Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kwa kunipa nafasi, niishukuru Wizara kupitia kwa Waziri kwa kazi nzuri sana ambayo imefanyika ndani ya kipindi cha miaka mitano. Tumeshuhudia ongezeko la vituo vya afya, shule nyingi zimejengwa na fedha zilikuwa zikienda, na mimi jimboni kwangu nilipata hizo sehemu ya huduma za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita zaidi kwenye eneo ambalo Wabunge wengi wamezungumzia, suala la TARURA. TARURA kwa bajeti ambayo ipo haitakuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile, na Waziri nikuhakikishie dada yangu, kama utakuwa na bajeti uliyonayo ni ngumu sana kutekeleza miradi ya maendeleo. Tuna kilometa zaidi ya 100,000 za barabara za mijini na vijijini. Pamoja na ongezeko uliloleta la shilingi bilioni 124 kwenye bajeti hiyo, haiwezi kufanya kitu chochote kile kwani mahitaji ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, sasa ninawaomba tutoke na maazimio ya kuishauri Serikali na maamuzi magumu ambayo tukiyafaya tutapata suluhisho la kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia kwenye Bunge hili, Bunge hilo ndilo lililotoa maamuzi tukapata fedha za kujenga barabara Mfuko wa TANROADS, zilipatikana kupitia Bunge. Mfuko wa REA, Wabunge hapahapa ndio tuliopitisha tukapata fedha za kuendeleza miradi ya umeme vijijini. Bado tumekuwa na mawazo ya kujenga uwezo juu ya Mfuko wa Maji. Ni sisi hawahawa Wabunge ambao ndio tunahitaji kutoa mawazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mapendekezo ambayo yataisaidia Serikali kutoka mahali tulipo. Naomba Waheshimiwa Wabunge turidhie, tutenge shilingi 100 – haya ni mawazo ambayo ataweza kuangalia sasa Waziri wapi watakwenda – tuna maeneo matatu ya mapendekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la kwanza alilitoa Mheshimiwa Zungu; shilingi 50 tuitenge kwa ajili ya sekta ya mawasiliano, kila mtu anapopiga simu kwa siku tuwe tunachangia shilingi 50, na tuweke wazi kwamba shilingi 50 tunatenga kwa ajili ya kujenga barabara za mijini na vijijini. Itatusababisha kupata shilingi bilioni 540.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutaona shilingi 50 haitoshi, tukitenga shilingi 100 kwa siku, kila mtumiaji wa simu akitumia shilingi 100, tutapata shilingi trilioni moja na bilioni 80 ambayo ni fedha zitakazoweza kwenda kujenga miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda mbali zaidi kama tunaweza tukatenga shilingi 200, kila siku mtumiaji wa simu akawa anatenga shilingi 200 Watanzania tukawaambia ukweli, na sisi Wabunge twende tukawaeleze ukweli wananchi wananchi kwamba shilingi 200 tunaitenga kwa ajili ya kuhudumia barabara za mijini na vijijini; tutapata trilioni mbili na bilioni 160. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka mitano tutakuwa na miundombinu bora sana kwenye nchi yetu. Na zile fedha ambazo zimetengwa kwa sasa tulizonazo zitasaidia kwenda kuimarisha miundombinu ya zahanati, vituo vya afya na hospitali, mtajenga na majengo mengine kwa hii bajeti uliyonayo. Kwasababu tutakuwa tumepata chanzo kikubwa ambacho kitatoa fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vinginevyo tutakuwa tunasema maneno ambayo yatajirudia. Kila mtu atakuja atasemea juu ya TARURA, TARURA haina fedha ya kutosha. Naomba hili Waheshimiwa Wabunge tuungane kwa pamoja, tuwe na maamuzi ambayo yatatusaidia kupata mahali pa kutoka kupata fedha za kutosha za kuhudumia maeneo ya huduma za simu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie fedha za Mfuko wa Jimbo; kumekuwa na uwiano usiokuwa sawa kwenye majimbo mbalimbali ambayo yanatofautiana. Bado Mfuko wa Jimbo ni uleule, tena ambao haujapitia tathmini ya kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnakuta mtu ambaye ana kata tatu, tano au sita mnapewa sawa na wale ambao wana kata zaidi ya kumi mpaka ishirini, naomba hili mkalifanyie kazi, mfanyie review ya majimbo yote, muangalie ukubwa wa majimbo ili tuweze kupata uhalisia mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ninapenda kuiomba Serikali; zipo halmahsauri kama ya kwanga ambayo mimi nimetoka, Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda, ndiyo iliyozaa halmashauri zote ambazo zipo Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kila halmashauri iliyokuwa inazaliwa walikuwa wanatoa magari kwenye halmashauri mama, matokeo yake halmashauri mama ilikosa vyombo vya usafiri. Tumetoa kupeleka manispaa, tumepeleka Mlele, Mpimbwe na Nsimbo, matokeo yake hii halmashauri haina vyombo. Ninaomba kupitia kwa Waziri, aiangalie halmashauri hii aipatie vyombo vya usafiri ili viweze kwenda kutekeleza miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, tunayo majengo yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi, ni karibu sehemu zote. Naamini kama mapendekezo tuliyotoa yakifanyiwa kazi zile fedha zitakazobaki hapo tuzipeleke ziende zikaimarishe kujenga majengo ambayo wananchi wamejitolea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni karibu nchi nzima kila sehemu wanajitolea, wanajenga kwa nguvu zao, bahati mbaya yale majengo yanachukua muda mrefu na wakati fulani yanaanguka kuwavunja nguvu wananchi. Tunaomba sehemu ambako wamejenga majengo ya zahanati, vituo vya afya, shule za msingi na sekondari, Serikali muwaunge mkono mpeleke fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ni kauli ya kwenu ninyi Serikali ambayo mnaitoa kwamba asilimia 20 ikifanywa na wananchi na asilimia 80 Serikali itakuja kuwa-support sasa matokeo yake wananchi wako fasta kuliko Serikali inavyopeleka huduma hiyo ya msingi. Naomba hili mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba muangalie sana posho za wenyeviti wa Serikali za vijiji, posho za Waheshimiwa Madiwani, ambao wanafanya kazi kubwa sana. Kila jambo linalotekelezwa na Serikali linashuka huku chini. Wanaofanya hiyo kazi ya hamasa ni hawa wenyeviti wa Serikali, wenyeviti wa vitongoji na Madiwani ndio wasimamizi wakubwa. Kwa hiyo tunaomba eneo hili mliangalie ili waweze kufanya kazi kwa tija na kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)