Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kupata nafasi ya kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kutuletea mpango huu tuujadili hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nipo kwenye Kamati ya Nishati na Madini, tarehe 12 tulifanya ziara kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere Rufiji, ule mradi unaenda vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia, huu maradi umeanza mwaka 1970. Nitumie tu muda huu kuishauri Seikali. Kweli tuna miradi mingi katika Mpango huu wa Taifa, lakini ipo miradi ya kuipa kipaumbele ikaweza kwisha kabla nasi tukiwa hai duniani tukafaidi matunda yake. Simaanishi kwamba labda miradi mingine ninaipinga, hata yenyewe ni mizuri, ila nikiangalia pato letu kwa Taifa la Tanzania, kwa mfano hii SGR ina gharama kubwa sana. Tunaweza tukajikita kule tukafeli kufikisha malengo na mwishoni tukaonekana tu, watu wa ajabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri aliyewasilisha huu mpango, kwa kuwa wewe ni mzoefu sana ndani ya hii Serikali, leo tunajadili huu mpango, tunapitisha mabilioni na matirioni yaende tena kwenye mipango, ila nikiangalia ripoti ya CAG hapa kwenye usafiri wa anga kwamba tuna short ya shilingi bilioni 150, kiukweli kwa mtu mwenye akili timamu, yaani inatia uchungu na inaumiza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia kwenye ili Taifa kuna watu wengine wanafanya kazi bure. Tukishuka chini huku Serikali inapoanzia kwa maana ya Vitongoji pamoja na Wenyeviti wa Serikali wa Kijiji, mimi Pasaka hii sikuila, nilikuwa nafanya ziara kwenye jimbo langu. Ukikaa nao wale watu, madai yao ni ya msingi sana. Hawalipwi mshahara, hawana posho yoyote, wanafanya kazi kubwa za Kiserikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye huu mpango nimeangalia, Mheshimiwa kaka yangu Waziri wa Fedha ni vema ungewaingiza hawa watu ili nao wapate haki yao ya msingi maana wanafanya kazi kubwa sana na wanaumia sana. Japokuwa hawana uwezo wa kuingia ndani ya hili Bunge Tukufu na kuzungumza mawazo yao, wanapoona watu wakubwa wanaleta hasara kwenye hili Taifa, kwa mfano shilingi milioni 150 wakati Watanzania wote tunafurahia sana uwepo wa usafiri wa anga, lakini pale inapoonekana loss yaani hapa ni lazima tukae vizuri tujiulize.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeze sana CAG huyu aliyetoa hii ripoti, maana imetupa dira. Ninamwomba au nawaomba ma-CAG wote, hata tunapopitisha haya mabilioni yaweze kuwa na udhibiti. Nawapongeze Baraza la Mawaziri kwa kuaminiwa tena na Mheshimiwa Rais, maana wengi walikuwa wana-vibrate baada ya hili tukio kubwa tuliyolipata Kitaifa kwamba wengi labda wanaweza wakakosa nafasi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Mawaziri, sisi Wabunge tuna kazi ngumu sana. Tunapofanya ziara kwenye majimbo yetu tunabaini changamoto na tunawaleteeni, kuna baadhi ya Mawaziri hawatujali vile, tunabaki sasa hatuna majibu na ukiangalia watu wanahitaji kupatiwa majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo sehemu nyingi ambazo zinachangamoto kwa mfano Wizara ya TAMISEMI; nampongeza tu dada yangu kwa kuteuliwa, lakini ile sekta ni muhimu sana kwenye jamii, maana vitu vingi vinalenga TAMISEMI. Zipo changamoto Serikali kabla ya mimi kuwa Mbunge ilikaa ikapitisha bajeti kama leo tunavyopitisha mpango huu. Fedha zilienda zikaliwa, watu hawajawahi kuchukuliwa hatua hata siku moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami naiomba tu Serikali, hilo iliangalie kwa umakini sana na ichukue hatua haraka iwezekanavyo. Siyo sifa nzuri, wala siyo Uislamu wala Ukristo; kwa mfano, mtu anaonekana kabisa amehujumu fedha za walipa kodi ambao ni wafanyabishara wadogo wadogo, wanachangia kwenye pato hili la Taifa, wanajibana kununua hata nguo, halafu mtu mmoja tu au wawili wanakula pesa za wananchi wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huko mitaani kiukweli kuna shida kubwa sana. Hata kusema kwamba tuko katika uchumi wa kati, yaani mpaka inafikia wakati mwingine ukiangalia hali iliyoko mitaani jinsi ilivyo mbaya, unaona dhahiri kabisa kwamba sijui walitumia takwimu gani? Unashindwa kujua kwa vile huna elimu ya kuweza kudadavua mambo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa huu siyo wakati wa kampeni, naiomba Serikali, nawe Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ni mzoefu na haya mambo ya uongozi, ufanye sasa ile gear uliyokuwa unatumia hata miaka yote ili kusudi hata wenzetu hawa wa maisha ya kawaida waweze kupata maisha rahisi mifukoni. Mshauri Mheshimiwa Rais ili kusudi wananchi wetu wadogo wadogo wawe na pesa kwenye mifuko yao. Sasa hivi huko mitaani hali ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaongelea viwanda; tuna viwanda 4,460 na kitu, lakini kiukweli hali ni mbaya. Hata wapiga kura wetu waliotupigia kura wana hali mbaya. Tuliahidi barabara; naishauri Serikali tuelekeze nguvu nyingi kwenye miundombinu za barabara na kwenye miundombinu za maji. Kwa mfano mimi natokea Jimbo la Mbogwe. Kutoka ziwa Victoria kufika pale kwenye jimbo langu ni kilomita 80. Nimeangalia huu mpango, hakuna mahali panaonekana kwamba ni lini wananchi wa Mbogwe watapata maji kutoka pale kwenye Ziwa Victoria kwenda pale kwenye jimbo langu?