Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutuwezesha kufanya kuendelea kufanya kazi ya Taifa letu ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningependa nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri wote ambao wanamsaidia, Makatibu Wakuu na watumishi wote wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambao kazi hizi nzuri ambazo tunaziona zimefanywa kwa juhudi zao. Ukimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu bila kumshukuru Mheshimiwa hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli unakuwa hujakamilisha shukrani, maana huyo Waziri Mkuu ni matunda ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepata bahati sana ya kufanya kazi muda mrefu kwenye chama chetu. Nimeanza kazi ya uongozi mwaka 1988 na sasa nina miaka 33 nikiwa mjumbe wa NEC. NEC yenyewe nimekaa miaka 15 lakini nimeshika vyeo mbalimbali kwa muda wote wa miaka 33. Hata hawa baadhi ya makada na Wabunge wenzangu wanaosema hapa wengine walio wengi wamenikuta humo, wengi wote akina Kibajaji, akina Msukuma, akina January Makamba na wengine walio wengi. Niliowakuta ni akina Mheshimiwa Lukuvi hapa, kwa hiyo kwenye chama chetu nimekaa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niseme jambo moja. Nakijua sana chama chetu, naujua uwezo wa chama chetu katika kusimamia mambo yote ya msingi ya uongozi wa Taifa na hata ndani ya chama chenyewe. Kunapofika kuna jambo lolote ambalo wewe ni kama Mbunge, au ni mwana CCM au ni mwananchi una mashaka lipeleke kwa CCM litapata majibu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipopata msiba wa kiongozi wetu, wengi tulihuzunika sana, kwa sababu kwanza hatukuamini na pili, tulihuzunika kwa sababu bado tulikuwa tunamhitaji, lakini la tatu, tulihuzunika kwa sababu tulijiuliza nini hatima ya Taifa letu baada ya kuondoka kwake. Sisi makada tuliobobea vinenoneno vingine tunavyoviona vinapita tulivitarajia. Ninachokiomba, sisi wenye mapenzi mema wenye kujua kazi ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tutumie busara sana katika kusema jambo lolote tunaloliona linatokea. Inawezekana akatukana mtu halafu wewe ukasimama kusema, ukawa wewe unatangaza tusi badala ya kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui kama naeleweka vizuri? Umesikia neno huko, ulipime, hili ni la kwenda kusema au ni la kuliacha, maana chama chetu kinao uongozi imara kinaweza kupata majibu ya matatizo yote tuliyonayo. Naomba niseme kama mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, lakini nimo ndani ya Bunge; tabia ya mtu kujipa ukaka wa Taifa, kujipa udada wa Taifa, kujipa ushangazi wa Taifa, unakemea, unaweza ukakosea unaweza uka-overdo, tuache. Kama unaona jambo fulani lina shida, lipeleke kwenye chama chetu, litapata majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wabunge ningependa sana tuishi kwa kuheshimiana, kustahiana, hiki ni chombo kikubwa Watanzania wanatuangalia, wanarushiana vineno visivyokuwa na maana na wakati mwingine kama mwenzako hujaelewa vizuri alichokisema, pata muda wa kujifunza, hakuna kitu kibaya kama kumtafsiri vibaya mtu aliyesema vizuri, halafu umeshamchafua unajiuliza utarudije kumsafisha. Kwa hiyo nimesimama hapa kwa kweli kusema jambo hilo, chama chetu kina majibu yote ya nchi yetu juu ya matatizo ya wananchi na chama. Mtu asijipe jukumu lolote kubwa, ajue chama kipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ningependa niseme hivi, nimepongeza kazi nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na nimesikiliza hapa mchango wa ndugu yangu Mheshimiwa Shabiby juu ya TARURA, niseme nami nataka kuongezea jambo moja kwenye TARURA. TARURA haina tatizo tu kwenye bajeti au kwenye mahusiano na Councils bali ina tatizo hata la kimuundo ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye TARURA kuna mtu anaitwa regional coordinator yupo mkoani, huyo ndie anayetangaza tenda, ndiye anayetoa kazi, ndiye anayelipa, ndiye anayeweza kuvunja mkataba, hawa District Manager wa TARURA wamekaa kama sijui nitasemaje, yaani nitafute neno gani, lakini wanafanya supervision ambayo hawana nguvu nayo. Kwa hiyo, tunapokwenda kuipa nguvu TARURA kwa kuiongezea fedha, lazima tuangalie muundo wake, tugatue madaraka kutoka juu tuyarudishe chini, kwa Mameneja wa Wilaya wa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa nilizungumze, sisi wa Kigoma tulivyosikia Standard Gauge inaanza Mwanza, tukanung’unika nung’unika, unajua sisi hapa ndio ingekuwa na impact ya kiuchumi na nini, lakini kupanga ni kuchagua, tulikwisha chagua Mwanza, hakuna tena kurudi kuangalia huku na kule. Hata hivyo, inakuwaje huku mnapelekea standard gauge, halafu hii narrow gauge ambayo ilikuwepo huku ya mkoloni inaachwa hivyo. Hali ya reli yetu ni mbovu sana hasa kutoka Dodoma kwenda Kigoma. Maeneo mengi ni mabovu. Nimemwona Waziri Mkuu amekuja na mpango wa kununua mabehewa na vichwa vya treni, tunashukuru sana hilo ni moja ya tatizo, lakini na ile reli ikarabatiwe katika kiwango cha kufanya wanaosafiri wawe na uhakika na maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali si nzuri na niwaambie katika hali ya kawaida, unajua watu wakiwa wanalalamika mbona standard gauge imeanza huku, basi hii ya kwao mbovumbovu mnawatengenezea na wenyewe ili kuwafuta machozi kulikoni waendelee kubaki.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, muda umeisha! Naunga mkono hoja na nashukuru sana. (Makofi)