Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue fursa hii kuungana na wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini asiyeshukuru kwa kidogo hawezi kushukuru kwa kingi. Nishukuru sana kwa huduma aliyotupa Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa Taifa hili la Tanzania. Bado alama aliyoiacha itakuwa kumbukumbu kwa vizazi na vizazi. Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba hii ya bajeti ya Waziri Mkuu nitajikita sana ukurasa wa 30 ambao umezungumzia sana suala la kilimo. Moja, nipongeze watu wa Wizara ya Kilimo ambao wanaleta pembejeo kwa wakulima, lakini ombi langu kwao walete pembejeo hii kwa wakati. Maeneo ya Masasi korosho zinaanza kupuliziwa dawa kuanzia mwezi wa sita mwanzoni kabisa. Hata baadhi ya maeneo ya Lindi ukienda kule Nachunyu Lindi korosho zinapuliziwa dawa mapema sana. Sasa ni matarajio yangu mkakati huu wa kuleta pembejeo ni vyema ziletwe kwa wakati sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nishauri sana Wizara hii ya Kilimo wakati wanaleta pembejeo wawaambie wakulima mapema sana ni kiasi gani cha fedha watakatwa ili wawe na awareness kwamba hizi pembejeo wanazopewa leo bure siyo kwamba wanapewa bure ni ili baadaye waweze kulipa. Sasa ni vizuri mkatoa mchanganuo wanachotakiwa kulipa kwa wakati huu kabla ya kufika wakati wamelima, wamevuna then ukaleta tu mchanganuo ambao unaweza ukawachanganya wakulima. Hili nishauri sana lifanyike sasa mapema ili liweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ukurasa ule wa 30 umezungumziwa mfumo wa TMX, niipongeze Serikali imesema mfumo ule kwa sasa hautatumika. Kwenye hili nataka nitoe takwimu ili Wizara ione kwamba TMX kwa sasa haifai. Msimu wa korosho 2016/2017 tumeuza korosho mpaka Sh.4,000, msimu wa korosho 2015/2016 tumeuza korosho mpaka Sh.3,700. Hata hivyo, TMX ambayo imeanza kufanyiwa majaribio kwenye korosho na ufuta msimu wa mwaka jana kwenye korosho za Tandahimba zile za TANECU kwenye tani 51,000 TMX imeuza tani 4,600. Ukioanisha na bei TANECU wameuza bei kubwa zaidi ya Sh.2,700 ukilinganisha na TMX ambayo imeuza kwa Sh.2,500.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wanunuzi wake wa TMX ni wale wale wanaokwenda kwenye mnada wa kawaida. Sasa kwa namna hiyo tumeshaona wazi kwamba TMX imefeli. Kama kuna majaribio ya kwenda kufanyabiashara TMX isiwe kwenye korosho na ufuta huku kwenye korosho na ufuta uachwe utaratibu ule ambao umezoeleka ambao ni mfumo wetu wa Stakabadhi Ghalani ambao wenyewe umeleta tija kwa wakulima, kwa misimu mitatu wakulima wamepata neema imekuja TMX hamna kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nipongeze hotuba maana Waziri Mkuu amesema TMX isitumike nisisitize haimfai mkulima siyo wa korosho tu hata wa pamba, watu wa pamba msiingie kwenye huu mtego. TMX ni mtego mkubwa sana, sisi wa kwenye korosho tumefanya majaribio tumeona kati ya mnada wa kawaida na mnada wa TMX, wa kawaida umekuwa bei juu kuliko TMX. Kwa hiyo hii, TMX ni ugonjwa ambapo naomba Wizara ya Kilimo msiujaribu kabisa, uondoeni kwenye mfumo, hauwafai wakulima hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasisitiza sana hili kwa sababu hii tumeiona. Niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwenye korosho kuna kitu kinaitwa moisture ni unyaufu ambapo korosho ikiwa mbichi ukienda kuipima unapokwenda kwenye mfumo wa TMX kwa ajili ya kusema unapeleka sales catalogue kule mnunuzi anaporudi huku akakuta korosho iko tofauti TMX hana msaada wowote kwa mkulima. Mfumo wetu wa kawaida mnunuzi anakwenda anaiona korosho, tunaposema korosho hii auta ni 51 anaiona site pale, huyu TMX kwanza wanunuzi wake ni hawa hawa madalali siyo wenyewe wa Ulaya, hawa wanaofanya TMX ni akina Alibaba wako Ulaya na mambo yao yanaenda hivi. Kama mnaweza kuleta viwanda vya kubangua korosho mka- process korosho, mnaweza mkafanya TMX, lakini kwa hii raw cashewnut tuacheni kwenye mfumo huu tuliokuwa nao na tuliouzoea tutamsaidia mkulima kwa namna kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, hili mtatusaidia ninyi watu wa TRA, kuna mashine hizi za EFD, sisi wengine kule tunafanya biashara kidogo. Tuliambiwa tukinunua mashine zile tutarejeshewa fedha baadaye. Tumelipia Sh.590,000 mpaka Sh.600,000 lakini ukikaa baada ya muda fulani unakwenda ku-upgrade ile mashine unalipia shilingi 80,000. Sasa mbona tunapokwenda kwa wenzetu hawa wa TANESCO wakishatupa meter tumeshamaliza, sisi tunalipia tu kila wakati kwa nini? Sasa hawa wa TRA na EFD, moja, waturudishie fedha kama walivyosema maana ni mali yao ile siyo mali ya mfanyabiashara, EFD machine ni mali ya TRA, ni mali ya Serikali.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)