Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara lakini pia mimi nichangie katika eneo la elimu. Niikumbushe Wizara ya TAMISEMI kwamba Serikali ilichukua Shule ya Wasichana ya Kondoa na kuifanya shule ya Advanced Level na hivyo ikawa ni shule ya kidato cha tano na cha sita, lakini shule ile ilikuwa ni ya O-Level. Baada ya Serikali kuibadilisha hatukupata tena sekondari ya bweni ya wasichana ya Kondoa. Kwa hiyo, naomba katika mpango wa Wizara wa ujenzi wa sekondari kumi za bweni za wasichana, basi waende wakaifidie ile sekondari katika Jimbo la Kondoa Mjini ili mabinti zetu wa kidato cha kwanza hadi cha nne waweze kuendelea kupata masomo katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa elimu, tuna shule yetu shikizi ambayo sasa hivi imekwisha mature. Shule ile wananchi walijenga, sasa tuna madarasa manne, wako wanafunzi 300 ina mwalimu mmoja. Kwa hiyo, naiomba Wizara watusaidie kujenga majengo matatu ikamilishe majengo saba ili wanafunzi wale waendelee kusoma na isajiliwe iwe shule kamili ya msingi. Tukisema kuwarudisha katika shule mama itakuwa ni vigumu kutokana na mazingira magumu na umbali wa kutoka Chang’ombe hadi shule mama ilipo eneo la Tumbelo.

Mheshimiwa Spika, naishauri na kuiiomba Serikali kwamba walimu waliojitolea ni wengi, basi walimu wale katika ajira hizi wapewe kipaumbele kwa sababu wametumia muda wao mwingi kujitolea kufundisha katika sekondari hizo. Pia nishauri, wapo vijana wengi waliomaliza masomo ya ualimu, hawana kazi wako mitaani wakati Serikali inafanya mpango wa kuwaajiri basi watoe tamko la wale vijana waendelee kwenda kuzisaidia shule zetu kwa kujitolea angalau wawekewe fungu hata la kupata fedha ya nauli na sabuni kwa ajili ya kujikimu.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa afya, tunafahamu Hospitali yetu ya Wilaya ya Kondoa ilijengwa miaka mingi sana. Leo vituo vya afya vinavyojengwa kwenye kata ni bora kuliko Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa, ni hospitali kongwe sana. Naomba sasa katika ule mpango wa Wizara wa kujenga hospitali mpya, wafikirie namna gani sasa ya kupeleka fedha pia Kondoa kwa ajili ya kujenga hospitali mpya ukizingatia sasa Kondoa ni Halmashauri ya Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga barabara nzuri sana Kondoa, kwa hiyo, mazingira ya barabara ile yanavutia ajali nyingi. Mara nyingi zinatokea ajali, majeruhi wanapopelekwa kwenye hospitali ile wanakosa huduma na hivyo wanapewa transfer kuja Dodoma. Wakati huohuo, hospitali ya mji haina hata ambulance, kwa hiyo, wanaanza kuhangaika kutafuta ambulance kuwaleta watu Dodoma. Kwa hiyo, naomba mambo mawili hayo kwamba katika mpango wao waweze kusaidia kuijenga Hospitali ya Halmashauri ya Mji lakini pia basi wapeleke ambulance kwa ajili ya kusaidia watu wanapotakiwa kupewa transfer. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine kwenye hospitali hii tunayo X-ray ya kisasa kabisa lakini watu wanakwenda kupimwa pale wanapewa CD wanakuja kusomewa majibu Dodoma. Tunaomba basi papelekwe mtaalam kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa huduma hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha ajabu zaidi ni kwamba hospitali kongwe haina chumba cha maiti. Juzi imetokea ajali watu karibu nane wamefariki lakini hatuna mortuary. Kwa hiyo, tunaomba watusaidie kujenga mortuary kwa ajili ya kuhifadhi maiti wetu.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa miundombinu, matatizo ni kama yalivyo katika Halmashauri nyingine; barabara zetu ni mbovu. Tulikuwa tunaomba, Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Kondoa itenganishwe wapatikane Mameneja wawili wa TANROADS ili mmoja afanyie upande wa Kondoa DC na mwingine Kondoa Mjini ili kuwapunguzia mzigo maana eneo ni kubwa sana. Izingatiwe Kondoa ni kubwa imetoa wilaya mbili na majimbo matatu. Kwa hiyo, ni wilaya kubwa sana, tunaomba tupate Meneja wa tofauti kati ya Wilaya ya Kondoa na Kondoa Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa wakati huu. Naunga mkono hoja. (Makofi)