Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwanza, napenda kumpongeza Rais wetu, mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo amejikita katika kusimamia vizuri Serikali tangu alipoapishwa kuwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuweza kutuletea hapa Mpango wetu uliowalishwa tarehe 8 na Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha.

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kujikita kwenye eneo la kilimo hasa kilimo cha ufuta. Kilimo cha ufuta kimekuwa kikifanyika kwa wingi sana maeneo mengi ya nchi yetu kadri siku zilivyokuwa zinakwenda hadi kufikia sasa. Ukiangalia kwa mfano katika Mkoa wa Lindi peke yake, katika mwaka 2020 zao la ufuta liliweza kuchangia au kuuzwa kwa thamani ya shilingi bilioni 110.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kumekuwa na changamoto nyingi kwa wakulima wetu kuhusiana na hili zao ambazo napenda sasa Wizara ya Kilimo inayohusika na zao hili basi iweze kushughulikia hizo changamoto ili hatimaye tupunguze umaskini kwa wakulima wetu wa ufuta lakini tuongeze tija katika uzalishaji na pia tuweze kukuza uchumi wa Taifa letu kutoka wa kiwango cha kati chini kuwa cha kati juu.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo la upungufu wa watumishi katika sekta hii ya kilimo. Naomba hilo lizingatiwe na Wizara husika ili tuweze kuona namna ambavyo tunaweza tukakuza zao hili.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna suala la mbegu bora, Serikali imeahidi kwamba itaendelea kuongeza uzalishaji wa mbegu bora. Naomba suala hili lizingatiwe kwa sababu imeonekana kwamba katika zao la ufuta kumekuwa na ongezeko pale mbegu bora zinapokuwa zinatumika. Mbegu bora ukilinganisha na zile za asili zimekuwa zikiongeza tija kwenye uzalishaji karibu mara mbili ya zile mbegu za asili. Kwa hiyo, naomba hilo eneo hili lizingatiwe.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwenye eneo la vyama vyetu vya ushirika, kumekuwa na baadhi ya makarani ambao si waaminifu. Kwa mfano, katika Wilaya yangu ya Kilwa katika Kata ya Miguruwe, wakulima 110 hadi hivi sasa tunapozungumza waliuza mazao yao mwaka 2019/2020 lakini mpaka leo hawajalipwa fedha zao. Fedha hizo zilipotelea kwa hawa makarani wa AMCOS na TAKUKURU waliingilia kati suala hilo lakini mwisho wa siku mpaka leo matunda hayajaonekana. Kwa hiyo, naomba Wizara husika ilisimamie.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna changamoto ya wanyamapori …

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, leo Mheshimiwa Francis anasoma kabisa yaani hana wasiwasi, hongera sana Mheshimiwa Francis. (Makofi/Kicheko)

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kumekuwa na changamoto ya wanyamapori. Kuna Kijiji kule katika Kata ya Kandawale kinaitwa Ngarambeliyenga, kwa wale wasiofahamu ndiyo kule ambako yule shujaa wa Vita vya Majimaji Kinjekitile Ngwale alikuwa anaishi. Kwa hiyo, katika hiki kijiji kumekuwa na uvamizi mkubwa wa wanyama aina ya pofu na ndovu pamoja na Kata ya jirani ya Miguruwe. Kwa hiyo, naomba sana wenzetu wa Idara ya Maliasili watusaidie katika kudhibiti changamoto hizi sababu mpaka leo napozungumza wananchi wengi wamekimbia makazi yao lakini mazao yao yamekuwa yakiliwa na wanyama aina ya ndovu na pofu. Kwa hiyo, naomba sana Wizara inayohusika itusaidie.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa mifugo Wilaya ya Kilwa pamoja na Mkoa wa Lindi kwa ujumla kumekuwa na shida kubwa ya wafugaji wahamiaji, kwa sababu kwa asili Wilaya za Mkoa wa Lindi ni Wilaya za Wakulima. Kwa hivi karibuni tumewakaribisha wenzetu wafugaji katika Wilaya ya Kilwa peke yake. Katika siku za hivi karibuni imeingia mifugo zaidi ya 350,000, lakini huduma za ile mifugo zimekuwa zikikosekana. Kwa mfano kumekua na huhaba wa ujenzi wa malambo, majosho na hata watumishi wamekuwa wachache sana katika kushughulikia hii Sekta. Naomba hilo jambo lishughulikiwe.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kwa sababu ya muda. Nakushukuru sana Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane.