Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na kwa niaba ya wananchi wa Mtama nitoe pole kwa familia ya Dkt John Pombe Magufuli kwa kufiwa na Mheshimiwa Rais. Lakini kwa wana CCM kwa kufiwa na Mwenyekiti wa chama chetu na kwa watanzania nitoe pole nyingi sana kwa kifo cha huyu mzalendo wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajisikia fahari kwamba nilishiriki ndani ya chama na nje ya chama katika mchakato wa kumpata Dkt John Pombe Magufuli mwaka 2015. Amefanyakazi nzuri kwa Taifa letu ameacha alama nyingi kubwa ambazo hazitasahaulika. Lakini ameacha mafunzo mengi kwa nchi yetu, kwa chama chetu, kwa bara la Afrika na hata dunia inajadili mafunzo aliyotuachia. Kwa hiyo, ninajisikia fahari kwamba nilishiriki mchakato wa kupatikana kwake, na namshukuru Mungu kwa maisha ya Dkt John Pombe Magufuli kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kukipongeza Chama Cha Mapinduzi kwa kusimamia vizuri mchakato wa mpito kutoka Rais Dkt. Magufuli kwenda kwa Mama Samia usimamizi mzuri uliofanywa na chama umethibitisha kwamba CCM bado ni chama bora sana kwa nchi yetu, kwa Bara la Afrika na duniani. Wamesimamia vizuri mchakato niwapongeze viongozi na chama changu. Siyo nchi nyingi zinaweza kusimamia mchakato wa namna hii wengine ingekuwa fujo na vurugu. Chama kimeonyesha uwezo mkubwa wa kuendelea kuiongoza nchi yetu kwahiyo nakipongeza chama changu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze pia vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuiheshimu katiba ya nchi yetu na kuisimamia vizuri hongereni sana Mabeho na wenzako kwa kazi nzuri mliyofanya katika kipindi chote cha mpito. Nchi yetu imepitia Awamu tano na sasa tuko Awamu ya Sita ya uongozi Awamu ya Kwanza ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikaa miaka karibia 24. Awamu ya pili ya mzee Mwinyi, Awamu ya Tatu ya mzee Mkapa, Awamu ya Nne ya mzee Kikwete, Awamu ya Tano ya Dkt Magufuli na sasa Awamu ya Sita ya mama Samia Suluhu Hassan. Katika awamu zote hizi chama kimesimamia viongozi wake kufanyakazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Awamu ya Kwanza ya Mwalimu Nyerere alikuja mzee Mwinyi. Mzee Mwinyi Pamoja na kuendeleza mambo mazuri sana yaliyofanywa na Mwalimu Nyerere kuna baadhi ya mambo alifanya maboresho na marekebisho na ndiyo maana tukaenda vile tulivyokwenda. Alipomaliza mzee Mwinyi akaja mzee Mkapa akaendeleza mambo mazuri yaliyofanywa na mzee Mwinyi na akafanya baadhi ya maboresho na marekebisho pamoja na ndoto zake lakini tukasonga mbele na yale mazuri ya mzee Mwinyi na marekebisho aliyoyafanya mzee Mkapa tukasonga mbele nchi yetu ikapiga hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, akaja mzee Kikwete pamoja na ndoto zake za chama na mengine lakini alifanya baadhi ya marekebisho kwenye yale yaliyotokea wakati wa mzee Mkapa. Akaja Dkt Magufuli Awamu ya Tano amefanya mambo makubwa lakini alifanya marekebisho makubwa sana kwenye mambo yaliyotokea kwenye awamu zilizopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, marekebisho yale ndiyo yameipa heshima Tanzania yetu leo na tukamuunga mkono akafanya marekebisho na haikuwa nongwa hata kidogo. Amekuja Rais wa Awamu ya Sita mama Samia pamoja na ndoto nzuri na muendelezo wa ndoto na amesema hadharani tutaendeleza yale aliyoyaanzisha Dkt John Pombe Magufuli na sidhani kama kuna mtu anataka haya mambo yaachwe kama yako mahali ni marekebisho madogo madogo ambayo yanafanyika vizuri na mama Samia ameanza vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Awamu ya Sita pia kama zilivyofanya awamu zingine ataendeleza ndoto lakini kule ambako anapaswa kufanya maboresho ili mambo yatekelezwe vizuri nadhani tumpe ushirikiano ayafanye hayo maboresho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mzee Mwinyi alituambia kila zama na kitabu chake zama za Mwalimu zilikuwa na kitabu chake, zama za mzee Mwinyi na kitabu chake, na wakati huo mzee Mwinyi alifanya marekebisho makubwa na haikuwa rahisi kutoka kwa mwalimu amekaa miaka 24 anakuja mzee Mwinyi anafanya marekebisho haikuwa rahisi na wakati mwingine anafanya marekebisho mbele yake anasema ruksa tumevutana na IMF sasa tukae mezani haikuwa rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mzee Mwinyi akatuambia kila zama na kitabu chake, tumekuwa na vitabu vitano sasa tunaandika kitabu cha sita wito wangu kwa viongozi Wabunge wenzangu wana CCM na watanzania tumsaidie mama kwa kumuunga mkono aandike kitabu cha awamu ya sita, tusigombane bila sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ni yetu sote tumsaidie mama na yeye aandike kitabu chake tusimshike mikono kumwandikia kitabu tumuache aandike kitabu chake na ndugu zangu legacy haitetewi legacy inajitetea yenyewe na hasa ile inayofanywa na mtu kama Dkt. Magufuli legacy yake itajitetea itajisimamia kwa miaka unless mtu ana mashaka na legacy yake lakini kama hamna mashaka na legacy yake legacy yake itasikilizwa itasemwa itaombewa na sisi watoto wajukuu na vitukuu kwasababu haya aliyoyafanya watayakuta tu hatuna sababu ya kugombana hatuna sababu ya kutoana macho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa kiongozi kwenye chama nimesimamia Idara ya Maktaba na Nyaraka duniani kama kuna chama bora kime-document mambo mengi ya kutosha CCM ni karibia namba one kwa kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye document zetu tumesema kujikosoa na kukosoana ni silaha ya mapinduzi na kujiimarisha na siyo dalili ya udhaifu chama chetu kimeenda namna hiyo kwa miaka ya kutosha…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nape kengele ya pili imeshagonga ahsante sana nimeambiwa na katibu hapa

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na naipongeza Serikali kwa uamuzi kwa uamuzi wa kuondoa TMX nendeni mkasimamie okoeni zao la korosho na ufuta hongereni kwa uamuzi huo ahsanteni sana. (Makofi)