Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, nami nianze kukushukuru kwa kunipa fursa hii. Kwa namna ya pekee kabisa, nimshukuru Waziri na Mwenyekiti wa Kamati kwa hotuba nzuri ambayo tumeielewa vizuri sana.


Mheshimiwa Spika, nitachangia kwenye eneo la changamoto zinazowakabili walimu wa shule za Serikali za msingi na za sekondari hapa nchini. Wote tunakubaliana kimsingi kabisa kwamba walimu kwenye jamii yetu ni watu muhimu sana, wanafanya kazi ya wito kutoka kwa Mungu kabisa. Wanatusaidia sana kufundisha watoto wetu kuanzia elimu ya awali mpaka kufika sekondari form five na form six. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge tuliomo humu ndani tutakubaliana kwamba wote tumepitia kwenye mikono ya walimu kwa namna moja au nyingine. Hata hivyo, nasikitika kusema pamoja na hawa watu kuwa muhimu sana, Serikali tumewasahau, kuna vitu ambavyo haviko sawasawa na kuna malalamiko makubwa sana kutoka kwa walimu wetu.

Mheshimiwa Spika, niseme tu zamani walimu walikuwa wanatamba Rais wa Awamu ya Kwanza alikuwa mwalimu; Awamu ya Pili alikuwa mwalimu; Awamu ya Nne walikuwa wanamuita shemeji yetu; Awamu ya Tano alikuwa ni mwalimu na mama alikuwa mwalimu. Hata hivyo, pamoja na kuwa na bahati ya kuwa na viongozi wakuu wa Serikali waliokuwa walimu wamebaki kama yatima, stahiki zao kama Serikali hatujaziangalia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali kuwasahau kwa kiasi kikubwa, nitaeleza tu machache ambayo yanatoka rohoni kwangu, kumewafanya walimu wetu wafundishe wakiwa na msongo mkubwa sana wa mawazo. Walimu wengi hawafurahii kazi kwa sababu wanaona kama vile tumewasahau. Walimu wetu wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Nitatoa mfano tu; mwaka 2016 Serikali ilipunguza wafanyakazi na idadi ya walimu ilipungua kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya hii idadi kupungua Serikali ni kweli imeshafanya jitihada za kuongeza walimu lakini haijaenda na idadi ambayo inatakiwa ambapo mwalimu anatakiwa afundishe wanafunzi 45 kwenye darasa moja ukilinganisha na walimu 33 ambao ni idadi ambayo iko kwenye shule za private. Jambo hili limeshasababisha tukawa na ufaulu ambao sio mzuri sana. Wanajitahidi na tunawalaumu kwamba wakati mwingine labda hawafanyi kazi vizuri ni kwa sababu ya changamoto ambazo nitazitaja.

Mheshimiwa Spika, walimu wetu wana changamoto nyingi na niende harakaharaka, changamoto ya kwanza ni mishahara midogo. Walimu wanaingia kazini kuanzia saa moja asubuhi, wanafunzi wanashika namba wanatoka jioni, akirudi nyumbani hana hata muda wa kufanya vitu vingine, anaanza kusahihisha kazi ambazo amewapa wanafunzi na baada ya kusahihisha anaanza kuandaa somo la kesho. Kesho yake ni hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, maisha yao kusema kweli ni kazini, ni wito, muda wote wanautumia kufanya hii kazi. Wao siyo kama sekta nyingine ambazo huwa wanasafiri wanapata per diem. Hawa watu huwa ni kwenye kituo chake cha kazi kuanzia mwaka wa kwanza mpaka wa mwisho kama hajapata fursa ya kwenda kusahihisha mitihani.

Mheshimiwa Spika, mshahara wa shilingi 420,000/= kwa mwalimu wa Shule ya Msingi au shilingi 560,000/= wanaopata hivyo, alipie nyumba, avae vizuri ili aonekane ni kioo kwenye jamii, ale vizuri, achangie kwenye shughuli za kijamii kama wananchi wengine, hizi fedha ni ndogo sana, hazitoshi. Kwa hiyo, nitapendekeza baadaye ni nini kifanyike.

Mheshimwa Spika, changamoto ya pili ambayo walimu wetu wanakumbana nayo ni madaraja. Wengi wao hawapandishwi madaraja kwa muda unaostahili. Mwalimu anaweza akawa amekaa miaka 10 hajapanda daraja; na hii ina effect kubwa sana kwenye maisha yao wanapostaafu. Kwa hiyo, hili nalo ni jambo muhimu ambalo ningependa tuliangalie kwa pamoja ili tuwasaidie wapande madaraja kama sekta nyingine ambazo zinapanda madaraja.

