Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Mpango wa Tatu wa Bajti ya Taifa letu. Nijikite moja kwa moja katika sekta ya kilimo, ni Dhahiri kuwa sekta ya kilimo imekuwa ikichangia kwa asilimia kubwa katika pato la Taifa. Lakini kwa bahati mbaya bajeti ya sekta ya kilimo imekuwa haitekelezeki. Imekuwa kilimo kikipewa bajeti ndogo sana na kusababisha mambo mengi kukwama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na sekta hii kuchangia katika pato la Taifa letu wakulima wetu wamekuwa wakikutana na changamoto nyingi sana na kubwa katika suala zima la pembejeo za kilimo. Na changamoto hii inasababishwa na mlundikano mkubwa wa kodi uliopo kwa wafanyabiashara na umesbabisha wakulima wetu kuumia sana, lakini kwa kuwa ni jukumu letu sisi kama Waheshimiwa Wabunge, kuhakikisha tunaishauri Serikali ili tuweze kuzipitia sheria za kodi na kuzifanyia marekebisho. Tuna jukumu kubwa la kufanya maana sheria zilizopo zinawaumiza sana wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili pia liendane sambamba na kutafuta soko. Kumekuwa na changamoto kubwa ya masoko ya mazao, hususan katika Mkoa wa Songwe wananchi wetu wamekuwa wakijishughulisha sana na zao la kahawa, zao la mahindi, zao la mpunga na maharage na mambo mengine. Lakini kwa sasa ukienda Songwe mahindi gunia linauzwa kwa shilingi 30,000/= tu wakati huo mkulima nanunua mbolea kwa bei ya 65,000/= mpaka 70,000/= mbolea aina na DAP, kitu ambacho kinasababisha wakulima wetu kuumia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linawatesa sana wakulima wetu na kuwakatisha tamaa sana katika suala zima la kilimo. Kwa nini nasema tuangalie masoko? Asilimia kubwa wananchi wa Mkoa wa Songwe na Rukwa walikuwa wanategemea sana kuwauzia Wakongo mahindi na Wakenya, lakini leo hii biashara imekufa, Wakongo hawawezi kununua tena mahindi kwasababu, watu wa Afrika Kusini wameliteka soko la mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkulima wa Tanzania akibeba mahindi kwenda kuyapeleka Kongo kutoka Tanzania kwenda kufika Kongo ni kilometa zaidi ya 1,000 lakini mtu wa Afrika Kusini akitoka na mahindi kutoka Afrika Kusini kwenda kufika Kongo ni kilometa zaidi ya 2,000 lakini mtu wa Afrika Kusini anauza mahindi kwa kilo 250/= na Mtanzania anauza kwa 360/= lakini bado haimlipi. Jambo hili linawakatisha sana tamaa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna sababu ya kuweka uhusiano mzuri na mataifa ambayo yanatusaidia katika suala zima la soko, ili tuweze kuwanufaisha pia wakulima wetu na kutokuwakatisha tamaa. Lakini pia Serikali ituambie ni kwa namna gani kilimo ambacho ndicho uti wa mgongo wa Taifa letu kinaweza kuinua pato la Taifa. Ikiwa tu bajeti inayotengwa haitekelezeki kwa mwaka 2019/2020 utaona bajeti iliyotekelezeka ni asilimia 15 tu. Sasa tutawezaje kuinua wakulima kama bajeti tunayopanga ndani ya Bunge hili haiwezi kutekelezeka kabisa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo tuna haja kubwa ya kutunga sheria za kusimamia utekelezaji wa bajeti ambazo tunazipitisha ndani ya Bunge hili, ili ziweze kutekelezeka. Na kuwepo nidhamu katika kutekeleza bajeti ambazo tunakuwa tunazipitisha ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la umeme. Tumeendelea kuzungumzia suala la viwanda ndani ya Taifa letu. Ni dhahiri kabisa kwamba, viwanda