Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kupata fursa ya kuchangia kwenye Mpango huu wa Miaka Mitano. Nakushukuru zaidi kwa sababu pamoja na kupongeza Mpango huu mzuri, nitaanza kuchangia si mbali sana na alipomalizia mchangiaji aliyepita.

Mheshimiwa Spika, kwanza, niipongeze sana Serikali kwa kuja na Mpango huu ambao ukiusoma umezingatia sana michango ya Wabunge waliyotoa wakati Mpango huu umewasilishwa. Pia ukiusoma Mpango huu unakuja kuendeleza pale Mpango wa Miaka Mitano iliyopita; Mpango wa mwaka 2015-2020 ambao tumeona Serikali ikiwekeza kwenye miradi mikubwa ya kimkakati ambayo inaenda kulifanya Taifa letu kuwa na uchumi unaojitegemea.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika kwenye Bwawa la Stigler’s Gorge. Kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika kwenye Reli ya Standard Gauge. Kazi kubwa imeendelea kufanyika katika miradi ya kufufua Mashirika ya Umma ikiwepo Shirika letu la Ndege la ATCL. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mengine na mimi kidogo ni Mwanasheria. Ukisikiliza mchango wa Mwanasheria mmoja hapa dada yangu nauona kabisa umepungua sana knowledge ya kimkakati kwenye miradi ya kimaendeleo na fedha. Unapoongelea Shirika la ATCL…

SPIKA:Mheshimiwa Halima usikilize vizuri unasomeshwa shule hapa. Hii ni shule unasomeshwa, kwa hiyo tulia. Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, kule kwenye sheria tunafundishwa purposive approach ya legal interpretation, kwamba unasoma sheria kama ilivyoandikwa, kwenye fedha hatufanyi hivyo. Unapoongelea Shirika la Ndege, kwanza lazima utambue ni Shirika ambalo lilikuwa lina-operate kwa ndege moja. Katika miaka mitano iliyopita, Serikali imefanya kazi kubwa ya kufufua Shirika hili. Ndege ya kwanza imepokelewa mwishoni mwa mwaka 2017, zimekuwa zikipokelewa ndege mpaka tunavyozungumza zimepokelewa ndege nane (8) na ndege tatu (3) zitakuja kwenye Shirika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa wale wenye kufanya biashara wanafahamu, huwezi ukawa unafufua Shirika at the same time ukawa unatengeneza faida, haijawahi kutokea. Ziko aina ya biashara ambazo mpaka sheria zetu za kodi zinaruhusu hasara miaka mitatu mpaka miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako Waheshimiwa Wabunge hapa wamesema, Shirika la Ndege si biashara bali ni huduma inayoenda kuchochea maeneo mengine ya biashara. Ukisoma Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, maana Financial Statement hazisomwi kwenye purposive approach, husomi tu ile hasara ukabeba ukaleta hapa Bungeni kuja kupotosha umma wa Watanzania, unasoma uwanda mpana wa ripoti ile.

Mheshimiwa Spika, yapo madeni ya kurithi kwenye Shirika hili, lakini ningetegemea maana na majina tunaitwa wengine Njuka ningetegemea maneno hayo yasemwe labda na Njuka, mzoefu alitakiwa kufahamu kwamba hata ndege hizi zilivyonunuliwa zinamilikiwa na TGFA, ATC inazikodisha. Kwenye Ripoti ile ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ukiisoma inasema kabisa kwamba kuna deni limetokana na kipindi ambapo TGFA inakodisha ndege ATC lakini wote tunafahamu, si ATC peke yake au hamtembei jamani, dunia nzima ndege zimepaki kwa sababu ya COVID- 19! Hili siyo Shirika pekee lililoathirika! (Makofi)

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Elibariki.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe msemaji taarifa kwamba dunia kwa ujumla, kwa mwaka huu peke yake ime-accumulate loss ya dola bilioni 118 katika Mashirika ya Ndege. Kwa hivyo, hii haiwezi kutu- discourage sisi tuone kwamba ATC haina faida kwa Watanzania. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Jerry endelea.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea taarifa. Unaponunua ndege kwenye mizania ya kampuni ni capital expenditure. Kumbuka manunuzi haya yatakuja na mafunzo ya wataalam, marubani, wahandisi, kuboresha karakana; zote hizo huwezi ukaanza kuona faida kwenye miaka hii ya mwanzo. Pia ndege hizi, maana msemaji anasema ndege zimepaki, ndege haziruki kama kunguru zinaruka kwa mpango. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa bado dakika tano zako. (Makofi/Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, sisi wengine tumekulia kwenye familia za aviation. Tumenunua ndege za Bombadier Q4100 kwa sababu ya safari za ndani. Tumenunua Airbus, jamani hata mitandao hamuangalii? Ukiona Mheshimiwa Rais Mama Samia anasafiri ndani anasafiri na Q4100; jana ameenda Uganda na Airbus kwa sababu ndege zile zimenunuliwa kwa sababu ya Regional Flights. Zile Dreamliner, kila siku mnatangaziwa kwamba zilinunuliwa kwa sababu ya safari za masafa, trip za Guangzhou, London, India, ndege ya moja kwa moja toka nchini kwetu. Ukitoka zako ulikotoka ukaja Jijini Dar es Salaam ukakuta zimepaki, usishangae, mashirika haya yameathiriwa na magonjwa ya COVID-19 ambayo imeathiri sana usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, tunapofanya capital expenditure yoyote huwezi kuepuka kukopa. Swali huwa unakopa ufanyie nini? Kama tunakopa kwa ajili ya miradi mikubwa ya kimkakati, miradi hii ina tija kubwa kwenye uchumi wa nchi yetu, ni jambo la kupongezwa wala si jambo la kubezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa sisi tuliopewa dhamana na wananchi wa Tanzania, bila kujali umeingilia mlango gani, maana wako Wabunge hapa Vyama vyao wenyewe vinawakana…(Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini sisi tunawaheshimu kama Wabunge wenzetu, tukisimama hapa kuchangia tuweke maslahi mapana ya nchi yetu.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, tuweke maslahi mapana ya legacy aliyotuachia Rais wetu na tuisaidie Serikali.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. Naunga mkono hoja. (Makofi)