Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na kwa sababu ya ufinyu wa muda naomba niende moja kwa moja nizungumzie matatizo yaliyoko kwenye jimbo langu.

Mheshimiwa Spika, barabara ya King’ori inaanzia Malula kwenda King’ori kwenda Malulango, kwenda Leguluthi hadi Ngarenanyuki, sasa hivi iko kwenye hali mbaya sana sana na hivi karibuni nilipata picha kutoka jimboni ya hiyo barabara, nilikwenda kwa Waziri wa Ujenzi akaitizama, akaniambia ni kweli hii siyo barabara tena imekuwa shamba. Hii barabara nimeiongelea mara nyingi sana, lakini kwa bahati mbaya sana hata kwenye ilani haipo, hata kwenye mpango haipo.

Nilikwenda kumwona Waziri Mkuu tukazungumzia hilo jambo akaniambia niandike barua kwa Waziri wa Ujenzi niliandika. Kwa hiyo, naomba sana TAMISEMI waikumbuke barabara hii, iingie kwenye mpango na itengenezwe haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni nilipata jibu la swali langu namba 42 ambalo niliuliza TAMISEMI kwamba zilitengwa shilingi bilioni 1.259 kwa ajili ya kukarabati kwa kiwango cha changarawe ili ipitike mwaka mzima, lakini hizo fedha hazijapelekwa. Matokeo yake barabara ile imeharibika na haipitiki, wananchi wanateseka, wanashindwa kufuata mahitaji yao ya muhimu, wanashindwa kwenda kutafuta huduma zao za afya. Naomba sana, sana, hatua zichukuliwe. Hilo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napongeza Serikali imefanikiwa sana kuwafikia wananchi Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro ukitizama barabara zinatoka barabara kuu kwenda mlimani, barabara inayotoka Boma Ng’ombe kwenda Sanya Juu ni lami, barabara ya Kwa Sadala kwenda Masama ni lami. Ukienda barabara ya Machame kutoka Bashinituzi kwenda Machame ni lami, barabara ya Kibosho ni lami, KCMC kwenda Huru lami, KCMC kwenda Mweka lami, barabara ya Kawawa lami, barabara ya kwenda Marangu lami, barabara kwenda Mwika lami, hayo mafanikio, tunaomba wahamishe wapeleke Mlima Meru, Mlima Meru Terei inafanana na Mlima Kilimanjaro wananchi wengi wako kwenye mteremko, kwa hiyo, barabara zile huwa zinaharibika sana kila mvua zikinyesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali ya hospitali ya wilaya ni mbaya, yale majengo yalijengwa miaka 60, tunaomba sana TAMISEMI watupie jicho pale, wakarabati yale majengo na watusaidie kumalizia mortuary ambayo tuliianza kwa nguvu za wananchi kufikia mahali na imebaki kidogo tu, kama tukipata fedha kidogo tutamalizia ile mortuary, tuweze kuwa na mortuary pale Arumeru Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna upungufu wa Vituo vya Afya; tuna upungufu wa vituo 19, tuna vituo saba tu wilaya nzima, tunaomba TAMISEMI iliangalie hilo na kutujengea vituo vya afya, najua wananchi wanaangaika kujenga vituo vya afya, lakini wanahitaji msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, kuna Kituo cha Afya Momela, kilikuwa kinafanya kazi vizuri. Kwa bahati mbaya kwa sababu ilitokea sintofahamu mwaka 2019, wale wa hisani Africa Amini Alama ikabidi waondolewe kukiendesha kile kituo. Baada ya hapo huduma zimedorora sana, hakuna mashine X-Ray na ile iliyopo hakuna wataalam wa kusoma. Tunaomba Serikali ifanye juhudi iboreshe huduma za afya pale na kama ikiona ni shida sana, wale wahisani wako pale pale wanaendesha huduma za tiba mbadala, waitwe kile kituo kiendeshwe kwa mpango wa PPP. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niyaseme hayo machache. (Makofi)