Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami niungane na wenzangu waliotoa pole kwa kuondokewa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ngumu sana kusahau yale ambayo yamefanywa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa Watanzania wote bado wana kumbukumbu ya urithi ambao ametuachia kwa miradi mikubwa ambayo ameitekeleza hapa nchini. Naamini karibu kila Mtanzania ameguswa kwa sababu Dkt. John Pombe Magufuli alifanya kazi ya kujitoa kuwatumikia Watanzania kwa nia moja na kupeleka miradi karibu kila sehemu. Hakuna asiyejua dhamira ya Mheshimiwa Rais aliyokuwa nayo. Amejenga barabara, karibu kila mkoa kuna alama alizoziacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika,Hayati amejenga Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo litawanufaisha Watanzania wote kwa kupata umeme ambao utakuwa na gharama nafuu. Bado amejenga meli kwenye maziwa makuu, ziwa Victoria kuna ujenzi wa meli mpya na amekarabati meli ya MV Victoria na MV Butiama. Ziwa Nyasa kuna meli mbili ambazo zimejengwa, Ziwa Tanganyika kuna mpango wa kukarabati meli ya MV Lihemba na kuna ujenzi mpya wa meli ndani ya Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, amejenga bandari na kukarabati bandari; Bandari ya Mtwara, Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Tanga, haya yote yamefanywa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Amenunua ndege ambazo kimsingi zinaonekana na zimepata alama ya Taifa letu, huko nyuma tulikuwa na ndege moja tu, ameacha ndege nane na ndege tatu zilishanunuliwa japo kuna maneno mengi ambayo wananchi wanazungumzia ambayo hawafahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Ndege lilianza kuwekezwa upya na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa hiyo ustawi wa shirika hili hauwezi kustawi kwa muda mfupi kwani uwekezaji wake umetumia gharama kubwa na hasara ambazo zinasomeka kwa sasa ni za kawaida kwa mashirika ya ndege. Jirani yetu Shirika la Kenya Airways wamepata hasara ya zaidi ya shilingi bilioni 600 katika kipindi hiki ambacho tulikuwa na matatizo ya Covid. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie sana ujenzi wa reli. Wapo ambao wanapotosha ukweli, mimi na Kamati yangu kwa ujumla tumeshuhudia mradi wa reli ambao umejengwa kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro ulishakamilika. Hatua ambayo imefikiwa kwa sasa ushauri wangu kwa Serikali naomba katika kipindi wanakamilisha zile asilimia 97 ambazo zimefikia kwa sasa, tunaishauri Serikali wajipange kwa wakati ili wanunue vichwa vya treni, wanunue mabehewa ili treni ile ianze kufanya kazi. Pengine yale maneno yanazoyungumzwa yatakuwa yamekatika kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipo kipande cha reli cha kutoka Morogoro – Makutupora nacho kimejengwa kwa sasa karibu asilimia 60. Maendeleo ni mazuri sana, naishauri Serikali kwamba pamoja na jitihada ambazo zinajenga reli kipande cha kutoka Mwanza – Isaka, tunaomba Serikali sasa ijipange haraka kuhakikisha kipande cha kutoka Makutupora – Tabora kinajengwa ili reli iweze kukamilika. Tunafahamu mipango ya reli kipande kingine ni kukitoa toka Tabora kwenda Kigoma na kutoka Kaliua kwenda Mpanda na Mpanda hadi Karema ambako kunajengwa bandari. Niiombe sana Serikali iweke mahusiano na nchi jirani ya DR Congo kuhakikisha wanatengeza mahusiano ya kibiashara ili tuweze kuitumia vizuri fursa ya bandari. Naamini Serikali iliratibu vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo naomba Serikali iangalie ni mradi wa maji wa kutoka Ziwa Tanganyika kuleta maji Mkoa wa Katavi. Huu ni mradi ambao utawasaidia sana wananchi wa Mkoa wa Katavi na mikoa jirani. Mradi huu ukikamilika utatoa fursa kubwa sana. Mradi mwingine ambao tunautegemea sana Mkoa wa Katavi ni Hospitali ya Mkoa wa Katavi. Tayari Serikali imetoa fedha, lakini tunaomba kasi ya utoaji wa fedha iongezeke ili tuweze kupata huduma ile ya kimsingi inayohitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo. Huwezi kuzungumzia maendeleo ya nchi hii kama hujazungumzia kilimo. Tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kusimamia mazao makuu ya pamba, tumbaku, kahawa, korosho, mkonge na mazao mchanganyiko. Mazao haya yanahitaji usimamizi mkubwa sana na Serikali inahitaji iwekeze ipasavyo ili kuweza kukuza uchumi. Unapokuza uchumi kwa mkulima utakuwa umetengeneza uchumi kwenye maeneo yote ambayo yatazaa viwanda kutokana na rasilimali iliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la kilimo kunahitajika sana kitengo cha masoko kiweze kuimarishwa ipasavyo kwani eneo kubwa ambalo kuna shida kubwa sana kwenye mazao pindi yanapozalishwa ni uhaba wa masoko. Niiombe Serikali ihakikishe inafuatilia masoko hasa ya nje kwenye mazao haya ambao ni ya kimkakati hasa yale ambayo sio ya chakula ambayo yanahitaji mfumo mzuri wa mawasiliano ya nchi na nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tukihitaji kutengeneza uchumi wa nchi hii ni kuwasaidia wafugaji na wavuvi. Kwenye maeneo haya bado Serikali haijawekeza fedha za kutosha kwani tukiwekeza kwenye maeneo haya ya ufugaji tutawasaidia sana wananchi. Maeneo ambayo tunahitaji Serikali ipeleke fedha za kutosha tuboreshe ranch, ranch za Taifa zitakapokuwa zimeboreshwa zitawafanya sasa ranch waweze kununua mazao kutoka kwa wananchi wale wa chini wafugaji na vile vile tukiimarisha viwanda kwa ajili ya kuchakata samaki vitasaidia kukuza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)