Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika hoja ya TAMISEMI. Nianze moja kwa moja kwa kuiomba Serikali itenge fedha kwa ajili kujenga daraja la Mwamanongu ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wakati akiomba kura mwaka 2015 kama Mgombea Mwenza. Alitoa ahadi hiyo akiwa katika Kata ya Mwabuzo kwamba daraja la Mto Mwamanongu lijengwe, lenye urefu wa mita 120 ambalo linaweza likagharimu shilingi billion 1.5. Sisi kama halmashauri tayari tumeliweka katika mpango wa mwaka huu katika fedha za maendeleo. Naomba katika miradi iliyowekwa katika miradi ya maendeleo lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, niungane na maoni ya Kamati ya TAMISEMI kwamba Serikali isimamie na kuhakikisha halmalshauri nchini zinatenga na kutoa fedha katika Mfuko wa Barabara. Kabla ya TARURA Julai, 2017, halmashauri zilitenga fedha kwa ajili ya miradi kwa ajili ya kuanzisha barabara mpya na fedha hizo zilitengwa katika miradi ya maendeleo. Kwa halmashuari niliyopo fedha hizi zaidi zilitengwa kwenye fedha ya CBG. Kazi ya halmashauri ilikuwa ni kuanzisha barabara mpya, baadaye zilikuwa zikichukuliwa wakati huo zilikuwa ni Mfuko wa Barabara (Road Fund).

Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kuanzisha TARURA, halmashauri imejitoa katika kuanzisha barabara mpya, kwa hiyo TARURA haina barabara za kuzirithi kutoka halmashauri. Niishauri Serikali katika asilimia 40 ya mapato ya ndani, Kamati ya TAMISEMI kila inapoidhinisha bajeti ya halmashauri, ihakikishe kiasi fulani kimetengwa kwa ajili ya kuanzisha barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga pia mkono kuhusu fedha za TARURA, Serikali iendelee kuziongoeza. Sisi Halmashauri ya Meatu mtandao wa barabara ni kilomita 1,041, lakini tumetengewa shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kilomita 253 na Makalvati 11, sawasawa na asilimia 24. Fedha hii haitoshi kabisa kwa ajili ya mtandao mzima. Kwa hiyo unakuta barabara nyingi zaidi ya miaka 10 hazijafanyiwa ukarabati, ikiwepo barabara ya Mwambegwa - Sapa, barabara ya Itaba - Mbushi mpaka barabara hizo zimeota miti mikubwa kwa sababu hazifanyiwi ukarabati. Halikadhalika zaidi ya miaka 15 barabara ya Mwamanoni mpaka Mwanzugi haifanyiwi ukarabati kiasi kwamba maji yameosha maboksi kalvati na wananchi wanapitia pembeni na wengine wameng’oa nondo katika makalvati haya.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwepo na utaratibu wa kuzipatia zamu za kufanyiwa ukarabati ili wananchi pia waweze kufaidika na kuweza kupita bila tatizo lolote. Lakini katika utangazaji wa kazi za barabara za TARURA naomba at least asilimia 50 ya barabara ziwe zinatangazwa mapema kuliko hivi sasa zinasubiri kutangazwa wakati zinaanza. Inakuwa ni masika, fedha yenyewe ni kidogo zinashindwa kutekeleza na wananchi wanaendelea kupata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo nina wasiwasi na mkandarai tuliyepewa katika Jimbo la Meatu. Nina wasiwasi na uwezo wake, mara ya kwanza alikuwa anasingizia mvua lakini sasahivi mvua hakuna na hakuna chochote kinachoendelea kwa ajili ya barabara ya Mwanuzi - Mwabuzo, barabara ya Mwambegwa – Mwamanigwa. Niiombe Serikali wakati wa utoaji tenda ufanyike katika level ya wilaya ili waweze kumu-own yule mkandarasi tofauti na sasa kazi zinatolewa katika ngazi ya Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi. (Makofi)