Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa na afya njema mpaka kufikia siku ya leo. Napenda niwatakie Ramadhan Kareem Waislam wote nchini Tanzania, wawe na mfungo bora na wenye amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka niwashukuru wapiga kura wangu wote wa Mkoa wa Dar es Salaam, kwa kweli wamenifanyia jambo kubwa sana. Nawashukuru sana nami nawaaidi mbele yako kwamba nitawatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee pia niwapongeze na kuwashukuru wagombea wenzangu 300 wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kunipa support kubwa sana kwa sababu pamoja na kujiombea wao walikuwa wananiombea na mimi pia. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije kwenye Wizara ya TAMISEMI, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kwa kuteuliwa kwake na sina mashaka naye maana ni ndugu yangu ambaye ninauhakika na utendaji wake wa kazi. Pia nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri na Makatibu Wakuu wote wa Wizara hii ya TAMISEMI, nina hakika kwamba watatutoa pale tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije sasa kwenye mchango wangu na utajikita katika maeneo manne; elimu, afya, barabara na masoko kama muda utakuwepo. Kuhusiana na suala nzima la elimu nitaanza kwanza na hoja ya walimu. Walimu wana masikitiko makubwa, walimu wa shule za msingi na sekondari waliostaafu wana madai yao ya nauli huu sasa ni mwaka wa tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu hawa Tanzania nzima Shule za Msingi na Sekondari wanadai fedha zao za nauli, wamelitumikia Taifa hili kwa amani kwa utulivu na kwa moyo wao wote na kwa sababu kazi ya uwalimu ni wito na moyo. Leo hii walimu wanastaafu wanahangaika wanakwenda kwa Wakurugenzi, kuna wengine wanawapa majibu mazuri, lakini kuna wengine wanawapa majibu yasiyofaa, wanawaambia nendeni TAMISEMI fungu lenu haliko katika halmshashauri. Hii ni kero kubwa, naomba Serikali sasa itoe majibu walimu hawa stahiki yao ya nauli au mizigo ipo au haipo. Kama imefutwa basi ni bora waambiwe watulie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu hawa wanataka kuja huku Dodoma, mimi wananiuliza wewe mwalimu mwenzetu umetoka hapa kwenye shule ya msingi leo umekwenda Bungeni unashindwa kututetea hata sisi walimu wenzio tunapata tabu. Mimi nasema walimu wenzangu leo wanisikie, naomba Serikali iwaangalie walimu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia naomba niishauri Serikali wangu, walimu hawa miaka ya nyuma walikuwa wanalipwa kwenye halmashauri zetu nikiwepo mimi, nimelipwa fedha yangu ya mizigo milioni moja laki tatu kwenda kwetu Lindi sikuwa na tatizo lolote, huu mpango ulivyokuja kubadilka wa kutoka huku kuja kwenye Serikali Kuu ndiyo shida ilipoanzia. Sasa naomba kuuliza hii shida itaendelea kuongezeka mpaka lini? Niombe Serikali sasa iwe na mpango. Mheshimiwa Waziri mdogo wangu, naomba akija hapa aje na majibu, walimu wake wanateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumzia masuala ya walimu, sasa nizungumzie suala la elimu ya shule ya msingi. Niombe Serikali sasa ije na mpango maalumu wa kukarabati sasa shule za msingi zilizo kongwe. Nimeona imekarabati vizuri shule za sekondari zilizo kongwe, lakini sasa twende kwenye mpango maalumu wa kukarabati shule za msingi zilizo kongwe. Kuna shule za muda mrefu, kwa mfano Shule ya Msingi Kisiwani, Kigamboni sasa hivi majengo yake baada ya ujenzi wa barabara yamekuwa mafupi mno kiasi kwamba imekuwa kama vibanda. Niombe Serikali katika mpango wake wa ukarabati waiangalie Shule ya Msingi ya Kisiwani, Kigamboni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ipo Shule ya Mchikichini, Mbagala, pale kuna uwanja mkubwa ambao Samatta aliweka television kwa ajili ya kuangalia, lakini ukienda kwenye majengo ya shule ile inatia huruma, mabati yote yamekwisha kwa kutu. Pia ipo Shule ya Nzasa, Mbagala ambayo ina historia kubwa ya kutoa wanafunzi wengi kwenda sekondari; wazazi wengi walikuwa wanaigombania shule hiyo ili watoto wao waufaulu, leo hii shule hiyo baadhi ya majengo ni chakavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo Shule ya Msingi Baruti katika Halmashauri yangu ya Ubungo inahitaji ukarabati. Pia ipo Shule ya Msingi Buguruni na Shule ya Msingi Mbezi Beach. Shule ya Mbezi haiendani na mazingira ya Mbezi Beach naomba shule iendane na mazingira ya Mbezi Beach. Pia Shule za Msingi za kwanza kabisa Uhuru na Msimbazi nazo zinahitaji ukarabat. Hizi nimetoa kama mfano tu lakini shule zote kongwe naomba ziangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoke eneo hilo niende kwenye eneo la afya. Naipongeza Serikali kwa kujenga hospitali za wilaya 102 nchi nzima, ni jambo kubwa, naipongeza sana Serikali yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo naomba waangalie baadhi ya hospitali katika Mkoa wa Dar es Salaam ambazo zimezidiwa. Hospitali ya Palestina Sinza kwa kweli ni ndogo lakini inategemewa sana; mgonjwa yeyote anayetoka kwenye hospitali ndogo anakwenda Palestina, kama Mungu akijalia itakapoisha Hospitali yetu ya Wilaya ndiyo atapelekwa huko.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele imeshagongwa.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naomba sana na Hospitali ya Mbagala Zakiem na Vijibweni ziangaliwe kwenye bajeti. Ahsante sana.