Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya TAMISEMI kwanza niwashukuru Serikali kwa yote yaliyofanywa katika Jimbo la Tunduru kusini. Kwasababu ya hotuba iliyotolewa na Waziri naomba nichangie katika sehemu tatu, sehemu ya kwanza ni suala la Utawala bora na sehemu ya pili ni Afya na sehemu ya tatu itakuwa ni suala la Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na suala la Utawala bora kama ulivyoeleza kwenye hotuba yako umeeleza vizuri namna ambavyo Utawala Bora inatakiwa viongozi wetu wa Serikali waweze kuwasikiliza wananchi ili kupata kero zao. Lakini kwenye Wilaya yetu ya Tunduru, halmashauri yetu ina vijiji 157 na ina vitongoji zaidi 1,100 tuna Mkurugenzi mmoja, tuna DC mmoja akitaka kupita maeneo yote kusikiliza kero vijijini maana yake kwa mwaka atabidi atumie zaidi ya siku 157 ili kupita kusikiliza kero katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni tatizo kubwa kwasababu linasababisha viongozi wetu wa wilaya wasiweze kufika maeneo ya vijijini kusikiliza kero za wananchi. Naomba sana tumewahi na tumepitisha mara nyingi maombi ya kugawa Wilaya ya Tunduru pamoja na kuwa na halmashauri mbili na Wilaya peke yake ziwe mbili, hii itarahisisha kupata Mkurugenzi, kupata Wakuu wa Wilaya wawili ambao watasaidia kuhakikisha kwamba wanasikiliza kero za wananchi kwa urahisi zaidi kuliko ilivyokuwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali iangalie Wilaya ya Tunduru halmashauri hii ilipata Wilaya tangu mwaka 1905 Mkoloni, walio wengi humu ndani tulikuwa hatujazaliwa, tunaomba sana Wilaya hii muifikirie, halmashauri hii iweze kugawika katika sehemu mbili ili kurahisishia wananchi wapate huduma hizi na kero zao wazieleze kwa urahisi zaidi kwasababu Mkurugenzi, Wakuu wa Wilaya watafanya kazi hii ya kuwasikiliza wananchi kwa wakati mmoja ili waweze kutoa kero zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili suala la Afya ukiangalia kama Halmashauri ya Tunduru ina kata 39, ina zahanati 52 tu kati ya vijiji 157. Kwa hiyo, kwasababu ya ukubwa wake ulivyo utakuta kituo cha afya kimoja kinahudumia kata tatu mpaka nne, tuchukulie mfano kituo cha Afya Mtina kuna kata tano zinahudumia kituo kimoja, kaini bado kuna matatizo ya miundombinu ya maeneo yale kwasababu hakuna Wodi ya akinamama hakuna Maternity ward kama nilivyozungumza hakuna chochote, hakuna chumba cha upasuaji, kwa hiyo watu wanatembea mwendo mrefu sana kwenda kufuata huduma za Afya Mtina. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mara nyingi kutokana na hali mbaya ya barabara zetu zilivyo wananchi wale wanabebwa kwenye matenga, matenga yanabebwa kwenye baiskeli au pikipiki kwenda Hospitali. Akinamama wajawazito wanabebwa kwenye matenga kwenda kwenye kituo cha Afya kwa ajili ya kuwahudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana kama sera inavyosema kila Kata iwe na kituo cha Afya, naomba tuboreshe kituo cha Afya Mtina ili kiweze kutoa huduma ile ambayo inatakiwa na ikiwezekana tuongeze kituo cha Afya kingine kwenye Kata ya Lukumbure, Nchesi Tuwemacho pamoja na Namasakata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kuna ahadi ya muda mrefu sana ya Rais wa Awamu ya Nne ya kujenga kituo cha Afya Nalasi jambo hili tangu mwaka 2014 nimeuliza Bungeni term iliyopita Bunge la Kumi na Moja zaidi ya mara tatu. Halmashauri imejitahidi imepeleka zaidi ya milioni 80 pale kuanza kujenga, lakini kila mwaka kwenye bajeti yetu tunatenga shilingi 100,000,000 kwa ajili ya kuendeleza kile kituo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kutokana na ukubwa wa Halmashauri yetu na mapato yetu pamoja na kwamba tunapata zaidi ya Bilioni tatu kwa mwaka lakini hazitoshi kwasababu eneo letu ni