombe Mji kwenda Njombe DC. Tunaomba wapewe fedha…

SPIKA: Mna makusanyo ya kiasi gani kwa mwaka? Mapato ya ndani Lupembe ni kiasi gani?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ni zaidi ya shilingi bilioni moja na milioni mia tisa.

SPIKA: Bilioni 1.9?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Kumbe ni hela ya kawaida tu.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ni hela ndogo sana. Kwa hiyo, naomba sana Serikali waliangalie Jimbo hili ili kusudi waweze kufanya kazi nzuri za maendeleo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunao uhaba mkubwa wa watumishi wa umma. Jimbo hili kwa maana ya halmashauri tuna upungufu wa watumishi zaidi ya 442, unaweza kupata picha namna ambavyo jimbo hili lilivyo na hali mbaya. Tunaiomba sana Serikali kwenye mpango huu wa bajeti mpya ya mwaka huu Jimbo la Lupembe litazamwe kwa upekee na wananchi wamenituma ndani ya Bunge lako kuja kuwanusuru wananchi hawa katika hali hii ambayo wanayo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, limesemwa sana humu ndani jambo la watumishi wa Serikali za Mitaa kwa maana ya Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji. Nilipokwenda kwenye kampeni na nilipokwenda kwenye ziara wananchi na viongozi hawa ndiyo wanaofanya kazi kubwa ya kusimamia maendeleo, wanaomba Serikali iwaangalie, iwape posho kwa ajili ya kujikimu.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Edwin Swalle. Hivi Jimbo la Lupembe ni halmashauri gani?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, Njombe DC.

SPIKA: Njombe Vijijini.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Yes.