Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushuru kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa. Vile vile namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na uzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile ni mara yangu ya kwanza kuchangia, naomba nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi ya kugombea katika Jimbo la Meatu. Kubwa pia, nawashukuru wananchi wa Jimbo la Meatu kwa kunichagua kuwa mwakilishi wao, nami nawaahidi sitawaangusha na ninamwomba Mwenyezi Mungu anisaidie. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hebu subiri kidogo Mheshimiwa. Subiri subiri, nimezima microphones zote, kwa sababu sielewi kelele inatoka wapi. Hebu hamia kwenye mic ya jirani halafu ujaribu kuisimamisha. Zima kwanza hapo ulipotoka.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utajikita katika moja ya maeneo makuu matano ya kipaumbele ambayo ni kuchochea maendeleo ya watu. Eneo hili linajumuisha utekelezaji wa miradi ambayo inajikita katika kuboresha maisha ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika mpango wa pili kumekuwepo na mafanikio makubwa katika Sekta ya Afya. Tumeona miundombinu katika Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali zikijengwa, vilevile na upatikanaji wa dawa, ongezeko la watumishi pamoja na vitendea kazi. Hata hivyo, sekta hii bado inakabiliwa na changamoto nyingi. Kwa hiyo, naomba katika Mpango huu wa Tatu changamoto hizi zitatuliwe ili tuweze kufikia malengo ya mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ikamilishe sasa maboma ya Zahanati na Vituo vya Afya ili yaweze kufanya kazi kama ilivyokusudiwa. Vile vile kukamilishwa kwa maboma haya kuende sambamba na upatikanaji wa vitendea kazi, watumishi wa kutosha na dawa za kutosha. Ni ukweli usiopingika kwamba Zahanati zetu nyingi hazina watumishi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ziara zangu, nimeshuhudia, baada ya mtumishi kustaafu Zahanati inafungwa. Mojawapo ni Zahanati ya Mwabalebi. Pia katika Zahanati ya Mwabagalu kuna watumishi wawili ambao mmoja amekwenda maternity, mmoja ni mgonjwa, Zahanati imefungwa. Kwa hiyo, naiomba Serikali iweke mkazo katika kuajiri wataalamu wa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Serikali itoe fedha za kutosha ambazo zitapaswa kutolewa katika chombo chetu cha MSD ili kiweze kusambaza dawa za kutosha nchini. Ni ukweli usiopingika, katika Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa Serikali imeongeza Bajeti kubwa ya madawa kutoka shilingi bilioni 29 mpaka shilingi milioni 250. Madawa katika hospitali zetu yaliongezeka mpaka upatikanaji wa dawa muhimu ulifikia asilimia 80 mpaka 90. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ninavyoongea, ukienda kwenye hospitali zetu, hakuna dawa. Wananchi wanaandikiwa dawa na kuhitajika kwenda kununua dawa katika maduka ya dawa. Naiomba Serikali niweke mkazo katika mauzo ya dawa. Tutategemea bajeti zitaongezwa, lakini Serikali ikiacha tu kutoa fedha, hospitali zile zinakosa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano tu. Robo tatu zilizopita za basket fund haikuweza kuletwa katika hospitali zetu. Kwa hiyo, ilisababisha ukosefu wa dawa katika hospitali zetu. Kwa hiyo, Serikali ikiweka mkazo katika mauzo ya dawa, itasaidia kuwa na mzunguko, kutakuwa na revolving. Hata hivyo, wataalam wetu wamekuwa na kisingizio kwamba madawa haya yanamalizwa na wagonjwa ambao wako kwenye makundi ya msamaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, naishauri Serikali, ijue ni asilimia ngapi itakwenda kwenye makundi ya msamaha, ni asilimia ngapi itakuwa ni ya mzunguko na hiyo isimamiwe. Hata kama Serikali ikichelewa kupeleka fedha za ruzuku, hospitali hizo kuwe na mzunguko wa kutosha na madawa yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sekta ya Elimu kumekua na mafanikio makubwa. Tumeona ongezeko la wanafunzi kutokana na Elimu Bila Malipo na miundombinu mingi imejengwa. Hata hivyo, sekta hii bado ina changamoto nyingi katika miundombinu ya kujifunzia na ya kufundishia. Kwa hiyo, kwanza naiomba Serikali itoe fedha iweze kukamilisha maboma ya maabara katika Shule zetu za Sekondari, itoe fedha za kutosha kukamilisha maboma ya vyumba vya madarasa pamoja na nyumba za watumishi. Pia udahili wa wanafunzi uendane na ongezeko la vyumba vya madarasa pamoja na nyumba za watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri za vijijini, nimeshuhudia kuwepo kwa tatizo kubwa la walimu wengi kuhama. Hivyo Serikali inapaswa ifuatilie kujua ni nini kinachosababisha walimu hawa wanahama kwa wingi? Kwa mfano, katika Halmshauri ninayotoka ya Meatu, katika robo moja walihama walimu 60.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili linachangiwa na ukosefu wa nyumba za walimu. Kwa mfano, katika jimbo langu, Shule ya Mabambasi miaka mitatu iliyopita ilikuwa ya mwisho kitaifa. Ukifika pale, walimu wote sita wanaishi katika nyumba moja; na shule hiyo ni kilomita 30 mpaka Makao Makuu ya Wilaya. Kwa hiyo, familia zao inabidi ziishi Wilayani na wenyewe mwisho wa wiki inabidi waende kwenye familia zao. Kwa hiyo, kunakuwa na gharama kubwa za nenda rudi nenda rudi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule moja ya Mwanyagula yenyewe ina nyumba moja ambayo sasa inavuja na yule mwalimu amehamia Wilayani. Kwa hiyo, ukifika pale, hakuna mwalimu anayeishi shuleni, inabidi walimu wasafiri kila siku kilomita 20 kwenda na kurudi na hivyo kunakuwa na gharama kubwa ya kimaisha. Naomba Serikali iwekeze zaidi katika miundombinu ya nyumba za watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tatizo la miundombinu ya barabara inachangia walimu kuhama kutokana na gharama kubwa ya usafiri, huduma ya maji nayo ni tatizo na umeme nao ni tatizo. Endepo Serikali itasawazisha haya, ninaamini walimu wengi hawatapenda kuomba uhamisho kwenda kwenye maeneo ambayo yana huduma kama ambazo nimezitaja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sekta ya Maji, Serikali katika mpango wake imeeleza kwamba kwa ujumla miradi yote iliyotekelezwa imewezesha wananchi zaidi ya milioni 25 kupata huduma za maji, hivyo kupata wastani wa upatikanaji wa maji vijijini asilimia 70 na mjini asilimia 84 hadi mwaka 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyoiona Serikali, haipo serious na changamoto na upungufu wa maji. Katika takwimu hizo walizozitoa, ukiangalia wanananchi wanaopata milioni 25, na Watanzania tuko takribani milioni 50, kwa hiyo, ni dhahiri kwamba asilimia 50 tu ya wananchi ndio wanaopata maji. Kwa hiyo, takwimu hizi za asilimia 70 kwa 84 haziakisi uhalisia wa upatikanaji wa maji katika maeneo yetu. Ni vyema sasa Serikali ikatafuta nini chimbuko kubwa la ukosefu wa maji ili ije na suluhu, iweke mkakati maalum wa upatikanaji wa maji hadi tutakapokuwa tunamaliza Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)