Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa katika kuhakikisha kwamba Serikali yetu inaendelea kufanya kazi za maendeleo na kuendelea kukuza uchumi kwa Taifa letu lakini kuendelea kukuza ajira na kuboresha maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa pole kwa Watanzania kwa msiba mzito ambao umetupata pamoja na Waheshimiwa Wabunge nawapa pole sana kwa sababu tulizoea kufanya kazi na ndugu yetu Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Tumeona namna ambavyo ameweza kusimamia na kuendesha Serikali yetu kwa kipindi cha miaka mitano na ameweza kusimamia maendeleo makubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumpongeza Mama yetu Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu kwa uteuzi wake. Nina hakika kwamba ana uwezo mkubwa wa kusimamia Taifa letu na kuendesha yale mazuri yote ambayo alianza kufanya kazi na Mheshimiwa ndugu yetu Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba naanza kwa kuunga mkono hoja. Ukiangalia Mpango wetu hata ukiangalia mipango yote iliyopita tumeona kwamba kuna hoja ya Miradi ya Magadi Soda Engaruka, Mchuchuma na Liganga na LNG. Miradi hii mikubwa kila mwaka tunaiona ipo katika Mpango wetu wa Maendeleo wa Taifa lakini naona kwamba Serikali haijawa tayari kusimamia miradi hii kuhakikisha kwamba tunakwenda sasa kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Mradi wa Mchuchuma na Liganga soko la makaa ya mawe yapo ndani ya nchi na nje ya nchi lakini Serikali hatujakuwa tayari kuwekeza ili kuhakikisha kwamba uzalishaji huu unaendelea kuleta tija na manufaa kwa Taifa letu. Kwa hiyo, naiomba Serikali kusimamia ili kuhakikisha kwamba mradi huu unakwenda vizuri na unaleta tija na unaongeza mapato kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna Mradi huu wa LNG, kwanza niishukuru Serikali kwa hatua ambayo imefikia kuhakikisha kwamba imetoa fedha ya kulipa fidia kwa wanaopisha mradi pale Lindi katika eneo la Likongo. Hata hivyo, naiomba Serikali kuharakisha mradi huu ili sasa utekelezaji uweze kuanza na kuhakikisha kwamba tunakwenda nao vizuri kwa sababu mradi huu utatuletea manufaa makubwa na utaingiza mapato makubwa katika Taifa letu. Si kwamba tutakaofaidika ni wana Lindi lakini Tanzania nzima tutafaidika na mradi huu wa LNG. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali sasa kuharakisha mazungumzo ya mwisho yaliyobaki kuhakikisha kwamba sasa mradi huu tunakwenda katika utekelezaji. Nina hakika kwamba Mama yetu Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu atausimamia vizuri kuhakikisha kwamba tunakwenda kwenye utekelezaji. Pia naomba wafidiwa waliobaki kulipwa fidia zao basi Serikali iharakishe kutoa malipo ili wananchi wale tuweze kuwaondoa na waweze kupisha mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la afya. Katika Sera ya Afya tumeweza kutekeleza vizuri na Mpango wa Taifa wa Pili uliwekeza sana katika kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya, zahanati, hospitali za wilaya na hospitali za rufaa. Tunaishukuru sana Serikali kwa kusimamia Mpango huo vizuri. Changamoto kubwa iliyopo na naomba Mpango huu wa Tatu uweze kusimamia ni kuhakikisha kwamba vituo vya afya vilivyojengwa vinakamilishwa kwa kuweka vifaa tiba na kuongeza wauguzi na waganga ili wananchi waendelee kupata huduma kama ambavyo tulivyotarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano iliwekeza katika kuboresha sekta ya elimu na ilitumia trilioni 3.15. Ilifanya kazi kubwa katika kuhakikisha kwamba imewekeza katika sekta ya elimu. Naomba Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa kwa maono ya Mheshimiwa aliyekuwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wa kujenga Shule ya Sekondari ya Wasichana kila Mkoa kwa mchepuo wa sayansi uzingatie kuhakikisha kwamba tunakwenda kuendeleza