Mheshimiwa Spika, ni takwa la kisheria kila baada ya mwaka mmoja watumishi wanaenda likizo na wanalipwa na Serikali. Walimu wengi waliopo kule vijijini hawalipwi zile fedha za kwenda likizo. Hii ni shida! Mishahara ni midogo, mwisho wa mwaka ukifika hawezi kujisafirisha kwenda nyumbani. Kwa hiyo, naomba tuwaangalie kwa mazingira ambayo tunafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ni uhamisho. Kuna walimu wameshahamishwa kwenye maeneo ya kazi, lakini kwa bahati mbaya kutokana na ufinyu wa fedha, hawajalipwa fedha za uhamisho. Kuna madeni ya posho za kuhama, fedha ya kujikimu na fedha za kufunga mizigo. Kwa hiyo, naomba hii changamoto nayo tuiangalie kwa namna ya pekee ili tuweze kuwapa moyo walimu wetu kule walipo.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya tano ni madeni ya kwenda kwenye masomo. Walimu wengi wanakwenda kwenye masomo na kuna wachache wanaopata fursa ya kwenda kusoma na wanapokwenda kusoma kuna sheria inaruhusu wapate fedha ya kwenda kwenye masomo. Kuna madeni makubwa sana kwenye Halmashauri zetu na hawajalipwa hizi fedha.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine kubwa ni madeni ya posho za madaraka kwa Maafisa Elimu wa Kata na pia kuna posho ya madaraka pia kwa Wakuu wa Shule na Walimu Wakuu, hii ni changamoto. Ili kuwapa motisha walimu wetu ambapo ndugu zangu wote tumepitia kule, tuwasaidie hawa watu nao wajisikie ni sehemu ya ajira katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya saba ni nyumba za kuishi walimu wanaoajiriwa kule vijijini. Wenzangu wameshalisemea hili, nami ninasisitiza kabisa kwamba ni muhimu tuwajengee walimu hasa wale wanaokwenda kwenye mazingira magumu kule vijijini wapate nyumba za kuishi, otherwise wanaishia kuwa na maisha magumu sana. Utakuta wanaishi kwa namna ambayo siyo maadili ya Kitanzania kutokana na shida ambazo zipo kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto zote ambazo walimu wanapambana nazo, mimi nawashukuru sana na ninawapongeza kwamba wameendelea kufanya hii kazi kwa upendo, hawajagoma. Wakishirikiana na vyama vyao vya taaluma, wamekuwa watiifu sana na wameendelea kufundisha watoto wetu. Baada ya kusema hayo naomba niishauri Serikali mambo machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa hii sekta na specifically hapa nazungumzia walimu, naishauri Serikali itafute fedha mahali popote zilipo, kama ni huku ndani ama nje ya nchi, tuhakikishe tumetatua hizi changamoto ambazo zimewakabili walimu wetu. Changamoto ambazo nashauri tuzitatue kwanza, tuwalipe mishahara mizuri ikiwezekana. Dada yangu Mheshimiwa Ummy tujipige pige tupate fedha ili hawa watu wanaofanya kazi kwenye mazingira magumu sana walipwe mishahara mizuri, angalau ifanane fanane na wale wanaofundisha shule za private. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili, napendekeza wapandishwe madaraja. Kwa wale waliochelewa ikiwezekana tuwapandishe. Kuna kitu wanakiita mserereko. Tuwapandishe madaraja kwa kutumia ule mtindo wa mserereko, kama mtu miaka 10 alitakiwa awe kwenye daraja fulani, sasa hivi ufanyike utaratibu kuhakikisha wamepata hayo madaraja yao kwa sababu watakapostaafu ule mshahara wa mwisho unamsaidia sana kwenye maisha yake ya uzeeni. (Makofi)

Mheshmiwa Spika, ushauri mwingine, ninapendekeza tutafute fedha kama wenzangu walivyosema, tuwajengee walimu shule kule walipo. Kama tumeweza kujenga barabara, ni nini kinatushinda kuwajengea walimu hasa wale wa vijijini wakapata nyumba za kuishi wasidhalilike kule walipo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wa nne ni madeni ambayo yapo. Napendekeza Serikali ijitahidi ilipe likizo kwa wale ambao hawajalipwa, walipwe posho za madaraka wale ambao hawajalipwa na zile za uhamisho na za kwenda masomoni. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Profesa.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)