Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Na mimi nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natumia nafasi hii kwanza kumshukuru Mungu kwa mema mengi ambayo analitendea Taifa letu la Tanzania. Vile vile nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wa awamu ya Tano, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwa nchi hii katika kipindi cha miaka mitano. Amekuza uchumi wan chi, ametupa ujasiri Watanzania na kubwa zaidi ametufanya tujiamini na kujitambua kwamba sisi sio masikini ni Taifa tajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natumia nafasi hii vile vile kumpongeza aliyekuwa Makamu wa Rais na sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amirijeshi Mkuu wa Awamu ya Sita, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwa wakati ule ya kumsaidia aliyekuwa mtangulizi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa zaidi nataka niwaambie Watanzania na wapenda maendeleo katika Taifa hili kwamba Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan anatosha kwa nafasi ambayo anayo kwa sasa na kubwa zaidi, tutarajia makubwa kwa maendeleo ya haraka na kwa kasi kubwa zaidi katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ambayo sisi Wabunge na yeye mwenyewe na Hayati Dkt. Magufuli walipita kuwaahidi Watanzania na tukakipatia Chama cha Mapinduzi ushindi mkubwa wa kishindo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii vile vile kumpongeza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye leo hii ametuletea bajeti na tunaijadili, kwa kazi kubwa ya usimamizi wa shughuli za Serikali katika Bunge na nje ya Bunge katika kipindi cha miaka mitano. Ndani ya hotuba yake kumejaa yale ambayo yametekelezeka katika kipindi cha miaka mitano na yale ambayo tunaenda kuyatekeleza ndani ya miaka mitano katika kipindi cha mwaka huu mmoja ambao tunao katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika na Spika ambaye hayupo, niwape pongezi nanyi kwa kazi kubwa ambayo mliifanya katika Bunge la Kumi katika kuisimamia Serikali na kutunga sheria ambazo zimesababisha leo tumefika tuko hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge wenzangu nawaomba niwakumbushe, kazi kubwa ambayo tunayo kwa sasa, hata Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipokuja kufungua Bunge hili aliambia jambo moja; ana imani kubwa na Bunge hili. Sasa Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, hayupo, ametangulia mbele ya haki, tuelekeze nguvu zetu na tuonyeshe imani hiyo ambayo Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alitupa Bunge hili tujielekeze kumpa nguvu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan aweze kutekeleza yale ambayo tumewaahidi wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nianze kuchangia hoja. La kwanza, nichangie katika mipango ya miradi mikakati. Tuna Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo kwa namna moja au nyingine liko katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini na liko katika Jimbo langu la Morogoro Kusini. Ni mradi mzuri na mradi ambao kwa kweli ukikamilika utaleta mafanikio makubwa ya kujenga uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuthibitisha hilo nataka niseme tu mimi mwenyewe, ndani ya Halmashauri yetu, ndani ya kipindi hiki kifupi tumepata shilingi bilioni moja na karibu milioni 100 kama Service Levy ambapo fedha hiyo tayari asilimia 10 imekwenda kwa vijana na asilimia 40 imekwenda kwenye miradi ya maendeleo ya Halmashauri na nyingine zimeenda kufanya shughuli nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali, CAG amezungumza. Kuna 4% kama huduma katika shughuli za kijamii (corporate responsibility), ambayo inatakiwa itoke katika mradi huo iende katika shughuli za wananchi. Naiomba Serikali ikasimamie hili ili kusudi tuweze kuipata fedha hii katika Halmashauri tuweze kufanya shughuli nyingi za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna huu mradi wa Standard Gauge, ninaamini kabisa kwamba Wizara ya Ardhi, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Uchukuzi na Ujenzi zikishirikiana kwa pamoja wanaweza kutoa fursa kwa wananchi ambapo mradi huu utapita wakaweza kufanya kazi za maendeleo ambazo zitawaongezea uchumi na wakati huo huo mradi huu ukafanya katika misingi hiyo. Naomba tuangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la utawala. Katika Halmashauri yetu ya Morogoro Vijijini tuna jengo la Halmashauri. Serikali ya Chama cha Mapinduzi katika mwaka wa fedha uliokwisha tumepata shilingi milioni 700. Mkandarasi yuko site, kazi inaendelea. Naomba nijue, katika awamu hii ya mwaka huu wa fedha, Halmashauri yetu imetengewa shilingi ngapi ili mradi huo uende moja kwa moja, tusije tukasimama ili tuweze kufanya shughuli za kuleta maendeleo kama vile ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni afya. Katika mwaka wa fedha uliokwisha tumepata shilingi bilioni 4.3 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ambayo imekamilika na ujenzi wa vituo sita vya afya ambavyo vimekamilika. Sasa hivi kuna suala la vifaa tiba, kuna suala la dawa, ambulance na matabibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji hospitali ile ianze kazi ikiwa imekamilika, pia tunahitaji vituo hivyo vya afya vifanye kazi vikiwa vimekamilika, kufikia lengo ambalo Serikali inataka kutoa huduma kwa wananchi wa Jimbo la Morogoro Kusini na Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliomba katika bajeti hii shilingi milioni 600 kwa ajili ya kujenga wodi tatu katika Kituo cha Afya cha Mikese, Kituo cha Afya Kisaki na Kituo cha Afya cha Kisemo. Tukipata fedha hizi ni kwamba tutakuwa na uwezo wa kujenga, kukamilisha na hivi vituo vya afya vitafanya kazi na wananchi watapata kile ambacho tunakihitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili, Halmashauri ya Morogoro Vijijini iko katika jiografia mbaya sana. Naiomba Serikali, pamoja na kwamba tumepata vituo vya afya sita, bado tuna uhitaji wa vituo vya afya tu. Tunahitaji Kituo cha Afya kwenye Kata ya Kasanga; Kata ya Bwakilajuu na Kata ya Singisa. Kata hizi ziko milimani na ni mbali kufikika, kwa hiyo, wananchi wetu wanapata wakati mgumu sana katika kupata huduma za afya. Tukiweza kuwafikishia huko, tutakuwa tumewasaidia sana. Naiomba Serikali ione ni jinsi gani ya kufanya na kutusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nizungumzie kidogo kilimo. Mkoa wa Morogoro ni mkoa ambao una ardhi nzuri kwa ajili ya kilimo. Nimeona katika mpango ambao tumeletewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kuna fedha zilikwenda Njage Wilaya ya Kilombero, kuna fedha zilikwenda Mvumi Wilaya ya Kilosa, kuna fedha zilikwenda Kigubu Mvomero na kuna fedha zilikwenda Kilangazi Kilosa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na fedha hizo kwenda, lakini Mkoa wa Morogoro bado una maeneo makubwa kwa ajili ya kufanikisha kilimo cha umwagiliaji na ambacho nina uhakika ndiyo kilimo cha uhakika na cha kutusaidia. Niombe sana kuna mradi wa Kongwaturo, mradi mkubwa sana unahitaji fedha…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umekwisha.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)