Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuzungumza baada ya uchaguzi wa mwaka 2020, nikishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi na wapiga kura wangu wa Jimbo la Kisesa, kwa kunirejesha tena Bungeni kwa mara ya nne. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe na Naibu Spika mnavyoliendesha Bunge vizuri sana. Sasa kwa sababu ya muda naomba niongelee Jimbo la Kisesa; jimbo hili lina changamoto nyingi sana; moja ni uvamizi wa tembo ambao umekuwa ni wa muda mrefu. Wananchi wanavamiwa na tembo, mazao yao yanaliwa yakiwa shambani na hata yakiwa nyumbani. Chakula kinaliwa mashamba yote yanakanyagwa, watu wamepoteza Maisha, wengine wamepata vilema vya kudumu. Tumelalamika sana na tumeomba sana Serikalini kulitatua hili tatizo, lakini leo miaka miwili, mitatu sasa wananchi hao bado wanaendelea kwenye dhiki kubwa sana ya uvamizi wa tembo, lakini huu uvamizi wa wanyama wakali pia upo kwenye maeneo mengine ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni muda mrefu sana na tumekuwa tukipeleka haya malalamiko Serikalini na haijatatulia mpaka sasa hivi ambao imepelekea umaskini mkubwa sana kwa wananchi, tunaomba sasa kwa mara hii tatizo hili lifike mwisho. Tunajua Serikali ya Awamu ya Tano na Awamu ya Sita imetatua mambo mengi yaliyokuwa yameshindikana, imeweza kutatua mambo makubwa, haiwezi kushindwa kuwazuia tembo. Tumeweza kumaliza mambo ya rushwa na ufisadi, tumeweza kumaliza madawa ya kulevya, tumeweza kumaliza ujambazi na ujangili, tumeweza kumaliza uvuvi haramu, tuje tushindwe na tembo; hapa kuna mtu mmoja tu ambaye hajawajibika sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka safari hii wananchi waishi kwa amani katika maeneo yao na tatizo hili tembo Mheshimiwa Waziri Mkuu, aagize likomeshwe mara moja. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mpina, Waheshimiwa Wabunge wa Zanzibar wanashangaa kwamba jimbo limevamiwa na tembo, endelea kuchangia Mheshimiwa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, tunalo tatizo pia kubwa sana la wananchi wafugaji ambao walikuwa wanafuga wakakamatwa na wahifadhi kwamba wanachungia ndani ya hifadhi na baada ya hapo wakakatiwa rufaa wakaenda kushinda kesi mahakamani, zaidi ya wafugaji 30 wenye ng’ombe wasiopungua 5,000, ng’ombe wao mpaka sasa hivi wanashikiriwa na Serikali, licha ya kushinda kesi mahakamani. Wamefuatilia Serikalini kurudishiwa mifugo yao kwa sababu wameshapewa haki hiyo na mahakama kwamba warudishiwe mifugo yao, lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza ng’ombe hao hawajarudishwa.

Mheshimiwa Spika, sababu za kutorudishwa hazijulikani, mtu ameshinda kesi mahakamani, kwa nini uendelee kuzuia mifugo yake? wafugaji ukichukulia wa sehemu zingine mbalimbali lakini wa jimboni kwangu tu peke yake ni ng’ombe zaidi ya hizo 5,000 wa Jimbo la Kisesa ni zaidi ya 1,000 ambao mpaka sasa hivi zinashikiliwa licha ya wananchi hao kushinda kesi mahakamani. Wananchi akina Malimi Sendama na wenzake Ndatulu Malolo, Kwandu Malaba, Masunga Muhamali, Subi Maduhu na wengine ng’ombe 5,000 wanashikiliwa.

Mheshimiwa Spika, tunataka tuambiwe huko Serikalini aliyekataa hawa ng’ombe wasitolewe ni nani? Kama mahamaka imesha-grant haki ya hawa wafugaji, aliyekataa huko Serikalini ni nani? Namwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu aliingilie kati suala hili, tukatende haki kwa hawa wananchi wanyonge ambao mifugo yao imeshikiliwa na Serikali licha ya wao kushinda kesi mahakamani. Tukitoka kwenye hili Bunge niende na hao ng’ombe wa wananchi hao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hili suala limezungumzwa hapa, nataka nishauri, suala la ukusanyaji wa mapato. Wabunge wengi wamezungumza hapa mianya mbalimbali, fursa mbalimbali ya ukusanyaji wa mapato ambayo bado hatujakusanya sawasawa, nami nakubaliana nnalo. Naomba hapa tufanye upya tathmini ya mapato yetu, zile Wizara pamoja na taasisi ambazo zinakusanya mapato na zina vyanzo vingi vya mapato ziende kwenye Kamati ya Bajeti ili tuweze kuyaona maeneo ambayo tunaweza tukakusanya mapato kwa wingi. Hatima yetu na maendeleo yetu yanategemea upatikanaji wa fedha ili tuweze kutekeleza miradi hii ya maendeleo, hatuna njia nyingine ya mkato zaidi ya kutafuta fedha.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi kilichopita cha Serikali ya Awamu ya Tano iliyoongozwa na mbabe wa vita, Rais wa wanyonge, Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tulipiga hatua kubwa sana katika ukusanyaji wa mapato. Ndio maana tukaweza kutoka kwenye kuanzia ukusanyaji wa mapato wa bilioni 850 kwa mwezi mpaka leo tumefikia trilioni mbili kwa mwezi. Tukaenda kwenye maduhuli kutoka bilioni 697 mpaka trilioni 2.4.

