Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupewa fursa hii ya kuchangia Mpango huu. Nitajikita kwenye maeneo mawili; nitaongelea kilimo na uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mpango, umeongelea kwa kina suala zima la kilimo. Kama Wabunge wengi walivyochangia, kilimo ndiyo sekta pekee ambayo inaakisi uchumi jumuishi; inaajiri Watanzania zaidi ya asilimia 65. Kama Waheshimiwa Wabunge wengi walivyosema, kilimo hatujakipatia msukumo ambao kinastahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea zao moja. Kama Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma wanavyosema, kwa Mkoa wa Kagera zao la kahawa ni siasa, zao la kahawa ni elimu, zao la kahawa ni kila kitu. Miaka ya 1970 Mkoa wa Kagera ulibahatika kuwa na wasomi wengi kwa sababu ya zao hili la kahawa. Leo tunapoongea, Kagera zao la kahawa limekuwa kama laana. Bei imeshuka na wanapouza hata bei kama ni ndogo, bado kupata hela zao inawachukua zaidi ya miezi mitatu kama dada yangu Mheshimiwa Conchesta alivyosema pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la kahawa kwa Mkoa wa Kagera linahusisha kaya nyingi kama ilivyo kwa Taifa zima. Nilikuwa naangalia takwimu hapa. Zaidi ya 90 percent ya kahawa inazalishwa na wakulima wadogo wadogo. Hawa wakulima wadogo wadogo ndio wazazi wetu, kaka zetu, wadogo zetu, ambao wanahangaika usiku na mchana kuhakikisha kwamba wanapata pesa ya kusomesha watoto wao, kutunza familia zao na kuhakikisha kwamba wazazi wao wanaendelea kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo liko wapi? Naishukuru Serikali, kwa miaka mitano iliyopita walifuta tozo karibia 20 kwa zao la kahawa, tunawashukuru kwa hilo, lakini walipofuta hizi tozo, hatujatafuta suluhisho la bei na mauzo ya zao la kahawa, tumeviachia vyama vya msingi vinunue kahawa kutoka kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna sekta binafsi, tunaihusishaje kuhakikisha kwamba na wao wananunua kahawa kwa Mkoa wa Kagera ili kuleta ushindani? Tumeviachia vyama vya msingi peke yao, vinafanya kazi vinavyotaka vyenyewe, vinalipa wakati vinapotaka vyenyewe. Hata hivyo, kuna wazawa wa Tanzania ambao wamewekeza kwenye viwanda vya kusindika kahawa, tunawaambia hao kama unataka kununua kahawa, kanunue kwenye vyama vya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri atuambie, tunaoanishaje kilimo na Sekta ya Viwanda? Unapowaambia wanunue kwa vyama vya msingi, watanunua kwa bei ya juu kuliko wangekwenda moja kwa moja kununua kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna maneno hapa yanasemwa, eti watakwenda kuwalangua wakulima. Ndiyo! Wakalangue kule, lakini Serikali ihakikishe kwamba inaweka mazingira sahihi na mazingira huru kuhakikisha kwamba vyama vya msingi vinanunua na wafanyabiashara wananunua bila kuwaathiri wakulima wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mpango namshukuru Waziri, amesema tunakwenda kujenga uchumi shirikishi na uchumi shindani. Tunayo Sheria ya Ushindani hapa nchini, tuweke mazingira huko kwenye vijiji vyetu kuhakikisha kwamba hata huyu; vyama vya msingi na vyama vya ushirika vishindanishwe na wakulima na wanunuzi binafsi ili kuleta uwiano na ushindani kwenye masoko yetu. Tusimlinde huyu. Mnajua madhara ya uchumi hodhi? Mnajua matatizo ya protectionism? Tumevilinda kwa muda mrefu vyama vya ushirika na vyama vya msingi na tunajua matatizo yake kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaporuhusu ushindani, tunakaribisha ubunifu, tunakaribisha teknolojia na tunakaribisha wakulima wapate a fair deal kwa mazao yao wanayoyalima huko kwenye majimbo yetu. Nawaomba ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tushirikiane kuhakikisha kwamba baadhi ya sheria na Mashirika ambayo hayatuongezei ufanisi kwenye maeneo yetu tunakotoka, aidha, sheria zao wazilete hapa tuzipitie upya kuona kama zinatuongezea ufanisi au tufute. