Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Waziri Mkuu kwa namna ambavyo amewasilisha hotuba yake vizuri, hotuba ambayo imebeba matarajio makubwa sana, hasa kwa sisi vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda moja kwa moja kujielekeza kwenye hotuba, ukurasa wa 34 ambapo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelezea kuhusu suala la uvuvi. Kwenye hotuba ya Waziri Mkuu amesema kwamba Serikali inakwenda kufufua Shirika la Uvuvi (Tanzania Fisheries Corporation), napenda kupongeza jitihada hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kufufua Shirika hili la Uvuvi, Mheshimiwa Waziri Mkuu ameongelea pia ujenzi wa bandari na ujenzi wa meli za uvuvi. Napenda sana kuongelea hapa; pamoja na kufufua Shirika hili la Uvuvi, pamoja na kujenga bandari hizi, pamoja na kujenga meli, lazima tuangalie Sheria yetu ya Uvuvi ya mwaka 2003 na kupitia upya Kanuni zetu za Uvuvi, bado si rafiki sana kwa wavuvi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Tanzania tumebarikiwa sana kuwa na vyanzo vingi vya maji na wakati sisi tunasoma tulikuwa tukisoma kwamba Ziwa Tanganyika ni miongoni mwa maziwa yenye kina kirefu duniani na ni la pili kwa kina kirefu likiwa na kina cha kilometa 1.47. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitarajia sasa katika urefu huu wa kina cha Ziwa Tanganyika na umaarufu wake basi utuneemeshe sisi Watanzania, hasa tunaotokea Kanda ya Ziwa Tanganyika, lakini matarajio yetu yamekuwa ni tofauti. Najiskia vibaya kusema hivi lakini Ziwa Tanganyika tumesahaulika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukianza kabisa tunaona kwamba sekta ya uvuvi hii kama ingewekezwa vizuri ingeweza kutengeneza ajira nyingi sana kwa vijana. Wizara hii ya Waziri Mkuu ni Wizara ambayo inabeba dhamana ya kushughulikia ajira za vijana. Kwa hiyo niiombe sana Wizara hii ipige jicho mbele zaidi kuona namna ambavyo tunaweza kuwekeza katika Sekta ya Uvuvi na tukaleta tija kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ajira limekuwa la kidunia, limekuwa suala la Kitaifa. Hatuwezi kutatua changamoto hii nzito ya vijana kwa kutegemea asilimia nne za vijana. Kwa hiyo naomba Wizara hii itie nguvu katika sekta ya uvuvi, iwekeze katika vyombo vya kisasa vya uvuvi. Ni aibu mpaka leo Ziwa Tanganyika halina vyombo vya kisasa vya uvuvi; ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ajabu sana katika Kanuni zetu hizi, tunaona leo tunahamasisha vijana wajiingize katika uvuvi, wafanye biashara ya uvuvi, lakini sheria zetu bado ni kandamizi kwa vijana. Leo hii ukitaka kupata leseni ya kusafirisha samaki nje, kwanza kila aina ya samaki lazima uwe na leseni tofauti. Tafiti zilizofanywa na shirika la utafiti zimesema Ziwa Tanganyika lina aina zaidi ya 400 za samaki. Sasa leo ukitaka kusafirisha sangara uwe na leseni yake, ukitaka kusafirisha mgebuka uwe na leseni yake, ukitaka kusafirisha kuhe uwe na leseni yake; jambo hili ni kandamizi kwa wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ziwa Tanganyika hili kutokana na utafiti uliofanywa, tumesema tuna aina zaidi ya 400 na katika idadi hii tuna samaki pia wa mapambo ambao wangekuwa ni kivutio kikubwa sana kwa watalii wetu, lakini Wizara yetu ya Uvuvi ipo kimya. Niombe sana Wizara hii ya Uvuvi iwekeze katika utafiti, tujue hawa samaki wa mapambo tunanufaika nao vipi, hasa sisi tunaotokea Ukanda wa Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na samaki hao wa mapambo, Ziwa Tanganyika hili lina samaki ambao wanaweza kuzalisha umeme na kwa utafiti uliofanywa ni hadi kufikia volti 900; ni umeme mkubwa sana huo. Niombe sana Wizara hii ya Uvuvi ijitahidi sana kuwekeza katika tafiti, maana tafiti hizi zimefanywa na zipo na Wizara inazijua na inazo. Kwa hiyo niombe sana suala hili liweze kuangaliwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunajaribu kuongea na wavuvi, wana changamoto nyingi sana. Wavuvi wanafanya kazi katika mazingira magumu na hali ikiwa wenyewe ndio watu wa kwanza wanaotoa kura kwa Serikali hii. Wavuvi wametupatia kura nyingi lakini wamesahaulika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijielekeza katika Kanuni zetu hizi za Uvuvi, leo hii mimi kijana nikitaka kujiajiri kwenye sekta ya uvuvi, nikisema nataka kusafirisha samaki, kwanza Ukanda wa Ziwa Tanganyika hatuna maabara ya kupimia sample ya samaki. Lazima samples hizo tukazipime Mwanza na kipimo cha sample kwa mwezi kwa leseni moja, nimesema kila aina ya samaki ana leseni yake, leseni moja ni shilingi 150,000 kwa mwezi, kwa mwaka ni shilingi 1,800,000, hiyo ni kwa leseni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukiwa na leseni tatu au nne imagine itakuwa ni shilingi ngapi. Tunaua biashara ya vijana wetu, tunaua malengo na matarajio ya vijana wetu. Niombe sana Wizara husika waone namna ya kufanya ili hizi leseni ziwekwe pamoja. Niombe sana Wizara iingilie kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri Mkuu, Wizara hii ndiyo inasimamia ajira, lazima iwe na wivu na maeneo yote ambayo yanaweza yakatoa ajira. Lazima yenyewe iwe ya kwanza kushirikiana na hizi Wizara nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye kipengele kingine; wakati tunasema kwamba tutaanzisha viwanda ni wazi kwamba hatuwezi kuanzisha viwanda kama hatuna raw materials. Kwa hiyo lazima tuwekeze kwenye kupata malighafi ili viwanda vyetu viweze kupata malighafi hizo. Sasa hatuwezi kuanzisha viwanda kama tumeshindwa kuwekeza kwenye malighafi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019 wakati wa ziara ya Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli Mkoani Katavi, aliahidi kiwanda cha kusindika samaki. Mpaka leo Serikali iko kimya hatuoni dalili zozote na sisi vijana tunatamani maana tunajua kwamba kiwanda kile kikifunguliwa vijana tutapata ajira. Sasa leo zinatoka takwimu hapa kuna viwanda kadhaa, tunajiuliza hawa vijana wanaoajiriwa wako wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana Wizara husika, twendeni site, twendeni tukaongee na wavuvi, twendeni tukapokee kero za wavuvi ili sekta hii iweze kutupatia ajira nyingi za kutosha. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Sasa hapa nilikuwa najiuliza; mvuvi mwenye leseni ya mgebuka halafu akavua kuhe, anamrejesha ziwani ama anaondoka naye? Hebu tusaidie hilo.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni leseni ya kusafirisha, kama unataka ku-export.