Mheshimiwa Spika, ukusanyaji wa mapato haya umeiwezesha nchi yetu kuweza kugharamia miradi mingi sana, tumeweza kuzuia maeneo ambayo mapato yetu yalikuwa yanapotea. Tumetunga sheria, tumefanya marekebisho ya sheria, tumezuia hata ile transfer pricing ambayo ilikuwa inabeba mapato yetu mengi sana, tumedhibiti hata e-risk financial flow ambayo nayo inachukua fedha zetu nyingi sana tumeweza hata kufuta mikataba iliyokuwa inanyonya Taifa letu mikataba ya IPTL, Aggreko lakini Symbion iliyokuwa inachukua 719,000,000,000 kwa mwaka, leo tumeweza kufuta mikataba hiyo na Watanzania wanaendelea kupata fedha.

Mheshimiwa Spika, kwenye madini ndio maana hapa imezungumzwa, madini, tulikuwa tunakusanya 194,000,000,000; tumefika 500, 000,000,000; kule Mererani baada ya kujenga ukuta, tulikuwa tunakusanya 70, 000,000kwa mwezi leo tunakusanya 3,000,000,000 kwa mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Mifugo na Uvuvi tulikuwa tunakusanya 21,000,000,000 tu kwa mwaka, leo tunakusanya 74, 000,000,000 kwa mwaka. Sasa katika kuyafanya haya tumeweza kupiga hatua kubwa sana kwa maendeleo. Nataka niseme na nirudie kusema tena, nawahurumia hata wale ambao wanajaribu kubeza jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano iliyoongozwa na Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambapo aliweza kujipambanua na kupata haya mapato, wengine wanasema alikuwa fisadi.

Mheshimiwa Spika, hivi wewe fisadi, ukusanye fedha hizi, ununue ndege za Watanzania wote, huo ni ufisadi! Wewe fisadi, ukusanye hizi, ujenge barabara nchi nzima, ukarabati meli zilizokuwa hazitembei leo zinatembea, Watanzania wanaenda kote wanakotaka, ufufue reli iliyokuwa imelala miaka nenda rudi ya kutoka Dar es Salaam mpaka Arusha! Huyo ni fisadi! Kwa hiyo nawahurumia watu wa namna hiyo kwa sababu fikra zao ni fupi na uelewa wao wa kupambanua mambo ni mdogo sana. Tutaendelea kumuenzi Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika kazi kubwa ya maendeleo aliyopigania kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda unakimbia sana, nataka niongelee kidogo tu kwenye taarifa ya ukaguzi. Nizi-alert hizi kamati zinazoenda kufanya uchambuzi wa mambo yaliyopo kwenye taarifa yenyewe. Kuna mambo yalivyoandikwa kwa jinsi yalivyoandikwa si ya kawaida, kwa mfano ukienda kule maliasili, walipokuwa wanajaribu kuandika fedha zilizoibiwa na adhabu za watu wanapaswa kuchukuliwa hatua. Ukienda kule wanasema kuna matumizi ya fedha zinazotoka kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Utalii, bilioni 34, mwanzo wakasema sehemu ya fedha hizo bilioni 5.7 kama sikosei na bilioni 2.8 na milioni 100, zilihamishwa kupelekwa kwenye taasisi nyingine bila Afisa Masuhuli kujua. Halafu adhabu inayopendekezwa inasema Mkurugenzi wa Utalii pamoja na Mhasibu wake wachukuliwe hatua.

Mheshimiwa Spika, Afisa Masuhuli ambaye hakujua fedha zinahamishwa amekingiwa kifua cha nini? Kwa nini taarifa ya CAG iwe na kinga kwa wahalifu wengine, ukienda huku kwingine, upande mwingine utakutana na fedha 171,000,000 zimetumika kwa ajili ya bonanza, halafu milioni zingine kama 148,000,000 zilihamishwa na zenyewe zikatumika bila Afisa Masuhuli kujua, lakini adhabu inayopendekezwa, Waziri wa Maliasili wa kipindi kile, tena akatajwa kwa jina Mheshimiwa Dkt. Kigwangala na Katibu wake wachukuliwe hatua. Katibu Mkuu ambaye ndiye Afisa Masuhuli ambaye huyu Waziri aliandika dokezo, lakini waliyoidhinisha fedha na kutoka ni Katibu Mkuu na Ma-CEO hawa, kwa nini taarifa hii inawakingia kifua?

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Taarifa Mheshimiwa Spika.

SPIKA: Mheshimiwa Mpina pokea taarifa ya Mheshimiwa Kingu.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa anayezungumza, kwanza hatujaanza bado kujadili ripoti ya CAG. Bunge hili ni Bunge la utaratibu, ni Bunge linaloongozwa kwa misingi ya utaratibu, lakini hata sivyo, tusubiri hoja za Serikali zitakapokuwa zimejibiwa, tutakuja kuanza kuteteana humu, lakini si sasa hivi. (Makofi)

SPIKA: Pokea taarifa hiyo Mheshimiwa Mpina.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, sipokei taarifa yake na najua ninachokizungumza. Sasa hivi Kamati zetu za PAC na LAAC zimeipokea hii taarifa, zinaenda kufanya uchambuzi juu ya hizi taarifa. Zinapoenda kufanya uchambuzi sisi Wabunge hatujazuiwa kuzi-alert mambo yaliyomo humu, ziende zikayaangalie. Wewe jana ulikuwa unazungumza ATLC na unazungumza taarifa ya CAG, ulikuwa unazungumzia taarifa gani? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niongeze muda kidogo niongeze nimalizie.

SPIKA: Tunaendelea, Mheshimiwa Mpina inatosha, muda hauko upande wetu.