Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. ANGELLAH J. KAIRUKI - WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine waliochangia hoja hii. Napenda kuchukua fursa hii kuchangia machache yaliyojitokeza katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, lakini vile vile kwa michango ambayo Waheshimiwa Wabunge wameitoa kupitia hotuba hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa ufinyu wa muda, nitajaribu kujibu masuala machache na nitajikita zaidi katika suala la kupambana na rushwa, lakini vilevile katika masuala mazima ya Utumishi, hususan madeni mbalimbali ya watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia TAKUKURU kwa namna ambavyo ameweza kuonesha utashi na kuonesha njia yake katika kupambana na tatizo la rushwa. Kupitia TAKUKURU, nimhakikishie Mheshimiwa Rais na wananchi wote wa Tanzania kwamba tutaunga mkono azma yake hii, tayari ameshatuonesha njia, kwa kweli ameipa TAKUKURU silaha iliyo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa sisi TAKUKURU tutahakikisha hatutaacha jiwe lolote ambalo halitageuzwa. Yeyote atakayejishughulisha na vitendo vya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma atachukuliwa hatua stahiki. Hatutaona haya, hatutamwonea aibu mtu yeyote atakaye jikita na vitendo hivi, hatutaangalia cheo cha mtumishi yeyote wa umma alichonacho Serikalini, ili mradi amejikita katika vitendo hivi viovu, basi atapata malipo yake stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuliunga hili mkono, tumejaribu kushauriana na wenzetu wa TAMISEMI, kuangalia ni kwa namna gani sasa tunaweza kuziba mianya mbalimbali ya ubadhirifu wa fedha katika Halmashauri. Katika miaka mitano iliyopita, tayari tumeshachukua hatua na kesi mbalimbali zimefika Mahakamani. Watumishi takribani 6,794 wamefikishwa Mahakamani na wengine wamekuwa katika hatua mbalimbali za mashauri hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa tumepeleka Waratibu mbalimbali wa Kanda wa TAKUKURU ambao watakagua kila Mradi wa Maendeleo ili kihakikisha kwamba fedha inayokwenda katika miradi, basi ni fedha ile ambayo kweli imepangiwa matumizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa 2014/2015 kupitia Waratibu hawa wa Kanda wa TAKUKURU, tumeweza kuiokolea Serikali fedha takriban Shilingi bilioni saba. Kwa mwaka huu wa fedha tutajitahidi kuongoza kasi zaidi ili tuweze kuokoa fedha nyingi zaidi za miradi mbalimbali ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu Waheshimiwa Wabunge na vilevile wananchi mbalimbali kwa ujumla wenye miradi ya maendeleo katika Halmashauri, waweze kutoa ushirikiano wa dhati kabisa kwa Waratibu hawa wa TAKUKURU wa Kanda, lakini pia kwa Ofisi nzima za TAKUKURU katika maeneo hayo ili tuweze kuchukua hatua stahiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite sasa katika suala zima la Utumishi, hususan suala zima la madeni ya watumishi katika malimbikizo ya mishahara.
Tunatambua deni ni kubwa, lakini sisi kama Ofisi ya Rais Utumisi wa Umma tumejitahidi, tumeshalipa takriban shilingi bilioni 27.9 kwa walimu mbalimbali. Vilevile kwa mwaka huu wa fedha peke yake tumeshalipa takriban shilingi bilioni 7.9 ambayo ni malimbikizo ya mishahara kwa watumishi mbalimbali takriban 8,793.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaelewa mzigo walionao watumishi wa umma na niwahakikishie kwamba, mimi kama Waziri ninayesimamia masuala ya watumishi, lakini vile vile Mbunge wa Wafanyakazi, kwa kweli nitaangalia kwa kadri inavyowezekana kwa kushirikiana na Serikali yangu, kuona ni kwa namna gani sasa madeni haya yanapungua kama siyo kumalizika kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu kwa wenzangu watumishi, nyaraka mbalimbali za madai wanazowasilisha, basi ziwe ni nyaraka ambazo ni za kweli, nyaraka ambazo tutakapofanya uhakiki zisipoteze muda. Wapo watumishi ambao wamekuwa sio waaminifu. Unakuta kuna madai makubwa, baadaye tukifanya uhakiki, gharama inakuja kupungua. Vilevile kwa kufanya hivyo, unamcheleweshea yule ambaye anastahiki kulipwa malipo yake kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana ushirikiano wa watumishi wenzangu wa umma, tujitahidi tupeleke madai hayo kwa wakati, lakini vilevile kwa Halmashauri zetu, madai ambayo yanatakiwa kulipwa na Halmashauri zile, basi wayalipe kwa wakati na wasisababishe mzigo kwa watumishi wetu wa umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, ilijitokeza hoja mbalimbali kwa upungufu wa watumishi, niseme tu kwamba nakubaliana nao; lakini changamoto kubwa ambayo tunaipata kupitia Serikali, yako mahitaji makubwa kweli ya watumishi wa umma katika sekta mbalimbali, lakini ukiangalia hivi sasa wage bill yetu au malipo ambayo tunalipa kwenye mishahara ya watumishi wa umma ni takriban asilimia 51.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa watumishi wa afya mwaka huu, 2016 tutaajiliri takribani watumishi 10,873, vile vile tutaajiri walimu 28,975 na watumishi kwa ujumla wa sekta ya umma watakuwa 71,496.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, mengine tutaongea wakati wa kuchangia Mpango. Ahsante sana. (Makofi)