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shida kubwa sana ya maji, hasa Mbunge unapokuwa msibani, unalazimika unywe maji na baada ya kumaliza kuyanywa, unaenda tena unaugua na unatumia gharama kubwa kutibiwa typhoid pamoja na magonjwa mengine. Kwa hiyo, naiomba Serikali, yaani mpango huu, sawa tunauunga mkono, lakini i-sort vipaumbele muhimu kama vile maji ni kitu cha muhimu na afya. Kuna upungufu mkubwa sana kwenye hospitali, dawa hakuna kabisa kiuhalisia pamoja na vipimo. Kwa mfano pale Mbogwe kwangu, ninamshukuru Waziri wa Afya amefika amejionea hali iliyopo pale Masumbwe. Akina mama kila siku wanajifungua, lakini hakuna X-Ray, hakuna vipimo vya kumpima mtu kubaini kwamba ana shida gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni vyema sasa tunapopitisha huu mpango, lazima vitu vingine tuvipe vipaumbele, maana ni muhimu kulika hii SGR pamoja na mambo mengine ya matrilioni na matrilioni ambayo hayana sababu kwa wananchi wetu wale wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafasi nyingine ni hii ya kilimo. Toka mwaka 1992 nikiwa mdogo, Serikali ya Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, wakulima walikuwa wakipewa mbegu za pamba. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ukifanya huo mpango kwa wakati huu, wakulima wakapata pamba, tutakuwa tumelisaidia hili Taifa. Waheshimiwa Mawaziri mwangalie, unajua sasa hivi tuna nafasi hizi, lakini ipo siku tunaweza tukafungwa pengine kwa kupitisha hii mipango halafu inakuwa haina mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimeshuhudia Serikali ya Rwanda, kuna Mawaziri wamefungwa pale. Walikuwa wakipitisha hizi bajeti zinaenda ndani ya watumishi wa Serikali zinaliwa, hawafuatilii, wanarudi Bungeni tena kujadili, wanatuma tena mabilioni mengine yanaenda, lakini baadaye ufuatiliaji unakuwa haupo, halafu mnarudi Bungeni hapa hapa kupitisha tena bajeti nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mwaka 2015 mlipitisha bajeti, lakini ile miradi haijakamilika na haina kiwango, lakini fedha zilienda na hakuna majibu. Namwomba Mheshimiwa Rais, kasi aliyoanza nayo asilegeze, aendelee hivyo hivyo. Japokuwa anashabikiwa sana na watu, wengine sio wazuri sana kuwaongelea hata hapa. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, ukiona unashabikiwa sana hata jimboni, lazima usimame ufikirie, ni kwa nini wananishabikia sana kila mtu? Kuna wengine wanakushabikia ili ukosee kusudi wapate pa kupitia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajua tuko kwenye siku za mwisho, lipo hili janga la corona, watu wanapata shida. Ukiangalia Kenya pale, wananchi sasa hivi wanalia, Serikali ilikopa matrilioni na mabilioni, kumbe sijui hata ugonjwa haukuwepo, sasa hivi wananchi hata wale wa kawaida wanachangia lile deni kulilipa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Rais aangalie kwa umakini sana, anapoona anashabikiwa sana na watu, lazima afikirie kwamba hawa watu wanaomshangilia wana heri au wanataka kutuingiza kwenye matatizo kabisa ambayo hatutayamaliza tena? Afuate tu nyayo za Mheshimiwa Rais, siyo lazima afuate zote, ni kuchambua.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua Marehemu akifufuka hata leo akakuta hii ripoti kwanza iliyotolewa juzi hii ya ndege, siyo kweli Marehemu alinunua ndege hizi kusudi zile short, alinunua ili afanye biashara. Hawa watu waliosababisha hiki, wanatakiwa kuchukuliwa hatua. (Makofi/Kicheko)

Waheshimiwa Wabunge, msicheke. Sisi tunaolipa kodi wenye mitaji ya kuungaunga hatukubahatika hata kuwa na elimu za juu sana, tunajua uchungu na tuna uchungu mkubwa sana na tumekuja humu ndani ili kusudi kuweza kukabana nao hawa wanaojiita wana cv na degree. CV zisitumike kwa ajili ya kuibia watu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, waendesha bodaboda wana viparata wanalipa shilingi 20,000. Ina maana vyote vinaingia huku Serikalini, halafu inapoonekana shilingi bilioni 150 amekula mtu mmoja, halafu anabaki tu ana- survive, yaani tuwe serious ili nchi yetu ilete mabadiliko makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana. Ahsante sana. (Makofi)