Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kabla sijaanza kuchangia, kipekee nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya. Ni ukweli usiopingika, kazi kubwa zilizofanywa na Awamu ya Tano huwezi ukamweka pembeni Makamu wa Rais ambaye leo hii ni Rais wetu na pia na Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nakushukuru kwa ziara yako uliyoifanya Wilaya ya Kyerwa ambayo mimi kama Mbunge nimeanza kuona matunda yake. Mheshimiwa Waziri Mkuu, nakushukuru sana. Kabla sijaanza kuchangia, nikukumbushe ahadi ambazo tulikueleza na wewe ukaahidi. Mheshimiwa Waziri Mkuu ulipokuja, kabla hujafika kwenye Kituo cha Mkutano, ulipita Kata ya Nkwenda. Pale Nkwenda kuna upungufu wa kukamilisha jengo la mama na mtoto, nawe uliahidi ukiwa pale kwenye Kata ya Nkwenda, kuwa jengo hili litakamilishwa na ukaahidi pia kuongeza Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine Mheshimiwa Waziri Mkuu, ulipopita kwenye barabara ya Murushaka kwenda mpaka Mulongo ulijionea na wewe mwenyewe ukaahidi barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Nashukuru kazi imeanza. Mheshimiwa Hayati Rais Dkt. John Pombe Magufuli alipofika, aliahidi kilometa 50. Nimpe majibu dada yangu aliyekuwa anasema kuna sintofahamu; hakuna sintofahamu yoyote, barabara inajengwa kuanzia Rubwera kwenda Karagwe. Kwa hiyo, hilo nimpe majibu. Jambo lingine ukitaka kuuliza, mwulize mwenye nyumba, anaweza akakupa majibu kuliko kumwuliza mpangaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni upande wa maji. Nashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja, tulimweleza changamoto tunayoipata kwenye maji na ninaishukuru Serikali kwa jitihada ambazo zinaendelea. Kwa kweli kwa sasa hivi tuna hatua nzuri. Tumeshakutana na Waziri na Katibu Mkuu; kwa kweli mimi kama Mbunge naridhika na ninawaahidi wananchi wa Jimbo la Kyerwa kuwa nimejipanga vizuri pamoja na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuwapelekea majisafi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la umeme Mkoa wa Kagera. Kwa kweli tunayo changamoto kubwa kwenye Mkoa wa Kagera. Umeme wetu ni umeme ambao kwa kweli hautabiriki, unaweza ukawaka asubuhi, saa nne umezimika, saa sita unawaka. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali hili suala la umeme Mkoa wa Kagera lipatiwe majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la kilimo. Tumekuwa tukiongea sana hapa kuhusiana na kilimo, lakini mimi niseme zipo jitihada ambazo kwa kweli bado hazijaridhisha. Ni jambo ambalo linasikitisha, ukiangalia nchi nyingine ambazo zimeendelea na nchi hizi hazina mvua ya kutosha, lakini ukija kwetu tuna mvua nyingi, Mungu ametujaalia ardhi yenye rutuba, lakini hatujaona hii neema ambayo tunayo ni namna gani tunaweza kuitumia. Naiomba sana Wizara ya Kilimo, tujikite kwenye kufanya utafiti, ni kitu gani ambacho tunahitaji kukifanya ili kilimo chetu kiwe na tija? Vinginevyo tutakuwa hapa tunaimba bila kuwa na majibu ambayo ni sahihi. Kilimo ni afya, kilimo ni uhai, kilimo ni biashara na kilimo ni viwanda. Leo hii tunasema tumeanzisha viwanda, viwanda viko vingi zaidi ya 8,000, lakini hivi viwanda vinahitaji malighafi. Tutaenda kutafuta malighafi nje wakati tungeweza kuzalisha kwetu na neema ipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kwenye mazao ya kimkakati. Mazao haya hayajapewa kipaumbele. Pamoja na kusema haya mazao tumeyatenga kimkakati, lakini mimi niseme bado hayajapewa kipaumbele. Kwa mfano, kwenye zao la Kahawa; pamoja na kulima hili zao, bado hatuna soko la uhakika. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara tujikite kutafuta masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeondoa biashara ya butura na mimi kama Mbunge ninajua biashara hii ilikuwa inawanyonya wakulima. Ni mkakati upi ambao tumekuja nao kama Serikali? Huyu mkulima anapolima kabla hajaenda kuvuna kupeleka hii Kahawa kwenye soko, anapataje pesa ya kumsaidia ili aweze kuhudumia hii Kahawa? Tunasubiri mwishoni ndiyo tunakuja kwa mkulima na huyu mkulima hatujamsaidia mwanzo. Kwa hiyo, naomba sana tutafute masoko. Wizara tokeni mkatafute masoko. Naomba hili tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, ili kilimo chetu kiende vizuri, lazima tuboreshe miundombinu ya barabara. Barabara zetu ambapo huku kwa mkulima ndio kuna mzalishaji siyo nzuri, hali ni mbaya. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iboreshe barabara za TARURA ambako huku ndiyo kuna mzalishaji mkubwa. Kwa hiyo, naomba sana hili tuliangalie ili tuweze kumsaidia mkulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo nilisemeeā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Nakushukuru. (Makofi)