maono haya ili watoto wetu wa kike waendelee kupata elimu ya masomo ya sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunazo shule kongwe, najua mpango wa Serikali wa kujenga na kukarabati shule kongwe unaendelea kwa shule za sekondari pamoja na vyuo lakini bado hatujaangalia katika shule zetu za msingi. Kuna shule za msingi ambazo ni chakavu mno, ukiangalia kwa macho hazipendezi na hazikaliki madarasani na hazipo rafiki kabisa wanafunzi kukaa madarasani. Kwa hiyo, naomba Serikali sasa kupitia Mpango huu wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa uziangalie zile shule za msingi kongwe ziendelee kuingizwa katika Mpango maalum na Serikali iweze kuzikarabati ili tuwe na shule bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia sera ya barabara, tunazo barabara kuu za kiuchumi zinazounganisha mkoa na bandari lakini zinazounganisha bandari na nchi Jirani. Tuna barabara inayotoka Dar es Salaam – Pwani - Lindi – Mtwara; tuna barabara inayotoka Dar es Salaam – Morogoro - Dodoma - Mwanza, lakini tuna barabara zinazokwenda nchi za jirani maana yake zinaunganisha uchumi wa nchi yetu na uchumi wa nchi Jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara zetu zimekuwa dhaifu sana hata kama tunazikarabati utakuta barabara imekarabatiwa imetumika miezi sita tu tayari imeingia kwenye uchakavu. Kwa hiyo, Serikali yetu inaendelea kutumia fedha nyingi kukarabati kila mara barabara hizi lakini bado zinaonekana zipo chini ya kiwango. Kwa hiyo, naiomba Serikali sasa kuhakikisha kwamba sera yake inakuwa wazi namna bora ya kuzikarabati na kuzijenga barabara hizi kwenye kiwango cha hali ya juu ili ziendelee kutumika katika kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la TARURA. TARURA wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana lakini ukiangalia hata ofisi hawana, baadhi ya maeneo ofisi za TARURA hazipo tunatumia majengo ya kukodi lakini majengo yenyewe ni madogo hayana nafasi kubwa, pia bado hawana vifaa na magari na kuna upungufu mkubwa wa watumishi. Kwa hiyo, naomba sasa Serikali kuangalia namna bora ya kuwaboresha hawa ndugu zetu TARURA ili tuende nao vizuri na waweze kufanya kazi zao vizuri na sisi tuweze kufaidika na TARURA katika kuhakikisha kwamba wanaendelea kufanya kazi katika mazingira rafiki na tunategemea kwamba waweze kusimamia barabara zetu za kule kwenye Halmashauri zetu ziweze kuboreka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie Mpango wa Tatu wa Taifa katika uwekezaji wa uchumi wa bahari. Nimeona kwamba sasa tunakwenda kuwekeza katika sekta hii ya uvuvi na kuhakikisha kwamba Serikali yetu sasa inaingia katika uwekezaji huu wa bahari. Ni jambo jema sana lakini nafahamu kwamba sekta hii ya uvuvi inatoa ajira za kudumu zaidi ya laki mbili, lakini inatoa ajira za muda mfupi zaidi ya milioni 4. Kwa hiyo, ni jambo jema sasa kuingia katika uwekezaji huu na sisi tutaendelea kufaidika na Serikali yetu itaendelea kuingiza mapato ya kutosha. Nashauri tu tuwekeze katika rasilimali watu kwa kuhakikisha kwamba tunakuwa na wataalamu wenye ujuzi mkubwa wa kusimamia sekta hii ya uwekezaji huu wa uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wa Tatu wa Taifa pia umeonesha namna bora ya kusaidia ndugu zetu wa SIDO. SIDO wanafanyakazi nzuri sana na tukiwatumia ndugu zetu wa SIDO…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili Mheshimiwa.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, tuwekeze kuwasaidia na kuwapa nguvu ndugu zetu wa SIDO ili watusaidie kutoa elimu ya mafunzo stadi lakini tutakuwa na uwekezaji mkubwa wa viwanda vidogo vidogo kwa sababu wao wanasimamia shughuli hizi. Kwa hiyo, naomba tuwaunge mkono ndugu zetu wa SIDO ili kuharakisha maendeleo ya wajasiriamali wadogo wadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)