kubwa kata ni nyingi mgao unakuwa hautoshelezi kuweza kujenga kituo cha afya maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana kwasababu nimeuliza mara chungu nzima nimeenda kwa Mheshimiwa Waziri Jafo kipindi kile hadi kwa Katibu mkuu kuhusiana na ahadi hii naomba muiangalie namna ambavyo Nalasi inaweza kuingia kwenye bajeti hii kituo kile kiweze kujengwa ili kuondoa hii dhana ambayo Serikali imeshindwa kutekeleza ahadi ya viongozi wetu wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo suala la Elimu kwa kweli kwa Wilaya ya Tunduru tuna shule ya Msingi 152 kati ya hizo zina upungufu wa walimu zaidi ya 1,000 tunahitaji walimu 220 tunao 991. Shule nyingine zina walimu watatu hadi wanne, asilimia 60 zina walimu watano, maana walimu wengi wapo mjini hapa vijijini kwangu hakuna walimu. Naomba sana suala la walimu litakapokuja kufanyiwa ufumbuzi wa kuajiri walimu wengine tuone sisi wenye Majimbo ya vijijini kuhakikisha kwamba wanapata walimu wa kutosha ili kuhakikisha kwamba wanatoa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana shule zetu za Serikali ufaulu unakuwa ni mdogo kwasababu walimu hawapo, hawatoshelezi nichukulie mfano shule ambayo ninatoka shule ya Semeni ina zaidi ya wanafunzi 900 walimu wapo saba, madarasa yapo sita wanaelewaje hawa watu, wanafundishaje? Wanafauluje hawa Watoto? Naomba sana kwenye miudombinu ya madarasa tujitahidi kama walivyozungumza wenzangu kwenye mgao huu wa majengo ya zahanati, majengo ya shule za msingi muangalie maeneo au Majimbo ambayo yana vijiji vingi yapewe kipaumbele ili mgao uwe wa kutosha kuhakikisha kwanza tunapunguza tatizo la madarasa tunapunguza matatizo ya zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho ningependa kuongelea suala la TARURA, kwa kweli TARURA naungana mkono na wenzangu Bunge lililopita tuliomba tuongeze shilingi hamsini kutoka kwenye mafuta ili wapewe TARURA kuhakikisha kwamba barabara zetu wanatengeneza vizuri, naona wenzangu wamesahau tunaomba sana jambo hili tuliongea kwa uchungu miaka mitano iliyopita, kama mmeshindwa kwenye mafuta basi chukueni hata kwenye simu, ili tupate fungu la kuhakikisha kwamba tunajenga barabara zetu ziwe nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukulia mfano Tunduru Wilaya nzima ya Halmashauri ina kilometa 1,200 bajeti iliyopita tulipewa bilioni moja na Milioni 250 ambayo kwa hesabu ya kawaida ambayo wanatumia TARURA wana uwezo wa kukarabati barabara ambayo ina urefu wa kilometa 103 kwa maana hiyo Kilometa 1,100 zote hazina fedha, kwa maana hazijatengewa fedha, na kwa hali ilivyokuwa mbaya kama tutaendelea na mtindo huu wa TARURA kupewa fedha zilizopo bila kutenga fedha nyingine hizi barabara zitakuwa bado zina shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye Jimbo langu kuna barabara ambazo zina zaidi ya miaka 20 hazijawahi kupitiwa na greda, greda yao ni miguu ya watu na baiskeli, kwa hiyo inaonekana hapa kuna barabara kwasababu miguu ya watu inapita pale, baiskeli zinapita pikipiki zinapita unajua kwamba hii barabara inakwenda kijiji fulani. Kuna barabara ya Chemchem kwenda Ligoma mpaka Msinji ina zaidi ya miaka 15 haijawahi kufanyiwa ukarabati, kuna barabara ya Ipanje, Ndishyaje mpaka Marumba ina zaidi ya kilometa 40 haijawahi kufanyiwa chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ya Marumba - Masugulu nayo haijawahi kufanyiwa chochote kuna barabara ya Mchina Lashya Chemacho hamna kitu, barabara Amani kiungo mpaka Misechela, nayo haijawahi kutengenezwa kwa muda mrefu sana. Naomba sana jambo hili mliangalie TARURA wapewe fedha za kutosha ili waweze kuhakikisha kwamba barabara zetu zinapitika kwa wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)