asilimia kubwa vinategemea umeme. Lakini leo ukienda katika Mkoa wa Songwe limekuwa ni jambo la kawaida umeme kukatika siku mbili mpaka tatu bila sababu za msingi. Sasa hawa watu ambao tunataka wawekeze katika Taifa letu, wawekezaji wa ndani nan je tunawakatisha tamaa. Mtu hawezi kuweka kiwanda akitegemea kutegemea nguvu ya solar ama generator kuendesha kiwanda chake. Ni lazima ategemee umeme ili uweze kumsaidia kwenye kiwanda, sasa tusifike mahali kuwakatisha tamaa wawekezaji ambao wanakuja kuwekeza katika Taifa letu kwa njia ya umeme tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii umeme Mkoa wa Songwe umekuwa ni kawaida kukatikakatika, lakini ukikaa Dodoma hapa unaweza ukajisahau kwamba, Songwe na Dodoma ni nchi mbili tofauti, lakini kumbe mikoa yote iko ndani ya Taifa moja. Umeme Dodoma mimi sijawahi kushuhudia umeme ukiwa umekatika ndani ya Jiji la Dodoma, lakini Songwe ni kawaida umeme kukatika. Tunawahamasisha vijana wetu kujiwekeza, tunahamasisha vijana wetu kujiajiri, hivi leo kijana amejiajiri katika kazi anachomelea, wengine wana saluni, umeme unakatika siku mbili-tatu maisha yake atayaendeshaje kwa namna hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawakatisha tamaa pia vijana wetu. Tuombe suala la umeme pia lichukuliwe ili tuweze kuwatia moyo wawekezaji na vijana wetu ambao wameamua kujiajiri ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa mpango huu uendane na kuzipa nguvu halmashauri zetu ikiwa ni pamoja na kurejesha baadhi ya vyanzo ambavyo vimechukuliwa na Serikali kuu. Mfano chanzo cha property tax, chanzo hiki tuliona tu kwenye vyombo vya Habari kwamba, Waziri ametangaza kwamba, halmashauri watakusanya, lakini uhalisia ni kwamba, fedha hizo zitakusanywa na halmashauri na zitapelekwa Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pengine tuone tunaona kwamba, inaonekana Serikali Kuu tumekosa watu wa kutukusanyia tunataka halmashauri sasa itusaidie halafu mwisho wa siku fedha hizi zinakuja kwenye Serikali kuu. Tunaomba kama Serikali kuu imedhamiria kukirudisha chanzo hiki kwenye halmashauri, halmashauri wakusanye wao na fedha hizo ziingie katika mfuko wa halmashauri, jambo hili litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi sote tunajua kwa asilimia kubwa ukiangalia kwenye masuala ya barabara leo hii tunazungumzia mambo ya barabara ambazo zinaendeshwa na TARURA. Tumekuwa tukifeli sana kwasababu, aslimia kubwa TARURA wanategemea chanzo cha ndani cha halmashauri na halmashauri tumekuwa tukipata fedha kidogo kwasababu ya vyanzo vingi kuchukuliwa na Serikali kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuombe sasa kama itawezekana vyanzo ambavyo vinawezekanika halmashauri kukusanya turidishe mikononi mwa halmashauri na halmashauri iendelee kukusanya, ili iweze kujiendesha pia. Kwasababu, kuna wakati tunapata hata hati zisizoridhisha kwenye halmashauri zetu kwasababu ya miradi kuchelewa kutekelezeka yote ni kwasababu ya Serikali kuu kutopeleka fedha kwa wakati na kutopeleka fedha za kutosha kulingana na bajeti inavyokuwa imetengwa na halmashauri. Tuweze kuzipa miguu halmashauri, ili ziweze kutembea na ziepukane na kupata hati chafu na hati zisizoridhisha. Vyanzo vingi ambavyo halmashauri inaweza kuvirejesha tuweze kuvirudisha halmashauri iweze kukusanya. Nashukuru sana. (Makofi)