Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kukushukuru. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa anayoendelea kutupa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa namna ambavyo amekuja na hotuba ambayo ni dhahiri inakwenda kutimiza yale ambayo chama chetu kimeilekeza Serikali katika awamu hii kupitia ilani yetu ya mwaka 2020 - 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya sijasema niliyodhamiria, nitumie nafasi hii kuwapa pole wananchi wangu kutoka Jimbo la Mtoni ambapo mvua zinazoendelea kunyesha kule Zanzibar, baadhi yao kupitia Shehia ya Sharifu Musa Zone ya Chemchem B, wamepata athari ya kingiliwa na maji katika majumba yao. Nitumie nafasi hii kuziomba mamlaka zenye dhamana katika Serikali ya Zanzibar na katika Jimbo letu la Mtoni waone namna gani watakwenda kuwasaidia wananchi wale ili tatizo lile liwaondoke na lisijirejee tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba hii ya Waziri Mkuu, napenda nichangie suala la umeme. Ni vyema sana, nami nimefarijika kwa kweli nilipoona Serikali imeshalipa sehemu ya fedha za Mradi wa Bwawa la Umeme. Bwawa lile halina tija tu kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania peke yake ama kwa wananchi wanayoishi Tanzania Bara, lakini bwawa lile pia litaleta faida kwa sisi tunaotokea upande wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nikumbushe, Kisiwa cha Unguja, kinapokea umeme kupitia waya uliotandikwa chini ya Bahari kutoka Dar es Salaam hadi Zanzibar na Kisiwa cha Pemba kinapokea umeme kutoka Tanga uliotandikwa chini ya Bahari hadi Pemba. Umeme ule unatoka katika Mamlaka ya Shirika la Umeme la upande wa Tanzania Bara, TANESCO.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, bwawa likichimbwa, umeme ukizalishwa, bei ikishuka, wananchi wa Tanzania wakiwemo wananchi wa Zanzibar na Jimbo langu la Mtoni, watanufaika kwa bei ya umeme kushuka na kuboresha maisha yao. Naipongeza sana Serikali kwa hatua hii na ninawatia moyo, sisi wananchi wa Tanzania na sisi viongozi tuko nyuma yenu katika jambo hili na tutawaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipate fursa sasa ya kuzungumzia Mfuko wa Jimbo hasa kwa majimbo ya upande wa Zanzibar; mfuko ule wa kuchochea maendeleo ya jimbo katika Bunge la Muungano. Fedha hizi zimekuwa zikiandaliwa, zimekuwa zikitolewa, lakini mpaka jana majimbo takribani yote ya Zanzibar hayajapokea fedha za Mfuko wa Jimbo katika majimbo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua Serikali yetu imeshatoa hizo fedha, lakini yawezekana fedha zile zimekwama Ubungo. Kwa kuwa kuna flyover, sidhani kama kuna foleni tena; yawezekana fedha zile zimechelewa kupata boti, lakini kwa kuwa boti ziko nyingi, sidhani tena; lakini yawezekana fedha zile zimeelekezwa kabla ya kufika katika Mfuko wa Mbunge wa Jimbo, zikamsalimie shangazi, zimsalimie na mjomba na ziangalie kidogo uzuri wa binamu, halafu ndiyo ziingie katika Mfuko wa Jimbo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ione namna bora fedha hizi zitatoka na kama zitapita kumsalimia mjomba, kumsalimia shangazi na kuangalia uzuri wa binamu, lakini zifike kwa wakati katika majimbo yetu. Maana wananchi wa Jimbo la Mtoni wanazisubiri fedha hizo zikasaidie kutatua changamoto zinazowakabili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizi zilivyoanza kuingia katika Majimbo yetu upande wa Tanzania Bara, nasi kwa kifua mbele tukaanza kujinasibu kwamba ile miradi ambayo imeibuliwa na wananchi; mfano katika Jimbo langu la Mtoni, wameibua mradi wa kujenga daraja ambao lingeweza kuwaunganisha watoto wavuke kwa haraka kutoka school, kutoka upande mmoja wa Shehia kwenda upande wa pili; wameibua mradi wa kujenga jaa la kukusanya taka kwa muda kabla ya Manispaa kuja kuzichukuwa, wanachosubiri ni fedha tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana, wakati mambo haya yakiendelea kupangwa, jambo hili lizingatiwe sana. Hatuna tatizo na namna fedha zinavyopita, lakini zipite kwa haraka ili wananchi wa Jimbo la Mtoni na majimbo mengine ya Zanzibar waweze kujivunia hatua hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuzungumzia suala la Muungano kwa namna ambavyo limezungumzwa katika hotuba ya Waziri Mkuu. Naipongeze sana Serikali yetu kwa namna ambavyo inaendelea kushughulikia masuala ya Muungano. Leo naomba nishauri pia namna nyingine ambayo labda ipo, lakini natamani iendelee kuboresha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto za Muungano zipo nyingine kuzitatua kwake ni kuziondoa katika mambo ya Muungano; lakini zipo nyingine ambazo kuzitatua kwake ni kuziba mianya ile inayoleta changamoto na kuyaunganisha zaidi kwa mambo ya Muungano yaliyo imara zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa natolea mfano suala la mpira wa miguu. Natambua huko nyuma Zanzibar ilipata kuwa Mwanachama wa Mpira wa Miguu (CAF) Afrika. Baadaye kutokana na sheria za CAF na namna Muungano wetu ulivyo, ikashindikana. Sasa kwa nini tuendelee kufikiria kutenganisha baadhi ya mambo wakati ni muhimu tukaweza kuyaunganisha vizuri na yakaondoa changamoto hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naitaka Serikali iendeleze nguvu katika kujitapa na kuyasema wazi yale mafanikio ya kimuungano, kwa sababu changamoto huwa zinasemwa sana na wakati mwingine zinataka kutuamisha sisi tuliozaliwa baada ya Muungano, kama vile Muungano una matatizo mengi sana. Kumbe Muungano una raha nyingi sana. Muungano huu umetupa fursa Wazanzibari kutoka Zanzibar ambapo hakuna milima mikubwa mikubwa, tukafika Dar es Salaam, tukaona milima ya wastani ya Kisarawe, tukasogea Morogoro tukaona milima mikubwa mikubwa ya Ulugulu, tukasogea Kilimanjaro tukaona milima mikubwa sana ya Kilimanjaro. Hiyo ni moja ya raha na faida za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Muungano huu umewapa fursa ninyi wenzetu wa Tanzania Bara kuvuka maji na kwenda kushuhudia neema za Zanzibar zikiwemo shadow na poda nzuri zinazopakwa na wanadada wa Zanzibar. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, neema na faida za Muungano ni nyingi. Basi naiomba Serikali yetu, katika bajeti yake inavyoendelea kusema, iyataje waziwazi mambo ya Muungano ambayo yanafanya vizuri kwa faida ya kizazi chetu na kizazi kijacho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mtoni, nashukuru sana na mimi naunga mkono hoja hii. (Makofi)