Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia kwenye Wizara ya hii ya TAMISEMI. Moja kwa moja nijikite kuchangia upande wa elimu. Naipongeza sana Serikali yangu sikivu kwa kuweza kusimamia kujenga shule kwenye kila kata. Suala hili la kuwa na shule kwenye kila kata limetupunguzia adha kubwa ya wanafunzi kupata au kwenda mwendo mrefu kwa ajili ya kwenda shule. Pamoja na Serikali kufanya kazi hii kubwa ikatenga shilingi bilioni 23 kila mwezi kwa ajili ya elimu bure, imefanya kazi kubwa sana naipongeza sana Serikali yangu. (Makofi)

Mhehimiwa Spika, naomba kutoa ushauri kwa Serikali yangu sikivu, kwamba baada ya kujenga shule hizi kwenye kila kata, tuangalie sasa ni namna gani tunakwenda kujenga hostel, mabweni kwenye kila kata sasa ili wale wanafunzi ambao wanatoka umbali mrefu wasipate shida njiani. Nasema hivyo kwa sababu wanafunzi wa kike wanakutana na vishawishi vingi wakati wanakwenda shule. Wakati mwingine kutokana na umbali wanaokwenda wanaweza kurubunika katikati hapo wakaingia kwenye mitego mingine mingi kwa sababu wanaona muda wa kwenda shuleni na kufika kwa wakati unakuwa ni kidogo. Kwa hiyo naiomba Serikali yangu sikivu iweze kuangalia ni namna gani sasa tumemaliza kujenga shule za kata, tunatoa elimu bure, lakini namna gani tunaweza kujenga mabweni ili wanafunzi hawa waweze kupata elimu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ule muda wanaotoka shule na kurudi nyumbani wanatumia muda mrefu, lakini wangekuwa shuleni wangeweza kusoma kwa bidii, wakapata muda wa kusaidiana na wenzao, wakapata muda wa kufundishwa zaidi, tofauti na hapa ambapo leo wanatoka shule, wanakwenda nyumbani, wanakuta nyumbani kuna kazi ambazo watasaidia wazazi, kwa hiyo wanakosa muda wa kujifunza kwa muda mrefu. Naomba sana dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu sina mashaka naye, najua yeye pamoja na wasaidizi wake wataliangalia hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema kuhusu wanafunzi, niseme kuhusu Walimu. Walimu hawa wanatusaidia kuangalia watoto wetu, tunaenda makazini na tunafanya kazi zetu kwa sababu tunajua wapo walimu ambao wanatunza watoto wetu, lakini walimu hao hao wamesahaulika, kiwango chao cha malipo kipo chini. Ni lazima sisi kama Bunge Tukufu tuweze kuangaliana kuwapigania Walimu hawa ili waweze kuongezewa mishahara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si hivyo tu, Walimu hawa wanakwenda masomoni wakiwa shuleni. Wanapokwenda masomoni wengine wanaobaki shuleni ambao wanaendelea na kazi wanaongezwa mishahara au kupandishwa vyeo, lakini hawa walikwenda kujiendeleza pamoja na kwamba wanajiendeleza kwa pesa zao, tena kwenye kima kile cha mshahara mdogo wanaolipwa, wanaweza kwenda kujiendelea ili wafanye kazi kwa ufanisi mkubwa, lakini shida inatokea wao wakiwa masomoni wenzao wanapandishwa mishahara, wanapandishwa madaraja, lakini wao hawapandishwi wakiwa masomoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali yangu sikivu iweze kuwaangalia hao Walimu, imekuwa ni kada ambayo imeachwa nyuma, ni kada ambayo haiangaliwi, wengine wakienda masomoni wakirudi mishahara yao inaongezeka, lakini kwa hao walimu ambao wanatuangalizia watoto wetu, hao walimu wanaotusaidia kufuta ujinga, wamesahaulika. Kwa hiyo naiomba Serikali iangalie pia suala hilo la Walimu. (Makofi)

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika. Taarifa.

SPIKA: Uko wapi?

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, niko hapa!

SPIKA: Endelea.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, suala la mishahara na suala la kutokupandishwa vyeo wakiwa shule sio Walimu tu ni watumishi wote Tanzania. Naomba kumpa taarifa hiyo.

SPIKA: Unaipokea taarifa hiyo, Mheshimiwa Esther E. Malleko.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante naipokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Spika, kero nyingine kwa Walimu, ni kero kubwa kwa wale Walimu wanaostaafu. Baada ya kustaafu anapotakiwa kubeba mizigo yao na kurudi nyumbani kwao inakuwa wanacheleweshewa kupata yale malipo na hii inaendelea kukatisha tamaa kwa sababu hao watu wamefanya kazi hiyo kubwa kwa maisha yao yote, lakini wanapofika wakati wa kustaafu bado hata ile hali ya kuangaliwa waweze kurudi nyumbani kwao imekuwa ni shida.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)