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi nilikuwa nasoma kitabu kimoja wachumi wanakifahamu vizuri sana, “Why Nations Fail? The Origins of Power, Prosperity and Poverty.” Mwandishi anatuambia na kutushauri, kama tuna mashirika ambayo hayana ufanisi, tunakaribisha umasikini kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, nishauri kwenye hili, Wizara kwa kushirikiana na sekta binafsi tuhakikishe suala la zao la kahawa Mkoa wa Kagera lipatiwe ufumbuzi wa haraka, watu wapate bei nzuri na sekta binafsi ihusishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo, tatizo tulilonalo kwenye hili zao lenyewe la kahawa kutoroshwa kuuzwa nchi za nje litakwisha. Pia, tutakuwa tumeboresha Sekta ya Viwanda; kwenye jimbo langu tunavyo viwanda viwili vinasindika mazao ya kahawa, lakini wanalazimika kununua tu kwenye vyama vya msingi kwa bei ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni uvuvi. Tunalo Ziwa Victoria ambalo linazalisha, lakini ukiangalia takwimu za uvuvi na faida tunayoipata kutoka katika ziwa hili ni aibu. Sisi kama Tanzania, niliwahi kulisema hapa mwezi wa Pili. Tunamiliki eneo kubwa zaidi ya kilomita za mraba 35,000 ambazo ni sawa sawa na asilimia 51 na wenzetu asilimia 43; lakini ukiangalia tunachokipata na tunachokiuza nje, hakuna uwiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hapa nilikuwa nasoma ripoti moja, tumeambiwa sisi tunauza nje kwa asilimia 51 ukilinganisha na majirani. Kwa uchumi wetu tunachangia only two percent ya GDP, Uganda 3%, Kenya 2% na wenyewe. Ukiangalia viwanda ambavyo vimejengwa, Uganda wanaongoza, wana viwanda zaidi ya 20; sisi ambao tuna asilimia 51 tuna viwanda vinane tu na Kenya wana viwanda vitano. Tunaambiwa viwanda vinazidi kuporomoka kwa upande wetu na vinazidi kuongezeka Kenya na Uganda wenye eneo dogo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tunafanya hayo na sisi tuko hapa? Kazi kubwa tunayopaswa kuifanya kama tunataka kuchochea uchumi, ni kuhakikisha tunavuna hizi fursa ili wananchi wetu waweze kuchangamkia uchumi wetu. Hata mazao tunayoyapata kutokana na uvuvi ili yasafirishwe kupelekwa kwenye masoko ya nje, yanapitishwa Uganda na Kenya; Entebe na Jomo Kenyatta International Airport. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka ya nyuma tulifanya maamuzi mabaya, tuliweka a five percent surcharge kwa total consignment ya minofu ya samaki kutoka Mwanza. Ilifikia mashirika yote ya ndege yakakimbia. Mpaka leo ili tusafirishe minofu ya Samaki, lazima twende Entebe au Jomo Kenyatta International Airport. Kwa nini, Mheshimiwa Naibu Waziri? Ukiangalia chanzo chake ni tozo tulizojiwekea sisi wenyewe na tulizipitisha hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naongea tu, mabondo; ili usafirishe mabondo tuna tozo ya shilingi 7,500/= kwa upande wa Tanzania; Uganda ni shilingi 436/= na Kenya ni shilingi 34/=. Ukipitia tozo zote kwa upande wa samaki na mazao ya uvuvi, sisi tuna tozo ambazo hazibebeki na hazihimiliki na matokeo yake tunapoteza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nitachangia zaidi kwenye sekta.

Mheshmiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)