Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi hii, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia hii hotuba ya bajeti ya Wizara muhimu kabisa ya TAMISEMI, naomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Waziri, Dada yangu Ummy, hongera kwa kupewa hili jukumu zito. Sisemi kwamba, mwanzo alikuwa una majukumu mepesi, lakini kila mara amekuwa akipewa majukumu mazito anafanya vizuri. Nategemea kwa usaidizi alionao wa Manaibu Mawaziri kazi ataifanya vizuri; ndugu yangu Mheshimiwa Silinde, Mheshimiwa Ndugange, najua kazi yenu mlivyokuwa mnafanya na sasa mnalo jukumu la kusaidiana na Waziri Ummy kufanya vizuri zidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe ushauri katika Wizara hii. Mheshimiwa Waziri na Manaibu wako mnaweza mkawa na mipango mizuri sana ya kufanya kwenye Wizara hii, lakini sisi sote Wabunge humu ni mashahidi kwamba Wizara ya TAMISEMI imekuwa na shida kubwa sana kwenye usimamizi wa pesa zinazopelekwa kwenye halmashauri zetu. Nimeona hapa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna kama shilingi trilioni 2.9 karibu shilingi trilioni tatu zinaenda kwenye miradi ya maendeleo. Hizi pesa ndizo pesa watu kule kwenye halmashauri wamejipanga kuzipiga. Hizi pesa asilimia kubwa zinaenda kufanya kazi ambazo sio zenyewe. Ili tuweze kufanikiwa kwenye halmashauri zetu hizi pesa zinazotumwa kwenda kule na pesa zinazokusanywa kule ni lazima tuziimarishe halmashsuri zetu. Kwenye kuimarisha halmashauri zetu ni lazima tufahamu nani hasa ni msimamizi wa hizi halmashauri na kama zinafeli yeye anasababisha kwa kiwango gani?

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tunakimbilia kushughulika na watumishi wa halmashauri, simamisha Mkurugenzi na Mkuu wa Idara, kabla hatujaangalia msingi hasa wa usimamizi mbovu wa pesa za halmashauri. Kwenye halmashauri zetu na sheria zinavyoonesha wasimamizi wakuu wa halmashauri ni Baraza la Madiwani. Mimi ni ni-declare interest nilikuwa Diwani wa Kata ya Lyoma kabla ya kuwa Mbunge wa Sumve. Kwa hiyo, ninao uzoefu kidogo wa kukaa kwenye Baraza la Madiwani nikiwa Diwani wa Kata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Mabaraza ya Madiwani ndiko huu mwanya wa upotevu wa pesa unaanzia. Hauwezi kumwambia Diwani akasimamie Wakuu wa Idara wanaomzidi malipo mara kumi. Tumewahi kuangalia maslahi ya wasimamizi wa halmashauri zetu? Hawa Madiwani wanaosimamia halmashauri, je, wanazo nyenzo za kusimamia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kinachoangaliwa hapa ni upotevu wa mapato. Diwani anaambiwa asimamie shilingi bilioni 30, hela anazolipwa ni kidogo sana. Malipo ya Madiwani ni lazima tuyaangalie, hawa wasimamizi wa halmashauri; watumishi tunawalipa pesa ili wasimamie vizuri kazi zao, lakini Madiwani kwanza malipo yao yamekuwa ya hisani, wanalipwa kutokana na mapato ya ndani. Mkurugenzi akijifikiria ndio anawalipa kama hisani halafu haohao wakamsimamie. Kwa hiyo, mwisho wa siku tunatengeneza mwanya wa hawa watumishi kutumia uwezo wao wa kipesa kuwarubuni hawa Madiwani wasisimamie mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni lazima Serikali irudi iangalie kwanza, hata kwa hii pesa ndogo ya posho ya mwezi mnayowalipa Madiwani haitakiwi kulipwa kwa hisani ya Wakurugenzi iwe inalipwa kutoka TAMISEMI ili huyu mtu awe na nguvu ya kumsimamia Mkurugenzi. Kwa sababu siwezi kuomba hisani nasimama namshukuru Mkurugenzi, mimi nimehudhuria vikao vya Baraza la Madiwani, Diwani akisimama kwanza anamshukuru Mkurugenzi. Unamshukuru nini wakati wanaenda kumsimamia? Wanashukuru kwa sababu ili awe kwenye mgawo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pesa za marupurupu ya Madiwani ya ulipaji wa vikao na nini, ninyi Wabunge ni mashahidi kwa vile ni Madiwani, halmashauri nyingi wanadai. Pesa za bima za afya za madiwani hazipelekwi zinakusanywa, inaonekana ile mikopo ya benki haipelekwi kwa sababu hakuna utaratibu maalum wa usimamizi wa suala hili. Sasa kama hatuwezi kusimamia maslahi ya Madiwani nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri TAMISEMI hutaisimamia vizuri, lazima utaratibu wa wasimamizi walioko kwenye halmashauri ubadilishwe. (Makofi)

