Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ili nami nichangie kuhusu hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu 2021/2022. Mimi nitajikita zaidi katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri na kazi ambazo amezifanya katika Taifa hili la Tanzania. Pia niipongeze Serikali kwa kujenga na kuimarisha miundombinu ya afya katika nchi nzima ya Tanzania. Pia niipongeze Serikali kwa kutoa dawa na vifaa tiba katika maeneo mengi ya zahanati zetu pamoja na hospitali zetu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mipango mizuri ya Serikali tumeweza kujenga miundombinu mingi katika nchi yetu. Kwa mfano, tumepata vituo vya afya vya kutosha, zahanati za kutosha na hospitali za rufaa nyingi nchini Tanzania. Hata hivyo, kila lenye mafanikio lazima tukubali kuwa litakuwa na changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika zahanati hizi ambazo zimejengwa zimekuwa na uhaba wa madaktari pamoja na wauguzi. Utakuta maeneo mengine hasa maeneo ya vijijini zahanati moja inahudumiwa na daktari mmoja wakati wanaoitumia ni zaidi ya vijiji viwili au vitatu. Niiombe Serikali sasa ione umuhimu wa kuongeza bajeti katika sekta hii ili zahanati na hospitali zetu ziweze kupata watumishi stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna upungufu wa dawa. Nadhani Wabunge wenzangu wote wanakiri kwamba hospitali zetu zimebakia madaktari kwa professional zao ambazo wakishakuandikia dawa unaenda kutafuta hela ili ukanunue wewe mwenyewe, maeneo mengi dawa hazipatikani. Niiombe sasa au niishauri Serikali iweze kuongeza bajeti katika sehemu hii ambapo dawa zinahitajika sana ili wananchi wetu waweze kupata haki stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kwamba ugonjwa wa COVID-19 umetingisha sana nchi yetu, kumekuwa na upungufu wa mitungi ya gesi. Wananchi wengi wanaoishi vijijini wanaopata magonjwa yale wanakosa oxygen na hivyo kuhatarisha maisha yao kwa sababu unapotaka kupata mitungi ya oxygen ni lazima uende katika hospitali kubwa za mikoa, halmashauri au rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali sasa, ili kuwasaidia wale wananchi ambao wapo vijijini, Serikali itenge fedha za kutosha ili iweze kupeleka mitungi hii hata katika ngazi ya zahanati ili kuokoa wananchi wetu walioko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijatendea haki wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro kama nitakuwa sijachangia hospitali ya Rufaa ya Mawenzi katika Jengo la Mama na Mtoto. Hospitali ya Mawenzi ina jengo la Mama na Mtoto ambalo limejengwa tangu 2008. Ni takribani miaka 13 sasa jengo hilo halimaliziki. Hospitali ya Mawenzi inatibu wilaya saba za Mkoa wa Kilimanjaro. Kwa hiyo, ukienda katika wodi ya zamani ambayo pia ni chakavu kwa majengo, unakuta wanawake wanalala wawili wawili; mmoja anageuzia kichwa huku na mwingine kule na vitoto vyao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba katika hili Serikali iweze kutenga fedha ili iweze kumalizia jengo lile na wanawake waweze kujifungua salama na katika maeneo ambayo ni mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)