Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Kwanza kabisa na mimi nipende kutoa shukrani nyingi sana kwa wapiga kura wangu wa Jimbo la Maswa Mashariki na niendelee kuwapa pole kwa msiba uliotukuta sote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nitoe pongezi kwa Serikali kwa kukubali kuondoa TMX kwenye manunuzi ya mazao yetu. Tatizo lilikuwa kubwa sana na kule kwenye Jimbo langu kwa kweli ilikuwa ni tatizo, hata kwa wale wanaokwenda kuuza choroko kilo tatu, nne, tano ilikuwa inawapa shida sana kuuza mazao yao kwa kupitia mtandao huu. Kwa hiyo, tunaishukuru Serikali kwa usikivu na kwa kutoa maamuzi haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri kwa mambo kama mawili au matatu. La kwanza, naomba nitoe ushauri kuhusiana na bandari yetu. Serikali yetu imeamua kujenga reli ya standard gauge, reli hii ina manufaa makubwa sana katika uchumi wa nchi yetu. Reli hii inakwenda kujengwa kwenda kwenye mipaka ya nchi yetu lakini bado reli hii itategemea mzigo mkubwa sana kutoka nchi za jirani kwa mfano nchi ya Kongo, kila mwaka tumekuwa tukisafirisha shaba kutoka Kongo zaidi ya tani 500,000 hadi 700,000 kupitia bandari yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunajenga reli hii ni lazima tuone namna ya kuungana na wenzetu wa nchi za jirani ikiwezekana na kadri tunavyokuwa tukijinasibu na Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alikuwa anasema nchi yetu ni tajiri, nchi tajiri lazima isaidie na nchi jirani kuwa matajiri ili na yenyewe iwe tajiri zaidi. Ikiwezekana kwa namna yeyote ile tuingie mikataba kuhakikisha kwamba Kongo, Zambia na nchi nyingine kwa mfano Rwanda na wenyewe wanakwenda kwenye standard gauge. Nia yake ni kuhakikisha mizigo hii inakuja kwenye bandari yetu na bandari yetu iweze kusafirisha mizigo mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu gani? Bandari yetu ina uwezo wa kubeba au kuhudumia tani zaidi ya milioni nne kwa mwaka ya mizigo migumu yaani hard cargo lakini kuna mizigo ya liquid zaidi ya tani milioni 4.5, mizigo hii inapitia kwenye bandari yetu kwenda upande wa nchi kavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nalotaka kuzungumza leo, nimesoma Mpango wa Maendeleo, nimeangalia strategy za watu wetu ambazo wanaziandaa kwenye masuala ya bandari zetu nimeona ujenzi wa meli za kufanya huduma katika nchi yetu. Ni lazima sasa tufikirie kutengeneza reli kubwa za kusafirisha mizigo kutoka bandari yetu kwenda nchi nyingine za mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tukibeba shaba tukaileta kwenye bandari yetu ikakomea hapo zikaja meli nyingine kubwa zikabeba mzigo kupeleka nchi nyingine tunakuwa tumewapa biashara watu wengine. Faida ya pili meli kubwa zikibeba mzigo kutoka kwenye bandari yetu kwenda nchi za mbali mfano China, India na maeneo mengine zitakwenda kubeba bidhaa nyingine zitaleta kwetu; huduma au bidhaa kutoka nchi nyingine zilizoendelea cargo hizo zitaletwa kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, meli haiwezi kuja nchini kwetu bila kuwa na uhakika wa kubeba mzigo mwingine. Kwa hiyo, inapokuja kwenye bandari yetu ikakuta mizigo mingi imeletwa kwa standard gauge railway kwenda kuipakia kwenye ile meli nyingine itakwenda kutusaidia kuleta commodities nyingine kutoka nchi nyingine. Lazima hiyo biashara tuichungulie tuifanye. Tusiachie Rainier, Messina na Maersk wanakwenda kuchukua mizigo yetu kutoka kwenye bandari yetu kwenda kwenye bandari nyingine wanafanya biashara halafu sisi tumepaki tupo idle, tunaomba tufanya biashara kupitia bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nataka kuliongelea ni kuhusiana na Ofisi ya Waziri Mkuu kushughulikia masuala ya UKIMWI. UKIMWI tumeudhibiti, sasa hivi magonjwa ya UKIMWI yanauwa kwa kiwango cha asilimia 4.2 tu. Magonjwa yanayouwa Watanzania wengi ni non- communicable diseases na ugonjwa unaoongoza ni wa moyo unauwa asilimia 30.6, unafuatiwa na cancer inauwa asilimia 15 inafuatiwa na magonjwa ya figo na magonjwa mengine pamoja na kisukari.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumtibu mgonjwa mmoja wa magonjwa ya moyo na kisukari kwa mwaka siyo chini ya shilingi milioni nne. Ofisi ya Waziri Mkuu ibebe suala la non- communicable diseases. Kitu kikubwa ambacho kinashauriwa na wataalam ni watu kufanya mazoezi na kula chakula bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wa Miaka Mitano pamoja na Wizara ya Afya nimepitia katika Kamati mipango yao, hatuoni juhudi za kufanya mazoezi, hatuoni juhudi za kuzuia magonjwa yasiyokuwa ya kuambukiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba waingize hili katika mipango yao kila Wizara ije na mikakati ya magonjwa ya kuambukiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)