T A A R I F A

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mbunge wa wapi? Ndiyo nakuruhusu endelea.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, naomba tu nimpe Taarifa mzungumzaji anayeendelea kwamba, baadhi ya halmashauri, mfano Halmashauri kama kule Korogwe ambayo Madiwani waliomaliza udiwani wao mwaka 2020 mpaka leo wanaidai halmashauri. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kasalali unapokea Taarifa hiyo?

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, naipokea hiyo Taarifa na kuongeza kwamba kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba kuna Madiwani ambao wamefariki mpaka leo hata mafao yao familia hazijalipwa, akiwepo Marehemu Diwani wa Kata ya Lyoma ambayo mimi niliingia baada ya yeye kufariki na wengine. Kwa hiyo, bado tunayo kazi kubwa kwenye kusimamia maslahi ya Madiwani hawa ndiyo wanasimamia halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, niende mbele zaidi nikaangaliue jambo ambalo watu wengi wameliongelea hapa la TARURA. TARURA ni tatizo kubwa sana ndiyo maana Wabunge wengi wameliongelea hapa. TARURA ndiyo inahudumia watu wetu kule vijijini na mimi sielewi sababu za kutoa ujenzi Halmashauri tukapeleka TARURA, labda tuangalie kuna ufanisi gani upo kwa kufanya hivyo kwa sababu barabara bado hazipitiki.

Mheshimiwa Spika, nikienda Jimbo la Sumve kuna Kata kama ya Mwandu sasa hivi mvua zikinyesha huwezi kwenda, haipitiki kata nzima. Ukienda Kata ya Mwabomba haipitiki kata nzima. Nikisema nitoke Bungulwa niende Ng’undya kwenye kata hiyohiyo kuna Kijiji cha Ng’unduya huwezi kwenda kabisa, lakini tatizo kubwa TARURA uwezo wao wa kujenga madaraja ni mdogo sana. Barabara za vijijini kinachokwamisha sanasana ni madaraja, kuna madaraja sugu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kwimba hatuna Hospitali ya Wilaya, tuna Hospitali Teule ya Wilaya ambayo iko Sumve, kutokea Ngudu kwenda Sumve kuna mito mitatu ambayo mvua ikinyesha haupiti hata kama una mgonjwa na barabara ile iko TARURA. TARURA hawana hela za kujenga haya madaraja na hawana uwezo wa kujenga madaraja. Kwa hiyo, ni lazima muwaongezee uwezo na pesa ili tuweze kurahisisha maisha ya watu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja lakini naomba Mheshimiwa Waziri apokee ushauri wangu wa kuongeza ufanisi wa Mabaraza ya Madiwani kwa kusimamia malipo ya Madiwani, lakini pia kwa kuhakikisha TARURA inapatiwa pesa za kutosha. Nakushukuru sana. (Makofi)